Vichwa vya Habari

SOMA KITABU HIKI UJAZWE NGUVU - MWANAFUNZI KAZI YA KIONGOZI




                              




  MUHTASARI
Uhusiano wetu na Mungu, kama uhusiano baina ya mtu na mtu, lazima uwe na mawasiliano ili uwe hai, na wenye afya. Kitabu hiki kinakuonyesha jinsi ya kuendeleza hamu ya kweli katika kuongea na Mungu. Pia katika kitabu hiki kuna mafundisho kutoka katika neno la Mungu ya kukusaidia kuwa na maombi yenye matokeo. Pamoja na hayo utajifunza kuwahudumia wengine kupitia kwa huduma ya maombezi. Maelezo yaliyopangwa kamili ya Barry Wood kuhusu maandiko yanadhihirisha jinsi unavyoweza kuwa na uwezo kupitia kwa maombi yaliyojibiwa. Mafundisho haya yenye kuhamasisha yatakupa mijadala kwa kirefu kuhusu masomo yafuatayo, kando na masomo mengine: Kuomba kwa uwezo na ujasiri Vita vya kiroho, mavazi yetu ya vita, na silaha Kufunga na kufungua kutumia funguo za ufalme Maombi yasiyojibiwa, na mapenzi ya Mungu Kufunga na kuomba Maombi na Uinjilisti Jinsi kutokutii kunavyozuia uwezo wa maombi Huduma ya maombezi Kwa nini tunaomba katika jina la Yesu Jinsi kutokusamehe kunavyoathiri maombi Kitabu hiki kimeundwa kwa ajili ya: Kutufundisha kuomba Kututia motisha ili tuwe na huduma ya maombi yenye mafanikio na uthabiti. Unajua kuomba vizuri? Je unahisi kuwa na nguvu za Mungu kwa maombi yaliyojibiwa? Hebu tutembee katika hii changamoto pamoja. Tutapaza sauti kama wale wanafunzi wa kale tukisema “Bwana Yesu, tufundishe kusali.”

