Menu

Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. 2 Huyo mwanzo

Wednesday, July 8, 2015

AMRI MPYA TOKA KWA BWANA YESU - NAWAACHIA AMRI MPYA PENDANENI



KUMPENDA JIRANI YAKO

Somo: Luka 10

Katika somo hili tutaangalia zaidi maagizo ya Yesu kuwa, kama kweli tunataka tuwe wafuasi wake, ni lazima tuoneshe katika maisha yetu kiwango kisicho cha kawaida cha upendo kwa watu wengine. Mahali pa kuanzia pa somo hili ni mfano wa Msamaria-mwema uliotajwa katika somo letu lililopita. Tunapoangalia kwa ukaribu maneno ya Yesu katika Luka 10:30-37, tunaona mambo kadhaa ya muhimu.        

Kwanza, Yesu alichagua kumweka Msamaria katika mfano huo, kwa kuwa Wasamaria walikuwa wakichukiwa na Wayahudi; walikuwa wakionekana kama watu wa kudharaulika.

Pili, mtu aliyeshambuliwa na wanyanganyi, hakusaidiwa ni watu wawili waliokuwa wakistahili kwanza kumhurumia na kumsaidia. Makuhani waliokuwa wakitokana na kabila la Lawi, walikuwa wakiwajibika katika Sheria ya Musa kuangalia afya na huduma kwa ujumla za Wana wa Israeli, lakini hakuna kilichofanyika.

Ni Msamaria aliyeonesha upendo na huruma, kwa kufanya mambo aliyofanya kusaidia. Alimwosha majeraha, akambeba mtu huyu aliyeumizwa kwenye punda wake na kumweka mahali pa usalama kupumzika. Mwishoni, ndiye aliyeweka mpango wa msaada zaidi kwa ajili ya kuendelea kuhudumiwa.

Tunaposoma katika Injili juu ya matendo mengi ya uponyaji yaliyofanywa na Yesu, waandishi mara nyingi wanaongezea maneno, Yesu: ‘Alimwonea huruma’. Mfano upo katika Luka 7:11-15.

Yesu alipokuwa amewateua wanafunzi wake wa karibu kumi-na-wawili, alianza kuwafundisha juu ya upendo, msamaha na huruma. Kama ukifungua sasa nyuma kwenye Luka 6:17 utaona hayo kwa pamoja. Umati uliomsikiliza Yesu siku hiyo ulikuwa mkubwa sana, na wengi walikuwa wamekuja kutoka mbali sana kumwona. Walio wengi walikuja ama kuponywa, ama kuona matendo ya Yesu ya kuponya. Walikaa hapo muda wote kusikia mafundisho yake kuhusu ufuasi wa Kikristo, na tutafanya na sisi hilo, tukitazama zaidi mstari ya 27 mpaka na 36.

Hakuna hasa linaloshangaza; tunalosoma katika Injili ya Luka ni kama lile lile tulilolisoma katika Injili ya Mathayo, katika somo letu lililopita. Ujumbe huu ni wa maana mno kiasi kwamba unarudiwa mara nyingi katika Biblia. Kile kinachoanza kama wazo katika akili zetu, mara nyingi kinageuka kuwa tendo, kwa hiyo sheria ya Yesu inahitajika kwanza iongoze katika kufikiri kwetu, ndipo hatimaye inapoweza kutawala matendo yetu. Tunapoonesha upendo wa huruma kwa mtu mwingine, tunafanya hivyo kwa matendo yetu.

Muda mfupi kabla Yesu hajaondoka katika kile Chumba cha Juu, alipofurahia mlo wa pamoja na wanafunzi wake kabla ya kufa, uliirudia tena hii amri ya muhimu kipekee kuhusu upendo. Tunaiona katika Injili ya Yohana 13:34, 35.

Maneno yake yanahitaji kuzingatiwa kwa umakini kwa kuwa, upendo wa Kikristo unaooneshwa na wanafunzi wake, unatakiwa uwe mkubwa kama ule uliooneshwa na Kristo mwenyewe kwa hao wanaume na wanawake wa enzi yake, na wale wote ambao wangefuata katika nyakati zote.

Alionesha upendo wake kwa kujitoa kwa hiari kufa msalabani, ili wote wanaomfuata, wanaoonesha imani ya kweli, waweze kupata fursa ya kuwa na uzima usio na mwisho katika Ufalme wake katika dunia hii. Hebu angalia Yohana 15:9-14 na uone vile amri hii inavyorudiwa katika mstari wa 12 na wa 17.

Petro alipojitetea kuwa kamwe hatamwacha Yesu (Yohana 13:36-38), Yesu alimwambia, kabla jongoo hajawika (yaani kabla hakujakucha), angemkana Bwana wake Yesu mara tatu. Lilipotokea hivyo kama Yesu alivyotabiri, Petro alitahayari, lakini alijifunza somo kuwa, kumpenda Bwana Yesu hakuwi kitu kirahisi mtu anapobanwa.

Baada ya Yesu kufufuka, aliwakuta wanafunzi wake upande wa kaskazini katika Galilaya, mahali ambapo saba kati yao walikuwa wameamua kuchukua mashua na kwenda kuvua. Walijiunga na Yesu ufukweni mahali ambapo alikuwa ameandaa chakula cha mkate na samaki (Yoh. 21:9). Ni jambo la muhimu kuwa, Yesu alikuwa amewaonesha huruma yake umati ule wa watu elfu tano na baadaye elfu nne kwa kuwalisha kwa muujiza mikate na samaki.

