Vichwa vya Habari

SHERIA YA MWENYE HAKI

“Sheria ya Mwenye Hekima”—Ni Chemchemi yaUzima
“LO KINA cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia!” akasema mtume Paulo. (Waroma 11:33) Naye Ayubu mzee wa ukoo mwaminifu alisema: “Yeye [Yehova Mungu] ni mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Naam, Muumba wa mbingu na dunia ana hekima isiyo na kifani. Tunaweza kusema nini kuhusu sheria, au Neno lililoandikwa la Muumba kama huyo?
Mtunga-zaburi aliimba: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya BWANA ni safi, huyatia macho nuru.” (Zaburi 19:7, 8) Bila shaka, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alielewa ukweli wa maneno hayo. Alisema: “Sheria ya mwenye hekima ni chemchemi ya uzima, kuepuka mitego ya mauti.” (Mithali 13:14Zaire SwahiliBible) Katika mistari 13 inayotangulia ya Mithali sura ya 13, Sulemani alionyesha jinsi shauri linalopatikana katika Neno la Mungu linavyoweza kutusaidia kuboresha maisha yetu na kuepuka kuyahatarisha.
Uwe Mwenye Kufundishika
“Mwana ni mwenye hekima palipo na nidhamu ya baba, lakini mtu mwenye dhihaka niyule ambaye hajasikia kemeo,” linasema andiko la Mithali 13:1NW. Nidhamu ya baba inaweza kuwa ya upole au kali. Kwanza inaweza kutolewa kwa njia ya mashauri, na yakipuuzwa, basi adhabu inatolewa. Mwana mwenye hekima hukubali nidhamu ya baba yake.
Biblia inasema, ‘yeye ambaye Yehova ampenda humtia nidhamu, naye humpiga mijeledi kila mtu ambaye yeye ampokea kuwa mwana.’ (Waebrania 12:6) Mojawapo ya njia ambazo Baba yetu wa mbinguni hutumia kututia nidhamu ni Biblia, Neno lake lililoandikwa. Kwa kweli, Biblia hututia nidhamu tunapoisoma kwa heshima na kufuata yale tunayojifunza. Sisi hunufaika kwa kufanya hivyo, kwa kuwa yote ambayo Yehova husema ni kwa faida yetu.—Isaya 48:17.
Nidhamu inaweza kutolewa kupitia rekebisho la mwamini mwenzetu anayetaka hali yetu ya kiroho iwe nzuri. Tunapaswa kuona shauri lolote lifaalo ambalo linatolewa kupatana na Neno la Mungu kuwa linatoka kwa Mungu aliye Chanzo kikuu cha kweli bali si kutoka kwa mtu anayelitoa. Tunakuwa wenye hekima tunapokubali shauri hilo kuwa linatoka kwa Yehova. Tunapofanya hivyo na kukubali lirekebishe mawazo yetu, liboreshe uelewevu wetu wa Maandiko, na kurekebisha mwenendo wetu, tunafaidika na nidhamu hiyo. Tunapaswa kuwa na maoni hayohayo kuhusu shauri tunalopata katika mikutano ya Kikristo na vichapo vinavyotegemea Biblia. Kufuata mashauri tunayosoma au kusikia ni njia nzuri ya kujitia nidhamu.
Kwa upande mwingine, mtu mwenye dhihaka hakubali nidhamu. “Yeye hafundishiki kwa sababu anafikiri anajua sana,” kinasema kitabu kimoja cha kitaalamu. Hata hakubali kemeo, yaani, nidhamu iliyo kali zaidi. Lakini je, anaweza kuthibitisha kwamba nidhamu ya Baba ina makosa? Yehova hajawahi kukosea kamwe wala hatakosea kamwe. Kwa kukataa nidhamu mtu mwenye dhihaka hufanya adhihakiwe. Kwa kutumia maneno machache yaliyochaguliwa vema, Sulemani anaonyesha kwa ustadi manufaa ya kuwa mwenye kufundishika.
Linda Ulimi Wako!