UTANGULIZI “

Mtu alivyo katika chumba chake cha maombi faraghani, ndivyo alivyo kwa hakika.” – Robert M’Chyne Kama Wakristo, ni vigumu sana kujifunza kuomba. Maombi ni kazi ngumu. Ni vita vya mitaroni. Unaweza kufikiri kuwa kuomba ni rahisi, au ni furaha. Ndiyo, inaweza kuwa hivyo. Lakini maombi ya kweli ambayo humfikia Mungu na kuugusa moyo wake ili ajibu si rahisi! Labda wanafunzi wa Yesu walifikiri kwamba maombi ni rahisi, mpaka walipodumu na Yesu kwa muda. Walimtazama akiomba kwa Baba yake, akiugua. Wakapaza sauti wakisema “Bwana, tufundishe kusali hivyo!” (Lk. 11:1). Wanaume hawa wa kiyahudi waliofundishwa maisha yao yote jinsi ya kuomba waligundua kwamba kulikuwa na zaidi katika kuzungumza na Mungu ambayo hawakufahamu. Nimesafiri sana nikihubiri katika mamia ya makanisa na kuchunguza mitindo ya maisha ya Ukristo wa Wamarekani (pamoja na Ulaya Magharibi). Kutokana na safari zangu nimeshawishika kwamba maombi ya kweli ni fani iliyopotea. Hali hii ya “kutokuwa na maombi” hueleza hali yetu ya “kutokuwa na uwezo” kwa Mungu. Maisha yetu ya maombi ni uhai wetu kwa Mungu aliye hai. Muumini asiyekuwa na “nguvu za maombi” hana “nguvu za Mungu.” Thibitisho la mwamini katika kutembea na Mungu ni mazungumzo yake na Mungu. Kanisa linahubiri, linafundisha, linakuwa na mikutano na washa, na kupanga shughuli. Tunayafanya mambo mengi mazuri, lakini hatutilii maanani maombi! Maombi ni nini? Kuomba ni kuzungumza na Mungu. Ni sehemu katika maisha yetu inayohusiana na mazungumzo baina yetu na Baba yetu wa Mbinguni. Uristo, kwanza kabisa, ni uhusiano wa kibinafsi kati ya mwenye dhambi wa kawaida na Mungu wa jabu. Uhusiano wowote kati ya mtu na mtu lazima uwe na mazungumzo! Lazima kuwe na mawasiliano katika uhusiano ili kuufanya kuwa hai na yenye afya. Mungu ni Baba yetu, nasi ni wanawe. Jamii yetu ina shida ikiwa hatuwezi kuwasiliana kwa mazungumzao! Kwa nini tunapaswa kuomba? 1. Kuomba huonyesha uhusiano wenye afya kati yetu na Mungu. Kila mwamini anapaswa kuwa na hamu ya kweli moyoni ya kutamani kuzungumza na Mungu. Mtu anapoomba mara kwa mara, atathibiti maisha yake ya maombi na hamu ya Mungu zaidi. Ikiwa uhusiano wako na Mungu ni nzuri, basi hamu ya kuongea naye itakuwepo. Baadaye tutazungumzia jnsi dhambi na uasi huharibu maisha yetu ya maombi. 2. Yesu alituamuru tuombe. “Akawambia mfano, ya kwamba inawapasa kumwomba Mungu siku zote, wala wasikate tamaa” (Luka 18:1). Tutakata tamaa ikiwa hatuombi “nyakati zote.” kuomba ni tendo la tamaa na utiifu. Tunapaswa kuomba hata kama hatuna hamu ya kuomba. 3. Kuomba ni tabia ya ufahamu wa Mkristo mwenye afya. Yesu daima alidumu ndani ya Baba yake katika maombi. Tunapaswa kukaa ndani yake na ndani ya neno lake ili maombi yetu yaweze kujibiwa (Yohana 15:7). Mungu anataka maombi yetu, kwa sababu ulimwengu unahitaji majibu yanayotolewa na Mungu. 4. Maombi hufungua milango ya nguvu zisizo za kawaida katika maisha yetu. Maombi yetu yanaweza kumshughulisha Bwana Yesu kutenda kazi katika ulimwengu wetu. Kuomba kwa uwezo kutamruhusu Mungu kutenda kazi ambayo kwa kawaida hawezi kutenda. Baadaye katika kitabu hiki utajifunza kuhusu nguvu za maombi na jinsi ya kufanya nguvu hizo kutumika!46 Hebu tuvumbue “mambo ya kina” zaidi katika Neno la Mungu. Tunaweza kugawanyisha kweli hizi katika makundi ya maombi, vita vya kiroho, na maombezi. Hebu ingia na Yesu patakatifu zaidi kwa maombi na maombezi