Baada ya kula hapo ufuweni mwa Bahari ya Galilaya, Yesu alilihitimisha somo lake la upendo kwa kumuuliza Petro mara tatu juu ya upendo wake kwa Bwana wake. Yesu aliendelea kwa kuongeza maneno mengine kwenye maelekezo yake ya awali (ms. 15-18). Ilikuwa kwamba, kila mara Petro aliposema kuwa alimpenda Yesu, alipewa amri na majukumu ya: kulisha wana-kondoo, kuchunga kondoo, kulisha kondoo wa Yesu.

Katika miaka ya awali ya kanisa jipya (Ukristo), kulikuwa na wana-kondoo wengi (wafuasi wapya) wa kutunzwa. Eklesia nyingi zilipoanzishwa katika maeneo mengi ya Israeli na nchi zingine, majukumu yalibadilika kukawa na haja ya ulezi kwa jumuia zilizokuwa zimeanza (kondoo). Paulo aliitumia lugha hii hii katika ujumbe wake alipokuwa akiwaaga wazee katika eklesia ya Efeso (Matendo 20:28, 29).

Mtume Yohana naye alijifunza somo hili la muhimu sana la upendo kutoka kwa Yesu. Alipokuwa akining’inia msalabani, Yesu alisema na Yohana na kumpa jukumu juu ya mama yake, Mariamu (Yohana 19:26, 27).

Miaka kama 50 baadaye Yohana aliandika Waraka aliokusudia usomwe katika Eklesia zote. Katika huo alieleza kwa kifupi sheria ya upendo wa Kikristo (1 Yohana 4:7-21). Soma mistari hii kwa makini maana ni ya muhimu sana, na hasa katika nchi ambazo kuna chuki za kutisha kati ya kundi moja la kijamii na kundi lingine, wazimu wa kuangamizana kati ya kabila moja na jingine, vita kati ya eneo moja na jingine, mji na mji, kijiji na kijiji, chuki kati ya familia na familia, ndugu na ndugu.

Maneno ya Yohana ni thabiti na hayaachi shaka lolote katika mawazo yetu. Haiwezekani kwa mfuasi wa Kristo kusema kuwa anampenda Mungu, na wakati huo huo akawa na chuki kwa Wakristo wenzake moyoni mwake. Kama mtu anasema anampenda Mungu na anamchukia ndugu yake, ni mwongo. Hakuna namna ya kuweza kuyakwepa maneno haya, na kwa wale wanaotaka kubatizwa au wale waliobatizwa hivi karibuni, hili ni fundisho la muhimu sana.

Kuna mambo mengi sana ya sisi kukumbuka kutoka kwenye maneno hayo kiasi kwamba, ningependa nitumie sehemu iliyobaki ya somo hili kuyaangalia kwa undani:
Mstari wa 7: “Pendo latoka kwa Mungu” – hili lina maana kuwa katika uumbaji, uwezo wa kuonesha upendo wa kujitoa ulijengwa ndani yetu kwa namna Mungu alivyotuumba. Anatutaka tuuitikie upendo wake na upendo wa Yesu kwetu.
Mstari wa 10: Mungu alimtuma Yesu awe dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu. Hiki ni kipimo cha upendo wake kwetu.
Mstari wa 11: Kwa kuwa Mungu anatupenda, ni lazima tuoneshe upendo kwa wengine.
Mstari wa 12: Tunapouonesha huu upendo unaotoka kwa Mungu kwa watu wengine, kuna kitu kinachomhusu Mungu ndani ya kila mmoja wetu.
Mstari wa 17: Kama ni kweli kwamba tunajisikia kuwa tumeweza kuonesha upendo huo wa Mungu kwa wengine, basi hatuhitaji kuwa na hofu ya hukumu siku ya kurudi kwa Yesu.
Mstari wa 10: “Pendo lililo kamili huitupa nje hofu”. Kuna faida ya uhakika kwa wale wanaoweza kuuonesha upendo wa namna hii.
Mstari wa 20 na 21. Hii ni mistari ambayo tumekwisha itazama lakini kwa sababu ya kukua kwa chuki na mauaji kati ya watu katika nchi nyingi za dunia, nataka hasa nisisitize umuhimu wa ujumbe huu.

Hatuwezi kumpenda Mungu na kumchukia kaka au dada yetu. Kwanza Yohana hapa anaongea na wafuasi wa Yesu; watu waliobatizwa. Hakuna kabisa sababu ya kuwa na uadui kati yetu tunapokuwa tumebatizwa.

Kama ambavyo ‘jirani’ wa mtu katika mfano wa Yesu alivyokuwa Msamaria, ndivyo ambavyo jirani yetu anavyoweza kuwa mtu yeyote anayehitaji msaada wetu. Kwa maana pana, majirani wanaweza kuwa watu tunaokutana nao kila siku, kwa hiyo tunalo jukumu lililo kubwa. Kwa bahati hatuhitaji kujihusisha na watu walio wengi tunaopishana nao kila siku, lakini, inapotokea, amri ya Yesu ni lazima tuikumbuke: mpende Mungu na jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.                                

No comments:

Post a Comment