Mfalme wa Israeli analinganisha kinywa na mti unaozaa matunda ili kuonyesha umuhimu wa kuongozwa na Neno la Mungu katika usemi wetu. Anasema:“Mtu mwema hupata memakutokana na maneno yake, lakini wadanganyifu huishi kwa ukatili.” (Mithali 13:2) Matunda ya kinywa ni maneno naye mtu huvuna alichopanda kwa maneno yake. Msomi mmoja anasema: “Ikiwa mtu anatumia maneno yake kwa fadhili na kwa kusudi la kuwa na uhusiano wa kirafiki pamoja na majirani wake, atakula mema na kuishi kwa furaha na amani.” Lakini mambo yanakuwa tofauti kwa mtu mdanganyifu. Yeye anapenda kutenda jeuri na kuwadhuru wengine. Hupanga jeuri na kuvuna jeuri, nayo mitego ya mauti inamkaribia.
Sulemani anaendelea kusema: “Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; baliafunuaye midomo yake atapata uharibifu.” (Mithali 13:3) Usemi wa upumbavu unaweza kuharibu sifa, kuumiza hisia, kuharibu uhusiano, na hata kuleta madhara ya kimwili. Kuongea bila kujizuia kunaweza kumkosesha mtu kibali cha Mungu, kwa sababu kila mtu atamtolea Mungu hesabu kwa maneno yake. (Mathayo 12:36, 37) Kwa kweli kudhibiti kinywa chetu kutatuokoa na uharibifu. Lakini tunawezaje kujizoeza kudhibiti kinywa chetu?
Njia moja rahisi ya kufanya hivyo ni kutoongea sana. Biblia inasema: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu.” (Mithali 10:19) Njia nyingine ni kufikiri kabla ya kusema. Mwandishi huyo anaongozwa na roho ya Mungu kusema hivi: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.” (Mithali 12:18) Mtu anaposema bila kufikiri anaweza kujiumiza na pia kuwaumiza wasikilizaji wake. Kwa hiyo, Biblia inatupatia shauri hili linalofaa: “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.—Mithali 15:28.
Uwe Mwenye Bidii
Sulemani anasema: “Mtu mvivu hutamani asipate kitu; bali nafsi ya mwenye bidiiitanenepeshwa.” (Mithali 13:4) Kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema: ‘Mithali hiyo inamaanisha kwamba inafaa kuwa mwenye bidii badala ya kutamani tu vitu bila kufanya chochote. Watu wavivu hutawaliwa kabisa na tamaa zao, lakini tamaa hizo hazitokezi chochote.’ Lakini, nafsi au tamaa ya mwenye bidii inatoshelezwa, yaani, inanenepeshwa.
Tunaweza kusema nini kuhusu wale ambao husita kujiweka wakfu kwa Yehova kwa sababu hawataki kuwa na wajibu? Huenda wakatamani kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, lakini je, wako tayari kuchukua hatua yoyote kuhusiana na tamaa hiyo? Wale “watokao katika dhiki kubwa” wanapaswa kuonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu, kujiweka wakfu kwa Yehova, na kuonyesha wakfu huo kwa ubatizo wa maji.—Ufunuo 7:14, 15.
Ona pia yanayohusika ili kufikia cheo cha mwangalizi kutanikoni. Bila shaka, wanaume walio na tamaa ya kufikia kazi hiyo bora wanastahili sifa nayo Maandiko yanawatia moyo wafanye hivyo. (1 Timotheo 3:1) Hata hivyo, haitoshi tu kuwa na tamaa hiyo. Ili kuwa na sifa ya kustahili cheo hicho mtu anahitaji kusitawisha sifa na stadi zinazohitajiwa. Na jambo hilo linahitaji bidii.
Haki Ni Ulinzi
Mtu mwenye haki husitawisha sifa za kimungu naye husema kweli. Anajua kwamba kusema uwongo ni kinyume cha sheria ya Yehova. (Mithali 6:16-19; Wakolosai 3:9) Kuhusu hilo, Sulemani anasema: “Mwadilifu huuchukia uongo, lakini mwovu hutenda kwa aibu nafedheha.” (Mithali 13:5BHN) Mwenye haki haepuki tu kusema uwongo bali anauchukia kabisa. Anajua kwamba uwongo unaweza kuharibu uhusiano mzuri kati ya watu hata ingawa huenda ukaonekana kuwa usio na madhara. Isitoshe, mtu anayesema uwongo hawezi kuaminika. Labda kwa kusema uwongo au kwa njia nyingine, mwovu hutenda kwa aibu na hivyo hujifedhehesha.