JINSI YA KUISHI KIMIUJIZA

 Maombi ni mazungumzo kati ya mwanadamu wa kawaida na Mungu wa ajabu kila mara kuhusu mambo ya kawaida. Nyakati zingine wengi wetu huona kwamba kanisa, dini, na imani yetu hayatoshi kuleta mabadiliko katika ulimwengu wetu. Tunahitaji miujiza. Ingekuwa ajabu kutembea na Yesu kama walivyofanya wanafunzi! Miujiza iliahidiwa Mungu anataka kukuonyesha siri zake ili akukuwezeshe kuishi maisha yenye miujiza. Katika Injili ya Yohana tuna ahadi ya ajabu kutoka kwa Yesu. “Amin Amin nawambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa zaidi kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba” (Yohana 14:12). Hiyo ni ahadi ya kustusha! Yesu anasema kila mwamini wa kweli anapaswa kufanya miujiza miwili: Kuhudumu sawa na Kristo – “kazi nizifanyazo mimi yeye naye atazifanya…” Kuhudumu kuzidi Kristo – “na kubwa kuliko hizo atafanya kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” Ajabu! Inawezekanaje humu duniani, kwa Mkristo kuhudumu kuzidi Yesu? Ahadi kama hii inaonekana kama yenye mzaha. Inadhihirisha kuwa Yesu alikuwa na wazo la ajabu akilini mwake. Je, wazo hili ni lipi, na lingewezekanaje? Mambo Makuu Mawili Katika Maisha Ya Miujiza. Bwana wetu alitutazamia kuhudumu sawa naye, ama kumzidi. Alituambia jinsi tunavyoweza kutekeleza hayo. Katika Injili ya Yohana 14, Yesu anatufundisha jinsi mbili za kuishi katika miujiza baada ya kuondoka kwake: Kuomba kwa jina lake Roho Mtakatifu kuja kuishi ndani ya waumini Yesu alimaanisha kutekelezwa kwa ahadi ya kifungu cha 12 (kufananisha, na kuzidi) kwa maneno yake katika vifungu vya 13-14: “Nanyi mkiomba lolote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya mwana.Mkiniomba neno lolote kwa jina langu nitalifanya.” Ahadi katika kifungu cha 12 inatimizwa na “swali” lililoko katika vifungu vya 13 na 14. Maombi katika jina la Yesu ni funguo ya kufungua mlango wa miujiza katika maisha yako. Mambo ya kawaida yanaweza kuwa funguo ya miujiza. Ukisoma kifungu cha 15 na kuendelea, Yesu anaendelea kuzungumzia muumini kutiwa nguvu na Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu hukaa ndani yetu ili aongeze maana na imani katika maombi yetu. Tuna yote tunayohitaji ili kufungua mbingu. Sababu ya Kukosa Miujiza Kwa sababu gani hatuoni mambo yasiyo ya kawaida katika kanisa, au katika maisha yetu? Wakristo wengi hawana ufahamu kuhusu kweli hizi. Yesu anatuambia “tuombe jambo lolote” katika jina lake, naye atatenda. Ikiwa tunajua kuomba, basi atafanya. Wakati muumini anapomwomba Baba katika Jina la Yesu, Yesu huingia kazini kuendeleza huduma yake. Yesu atafanya huduma zaidi ikiwa wengi wetu watazingatia maombi. Unapowasilisha mahitaji yako kwa Mungu Baba, yeye humgeukia Mungu Mwana na kumwambia akutimizie hitaji lako. Yesu anaamka kitini pake pa enzi, na kwenda kukutimizia haja zako. Unaomba, naye48 Baba anamtuma mwanawe. Ni jambo la ajabu hilo! Na ahadi ya ajabu pia! Maombi yangu humshughulisha Yesu


JINSI YA KUOMBA KATIKA ROHO MTAKATIFU

 Jambo lililo kuu kuliko vyote ambalo Mungu alipata kunitendea lilikuwa kunifundisha kuomba katika Roho Mtakatiffu. Kwa kweli hatuwezi kuwa watu wa maombi mpaka tutakapojazwa na Roho Mtakatifu. Kwa hivyo Bwana, tufundishe kuomba katika Roho. -Samwel Chadwick, The Path of Prayer Je, umewahi kuomba “katika Roho”? Wakristo wengi hawafahamu jambo hili. Wengine huogopa na kuona kwamba pengine linafaa tu kwa wale waliojaliwa na uwezo zaidi, na kwa hivyo, huona haya kujihusisha nalo. Hata hivyo Maandiko yanatuagiza kuomba “katika Roho.” Mtume Paulo anatusihi “tuombe wakati wote katika Roho” (Waefeso 6:18). Roho Mtakatifu hutamani sana kutusaidia katika maombi. Bwana wetu Kristo, katika Yohana 14 anatuambia kwamba kuna funguo mbili za kutuwezesha kuishi maisha ya kipekee. Funguo hizo ni maombi na Roho Mtakatifu. Tunapaswa kujifunza kumruhusu Roho Mtakatifu kujihusisha kikamilifu katika mawasiliano yetu na Baba. Kuomba katika Roho kunaelezwa wazi katika Warumi: “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi ipasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea Watakatifu kama apendavyo Mungu (Warumi 8:26, 27). Fahamu kwamba Roho Mtakatifu mwenyewe hutamani kutuombea. Asili ya Roho Mtakatifu hudai kwamba atusaidie. Yeye ni “Roho wa Neema na dua” (Zakaria 12:10). Roho Mtakatifu ni msaidizi wetu katika maombi. Maombi yetu lazima yahusishe uwepo na uwezo wake. Kwa kweli Yuda 20 inatuamrisha tuwe “tukijijenga juu ya imani yetu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu.” Unaomba Wakati Gani Kwa Hakika? Maombi ya hakika ni maombi katika Roho Mtakatifu. Maombi mengine si maombi ya kweli kamwe. Ni mambo ya dini tu. Maombi hayo hayana maana yoyote kwa Mungu, wala kwa mwombaji. Ndio sababu maombi mengi ya hadhara ni sherehe za kidini, zisizo na maana, za kurudiarudia, na za kuchosha. Kinyume chake ni kuomba katika Roho, ambayo ni maombi yaliyo na nguvu, uwezo, na yamehuishwa na kudumishwa na Roho wa Mungu Mwenyewe! Kwa nini tunaona ajabu sana kwamba Roho Mtakatifu anapaswa kutawala maombi yetu? Tunamtegemea ayatie nguvu mahubiri yetu, kushuhudia kwetu, na kuabudu kwetu. Mbona tusimruhusu katika maombi yetu? Kipimo cha kutembea kwetu na Mungu hakimo katika mahubiri yetu, utoaji wetu, matendo yetu, wala mahudhurio yetu, ila kwa uwezo wetu katika maombi. Maombi ni kipimo cha uwezo wetu katika Mungu. Je Mungu husema nawe? Je, yeye hukusikiliza na kukujibu unaponena naye? Zaidi ya hayo, je yeye hukutia nguvu, hukupa uwezo, hukuhuisha na kuyakubali mazungumzo naye? Hiki ni kipimo halisi katika kumcha Mungu. Kuomba na Roho Maandiko yanazungumza juu ya kuomba “na” Roho na kuomba “katika” Roho. Mambo haya mawili hayafanani. Katika Wakorintho 14:14-15, Paulo anaeleza juu ya kuomba “na Roho.” Hapa haongei kuhusu Roho Mtakatifu wa Mungu, bali anazungumzia roho yako ya kibinadamu. Kuomba na roho ni kuomba na lugha isiyofahamika, bila kufahamu linalosemwa. Watu wengi husema ni kuomba kwa “lugha ya maombi.” Hata hivyo, kuomba katika Roho ni kitu tofauti. Hatukuagizwa kuomba tukinena katika lugha geni, lakini50 tunaagizwa “kuomba wakati wote katika Roho” (Waefeso 6:18- mkazo umetiliwa maneno yenye herufi nzito). Kuomba katika Roho si kwa watu wachache walio na uwezo wa “msisimko,” ambao ni washiriki wa kundi au dhehebu wajiitao