Ili kuonyesha kwamba ni muhimu kutenda yaliyo haki machoni pa Mungu, mfalme mwenye hekima anasema: “Haki humlinda yeye aliye mnyofu katika njia yake; bali ubayahumwangusha mwenye dhambi.” (Mithali 13:6) Haki humlinda mtu kama ngome, lakini uovu humwangamiza.
Usijifanye
Mfalme wa Israeli anasema hivi kuonyesha kwamba alielewa tabia ya mwanadamu: “Kuna mtu mwenye kujitajirisha, lakini hana kitu; kuna ajifanyaye kuwa maskini, lakini anamali nyingi.” (Mithali 13:7) Huenda mtu akaonekana tofauti na jinsi alivyo. Huenda watu fulani walio maskini wakajifanya kuwa matajiri—labda ili kujionyesha kuwa wamefanikiwa au ili waheshimiwe. Huenda tajiri akajifanya kuwa maskini kusudi tu asijulikane kama ana mali.
Haifai kujifanya tajiri wala maskini. Ikiwa mapato yetu ni kidogo, sisi na familia zetu tunaweza kukosa vitu vya lazima maishani tukitumia pesa kununua vitu vya anasa ili kujionyesha kwamba tuna mali. Mtu anayejifanya maskini ingawa ana mali anaweza kuwa mchoyo, na kukosa heshima na furaha inayotokana na ukarimu. (Matendo 20:35) Maisha yanakuwa bora unapokuwa mnyofu.
Usitamani Kuwa na Vitu Vingi
Sulemani anasema: “Fidia ya mtu ni mali yake, lakini maskini hana cha kutishwa.” (Mithali 13:8BHN) Tunajifunza nini kutokana na usemi huo wenye hekima?
Kuna manufaa ya kuwa tajiri, lakini hiyo haimaanishi kwamba sikuzote tutakuwa wenye furaha. Katika nyakati hizi zenye taabu tunamoishi mara nyingi matajiri na familia zao hujikuta katika hatari ya kutekwa nyara. Nyakati nyingine, tajiri anaweza kulipa fidia ili kuokoa uhai wake au wa mtu wa familia yake. Lakini mara nyingi mtu aliyetekwa nyara huuawa. Sikuzote matajiri huishi kwa wasiwasi mwingi sana kwa sababu ya tisho hilo.
Maskini hana wasiwasi huo. Ingawa huenda maskini asiwe na vitu vingi vya starehe wala vitu vya kimwili walivyo navyo matajiri, si rahisi atekwe nyara. Hiyo ni faida moja ya kutotamani vitu vingi wala kutumia wakati na nguvu zetu katika kufuatia mali.—2 Timotheo 2:4.
Shangilia Katika “Nuru”
Sulemani anaendelea kuonyesha kwamba kufanya mambo kupatana na njia za Yehova kunatunufaisha sana. Anasema:“Nuru ya mwenye haki yang’aa sana; bali taa ya mtu mbayaitazimika.”Mithali 13:9.
Taa inafananisha kifaa tunachotumia kuangaza njia yetu ya maisha. ‘Neno la Mungu ni taa ya miguu ya mtu mwadilifu, na mwanga wa njia yake.’ (Zaburi 119:105) Lina ujuzi na hekima nyingi sana ya Muumba. Kadiri tunavyozidi kufahamu mapenzi na makusudi ya Mungu, ndivyo nuru ya kiroho yenye kutuongoza inavyozidi kung’aa. Jambo hilo hutufurahisha kama nini! Kwa nini tukengeushwe na hekima ya ulimwengu au ule unaoitwa “ujuzi isivyo kweli”?—1 Timotheo 6:20; 1 Wakorintho 1:20; Wakolosai 2:8.
Taa ya mwovu itazimika hata kama taa hiyo inaonekana kutoa mwangaza mwingi kadiri gani au hata kama anaonekana kuwa amefanikiwa kadiri gani. Mwishowe atajikuta gizani, naye lazima atajikwaa. Isitoshe, mtu huyo “hatakuwa na mema baadaye.”—Mithali 24:20,BHN.