wasisimkwa au wapentekote. Kuomba katika Roho ni maombi halisi. Hii inahusu kila mmoja. Hakikisho la Majibu Umewahi kuomba Mungu na kutaka hakikisho la jibu? Au Je, umepata kuwa na mashaka kwamba umeomba kufuatana na mapenzi ya Mungu? Ni nini husababisha mashaka hayo katika maombi yako? Unapoomba katika Roho Mtakatifu, utakuwa na hakikisho kwamba maombi yako yanalingana na mapenzi ya Mungu, kwa kuwa Roho wa Mungu atakupa yale unayopaswa kuomba. Zingatia ukweli huu kwamba ni maombi tu yanayoombwa katika Roho Mtakatifu ambayo yanafuatana na mapenzi ya Mungu, na kwa hivyo jibu limethibitishwa tayari. Mtu Mpotevu Anapoomba Kiongozi wa dhehebu moja maarufu alizusha mabishano miaka kadhaa zilizopita alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari. Alitangaza kwamba Mungu hawezi kujibu maombi ya Padre wa Kiyahudi (Rabbi) kwa sababu hawamwamini Yesu Kristo kama Mwokozi na Masihi. Watu wengi walishutumu kiongozi huyu wa kidini. Alishambuliwa kwa ushupavu wake kwa mambo ya dini. Je, alikuwa shupavu wa dini? Maoni yako yanategemea ufahamu wako wa maandiko. Tukiyachunguza maandiko zaidi, tutaona matokeo ya kufurahisha sana kuhusu maombi, na wasioamini. Yesu anatufundisha kuomba kwa jina lake, si kwa Yehovah, au Allah, wala kwa Mungu mwingine awaye yote. Yeye ni mpatanishi wetu kwa Mungu. Tunakuja katika jina lake. Roho Mtakatifu huliheshimu Jina la Bwana Yesu. Kwa hivyo mpotevu hawezi kuomba katika Roho kwa sababu hana Roho Mtakatifu anayeishi ndani yake. Ni mtu “asiye na Roho” (Yuda 19). Mungu hujibu maombi ya mpotevu anapofahamu kwamba jibu litamhamisha mtu huyo na kumwelekeza kwa wokovu katika Yesu Kristo. Matendo 10 inaeleza wazi wazi jambo hilo kutokana na tukio la Kornelio, Jemadari wa Kirumi. Maandiko yanamweleza kama “mtu mtauwa, mchaji wa Mungu…. Na kumwomba Mungu daima” (Matendo 10:2). Katika kifungu cha 31 tunaona Mungu akisikia maombi ya Kornelio, na kuyajibu! Wakati mwingine Mungu hujibu sala za washenzi - lakini sala yale tu yatakayomwongoza mpotevu kwa mwokozi Yesu Kristo. Hakikisho Thabiti. Heri mwamini aliyezaliwa mara ya pili! Roho wa Mungu huishi ndani yake na hutamani kuomba kupitia kwake ili kuhakikisha majibu kwa maombi yake. Hebu tuelekeze mawazo yetu katika Warumi 8:26,27 ili tujifunze zaidi kuhusu ombi hili katika Roho Mtakatifu. Paulo anasema “...hatujui kuomba ipasavyo” (Warumi 8:26). Hii ni kweli kwa kila muumini. Wewe na mimi tunaanza kuomba. Punde si punde hatujui la kumwambia Mungu wetu mkuu. Mara kwa mara tunasema maneno yasiyo sahihi. Tunaomba “vibaya” kama vile Yakobo 4:3 inavyosema. Wakati mwingine ilinibidi kumshukuru Mungu kwa maombi yasiyojibiwa kwa sababu nilikuwa nikiombea vitu visivyo sahihi, kwa kusudi mbaya. Hali ya Kutokujiweza Katika Maombi Warumi 8:26 inatujulisha kutokujiweza kwetu katika maombi inaposema “hatujui kuomba itupasavyo.” Kwa nini hatujui kuomba itupasavyo? Kumbuka kwamba Roho Mtakatifu hutusaidia katika “udhaifu wetu” (Warumi 8:26). Neno hili “udhaifu” linaonyesha hali ya kuwa pekee. Halina wingi. Halionyeshi kwamba tuna udhaifu mwingi au upungufu katika maisha yetu ya maombi, ijapokuwa tuna udhaifu mwingi. Kwa kweli tuna udhaifu mmoja mkubwa ambalo huathiri kila eneo la maisha yetu, kando na maombi. Udhaifu huu ni wa mwili. Asili yetu ya anguko, iliyoharibiwa na dhambi na ubinafsi, ndio udhaifu unaotulemea.

Hatuwezi kumpendeza Mungu katika “mwili” (Warumi 8:8). Hatuwezi “kufanya” matendo ya kiroho ambayo yatamfurahisha Mungu katika nguvu zetu wenyewe. Kuhubiri, kuomba, kushuhudia, kutoa, na huduma zinazofanyika kwa nguvu zetu haziwezi kumfurahisha Mungu. Huu ni “udhaifu” wetu. Wakati moja nilisikia udhaifu huu ukielezwa kama ukweli wa kiroho usioweza kukanushwa kabisa. Tunawajibika kuishi na ukweli huu. Udhaifu wetu ni “hali ya kushindwa kabisa kufanya lo lote katika maeneo ya roho kwa kutegemea mwili wetu.” Hii ndio sababu Roho Mtakatifu lazima atusaidie. Ni lazima aingie ndani yetu, atujaze, atutawale, na kuishi maisha yake kupitia kwetu. Tunapofikia wakati wa kushindwa kuomba, basi Mungu huwa ametuweka anapotaka – yani tumtegemee. Mungu hawezi kutusaidia tunapojaribu kumsaidia. Kristo Yesu anataka awe zaidi ya mwokozi wetu. Anataka kuwa chanzo cha uhai wetu. Roho Wake awe mfariji katika maombi yetu kwa kuponya maradhi yetu, na kuwa nguvu zetu katika kuondoa udhaifu wetu. Msaidizi Tunapoomba Roho Mtakatifu atatuchochea na kututiia hamu ya kuomba tunaposhirikiana naye. Tunapaswa kujirekebisha naye tunapokosa hamu ya kuomba. Hamu ya kuomba huja tunapomruhusu kuwa Bwana maishani mwetu. Tutataka kuomba mara kwa mara Roho Mtakatifu anapotutawala. Vile vile atatupa maneno ya kuomba. Kuomba katika Roho Mtakatifu kunamaanisha kwamba Roho Mtakatifu huomba na kufanya maombezi kupitia kwetu. Kwa kutumia akili yako na utu wako, Roho huomba kwa Baba kupitia kwako. Hayo ni maombi ya kimaajabu. Je, unaamini kwamba haya yanawezekana? Ndiyo. Roho Mtakatifu anaweza kusema kupitia maeneo mengine ya maisha ya Mkristo, kama vile: Unapohubiri – Mungu anaweza kuhubiri kupitia kwa mwanadamu Unapofundisha – Mungu hufundisha kupitia kwa mwanadamu Unapoishi – Mungu anaweza kuishi kwa kutumia mwanadamu Mbona isifanyike hivyo wakati wa kuomba? Je, Mungu hawezi kuomba kwa kutumia mwanadamu? Ndiyo, anaweza, na anatamani sana kufanya hivyo. Warumi 8:26 inasema yeye “huugua” ndani yetu. Ana hamu kubwa sana ya kutaka kuomba kupitia kwa maombi ya muumini. Kuugua kwa Roho “Kuugua” huku si lazima kuwe kwa maneno ya kibinadamu. Mara kwa mara ni Roho wa Yesu ndani yako anayetamani kushirikiana nawe. Kuugua huku kunatokana na Mungu tu. Mara kwa mara hakuna maneno. Roho hututaka tuwe shirika pamoja naye. Mungu wetu ni wa thamani kiasi cha kutamani kushiriki nasi katika ubinadamu wetu wa dhambi. Mara nyingi tunakariri tu maombi, badala ya kutulia na kujua kwamba yeye ni Mungu. Maombi kufuatana na Mapenzi ya Mungu Kuna wazo lingine moja katika mafundisho ya Paulo, katika Warumi 8:27: “Huwaombea… Kama apendavyo Mungu.” Utathibitishaje kuwa maombi yako yatajibiwa? Kudhibitisha ni rahisi sana, nalo ni kuomba daima katika Roho Mtakatifu. Kila mara Roho Mtakatifu huomba kwa kufuata mapenzi ya Mungu, na kila ombi linalowakilishwa kufuatana na mapenzi ya Mungu litajibiwa kwa “Ndiyo” itakayojulikana pote. 1 Yohana 5:14 inaahidi hivi: “Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusia.” Omba katika Roho, nawe utapata majibu! Kuombea Uponyaji Mtu fulani akihitaji maombi kutoka kwako kwa ajili ya uponyaji, lakini hujui kama ni mapenzi ya Mungu kumponya mtu huyo! Mara nyingi tunaomba hivi, “Mungu, kama ni mapenzi yako, mponye mtu huyu.” Hicho ni kifungu chetu cha kutorokea. Tunaweka “ikiwa” ya kitheologia kwa kujilinda. Maombi ya “ikiwa” si maombi ya imani. Ni wakati ambapo hatujui mapenzi ya Mungu kwa uwazi, ndipo tunahitaji kuomba Roho Mtakatifu atusaidie.52 Tunapoomba Tuangalie baadhi ya maelekezo kadhaa, au hatua za nidhamu ambazo zitamruhusu Roho wa Mungu kutia nguvu maombi yetu kabla hatujaomba: 1. Ungama kila dhambi unayojua. Isaya 59:2 inatuambia kwamba; “dhambi zenu zimefarikisha nyinyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone hata hataki kusikia.” 2. Chagua kwenda kinyume cha ubinafsi. Jitoe mwenyewe kwa Mungu, na kwa mapenzi yake. Mtangaze Yesu kuwa ni Bwana wa vyote. Jinsi unavyoanza muda wako wa maombi kwa kuungama dhambi, ndivyo utakavyohitaji kumwambia Mungu, “Yesu ni Bwana wa maisha yangu; Bwana Yesu, mimi ni wako.” Ungamo hili kwa mdomo huthibitisha kujitoa ndani ya moyo wako, na humfurahisha Mungu. 3. Weka Muda wako wa maombi kwa Roho Mtakatifu. Kwa kinywa chako mwambie kutokuweza kwako. Mkaribishe aombe kupitia kwako. Mwombe atawale ibada yako. 4. Mngoje Bwana. Maandiko yanasema, “Tulia mjue ya kuwa Mimi ni Mungu.” Ngojea kimya, au soma Neno kwa sauti. Roho wa Mungu ataanza kushiriki nawe. Unaweza kupata wazo fulani. Omba hilo wazo kwa sauti. Una kila haki ya kuamini kwamba mawazo hayo yametoka kwa Mungu. 5. Uliza, Je, ni mimi au ni Mungu? Utaweza kushangaa na kuuliza, “sijui wazo hili ni langu, au ni la Bwana.” Mbona kuwe na tofauti kati ya matakwa yako, na matakwa ya Mungu? Ikiwa umemtangaza Yesu kuwa Bwana, na kuungama kila dhambi unayojua, na kumwomba Roho Mtakatifu atawale mawazo yako, basi mawazo yako na ya Mungu yatafanana! Zaburi 37:4 inasihi kwamba, “Nawe utajifurahisha kwa Bwana, naye atakupa haja za moyo wako” Kuomba Bila Kuwa na Hakika Mara nyingi kufahamu mapenzi ya Mungu si rahisi. Wakati mwingine tunapaswa kufuata miongozo fulani katika maombi” Omba hadi upate jibu Omba hadi upate thibitisho la jibu. Omba hadi Mungu aseme “la.” Unaweza kuwa na mashaka jinsi Mungu huzungumza nyakati kama hizi. Hufanya hivyo kwa njia ya Roho wake Mtakatifu akaaye ndani yetu. Maandiko yanatuagiza kuwa “Amani ya Kristo itawale ndani ya mioyo yenu…” (Wakolosai 3:15). Unawezaje kuwa na amani moyoni mwako kutokana na hitaji fulani? Roho wa Mungu ataleta amani yake akiruhusiwa “kutawala” ndani ya roho zetu. Neno tawala ni miongoni mwa maneno sita ya Kiyunani yaliyotafsiriwa “tawala” katika Agano Jipya. Lina maana ya “kutenda kama mwamuzi.” Roho wa Mungu atakuwa mpatanishi katika nyakati hizi za kutokuwa na hakika. Kwa hivyo omba bila kukoma. Atakupo amani! Majibu Yaliyoahidiwa Kuomba kile ambacho Mungu ameahidi katika Maandiko ni azimio tofauti. Roho aliye ndani yako ndiye aliyeandika kitabu kilicho na upuzio wake. Kudai ahadi zilizomo Bibliani ni tendo la imani. Omba: Ukimkumbusha Mungu ahadi yake. Mnukulie Neno lake. Ukileta hitaji mbele yake, “Mwambie Mungu mahitaji yako na usisahau kumshukuru kwa majibu yake” (Wafilipi 4:6). Ukidai jibu kwa imani. Yesu aliahidi kwamba “Yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu” (Marko 11:24)