Namna gani ikiwa hatujui tunalopaswa kufanya katika hali fulani? Namna gani ikiwa hatujui kama tuna mamlaka ya kuchukua hatua? Andiko la Mithali 13:10NW, linaonya:“Kwa sababu ya kimbelembele mtu husababisha tu pambano.” Kutenda bila kujua au bila mamlaka ni kimbelembele na husababisha matatizo. Je, halingekuwa jambo bora zaidi kupata shauri kutoka kwa wengine walio na ujuzi na utambuzi? Mfalme mwenye hekima anasema, “Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.”
Jihadhari na Matarajio ya Uwongo
Pesa zinaweza kuwa na manufaa fulani. Kuwa na pesa za kutosha ni bora kuliko kuishi maisha ya kujinyima au ya umaskini. (Mhubiri 7:11, 12) Huenda mtu akafikiri kwamba mali inayopatikana kwa njia isiyo halali inaweza kumfaidi, lakini atakuwa anajidanganya. Sulemani anaonya: “Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; bali yeye achumaye kidogokidogo atazidishiwa.”Mithali 13:11.
Kwa mfano, fikiria kishawishi cha kucheza kamari. Mchezaji wa kamari anaweza kutumia pesa alizochuma kwa kufanya kazi kwa bidii akitumaini kwamba atashinda pesa nyingi. Lakini mara nyingi yeye hufanya hivyo kwa hasara ya familia yake. Namna gani ikiwa mchezaji wa kamari anashinda? Kwa kuwa amepata pesa hizo kwa urahisi huenda asizithamini. Isitoshe, huenda asiwe na ujuzi wa kutumia vizuri pesa hizo alizoshinda. Pesa zake zinaweza kwisha upesi kama vile alivyozipata. Kwa upande mwingine, utajiri ambao mtu amekusanya polepole kwa kufanya kazi kwa bidii, huongezeka hatua kwa hatua na unaweza kutumiwa kwa njia ifaayo.
Sulemani anasema: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtuikipatikana, ni mti wa uzima.” (Mithali 13:12) Bila shaka, matarajio yasiyotimizwa yanakatisha tamaa na hufanya moyo uugue. Hilo ni jambo la kawaida. Lakini, sivyo ilivyo na matarajio ambayo yanategemea kabisa Neno la Mungu. Tuna uhakika kamili kwamba yatatimizwa. Yaelekea hata hatutakatishwa tamaa na matarajio ambayo huenda tukaona kama yanakawia.
Kwa mfano, tunajua kwamba ulimwengu mpya wa Mungu unakaribia. (2 Petro 3:13) Tunatazamia kwa hamu na kwa furaha kutimizwa kwa ahadi za Mungu. Inakuwaje ikiwa tunapongojea kutimizwa kwa ahadi hizo tunakuwa na mengi ya kufanya “katika kazi ya Bwana,” tunawatia moyo waamini wenzetu, na kujenga uhusiano wa karibu pamoja na Yehova? Badala ya ‘kuugua moyoni,’ tunajawa na furaha. (1 Wakorintho 15:58; Waebrania 10:24, 25; Yakobo 4:8) Haja ya muda mrefu inapotimizwa, ni mti wa uzima na jambo hilo hutia moyo na kuburudisha.
Sheria ya Mungu Ni Chanzo cha Uhai
Andiko la Mithali 13:13NW linasema hivi kuonyesha uhitaji wa kumtii Mungu: “Yuleambaye amelidharau neno, atadaiwa rehani ya mtu mwenye deni; lakini mtu anayeiogopaamri ndiye atakayepewa thawabu.” Ikiwa mtu mwenye deni anadharau neno kwa kukataa kuilipa, atapoteza kile alichotoa kama rehani. Vivyo hivyo, tunaweza kupata hasara tusipotii sheria za Mungu. Hasara gani hiyo?
Sheria ya mwenye hekima ni chemchemi ya uzima, kuepuka mitego ya mauti.’ (Mithali 13:14ZSB) Tutakosa mwongozo unaoweza kutusaidia kuwa na maisha bora na marefu ikiwa tutaishi bila kutegemea sheria ya Yehova Mungu mwenye hekima yote. Hiyo itakuwa hasara iliyoje! Basi ni jambo la hekima kujifunza na kutafakari Neno la Mungu na kuacha liongoze mawazo, usemi, na matendo yetu.—2 Wakorintho 10:5; Wakolosai 1:10.

No comments:

Post a Comment

NENO NI UZIMA Designed by 5gear Copyright © 2014-2015

Theme images by Jason Morrow. Powered by Blogger.