Ukimsifu daima, na kuamini kwamba jibu liko njiani. Hapa tutajifanya kama watu walio na jibu tayari, na kumwachia Mungu wetu Mkuu maswali kama ya lini, wapi, na jinsi gani, tukijua kwamba “yatakuwa yenu.” Katika sehemu zifuatazo, tutaendeleza ufahamu wetu kuhusu uwezo wa maombi. Misaada 1. Katika kitabu kilichotangulia, nilieleza uponyaji na maombi kwa kirefu zaidi. Tazama sura ya 7 ya Questions New Christians Ask (Old Tappan, New Jersey: Fleming H. Revell Company, 1979), pp.76 – 86. 2. Angalia sura ya 1, “Jinsi ya kujua Mapenzi ya Mungu”, katika Questions New Christians Ask. 3. Neno ni brabeuo; Angalia W.R. Vines Expository Dictionary of Old and New Testament Words (Old Tappan, New Jersey: Fleming H. Revell Company, 1981), P. 307.


JINSI YA KUOMBA NA NGUVU

 Vipengele viwili muhimu katika maombi ya mamlaka ni kujua ni nani unayemwomba. Pili, ni kujua wewe u nani ndani yake. “Naomba macho ya mioyo yenu yatiwe nuru”(Waefeso 1:18). Kwa nini Mungu hajibu maombi yangu? Je, umewahi kuuliza swali hilo? Ni nani ambaye hajawahi kuuliza swali hilo kwa wakati fulani? Kuna sababu nyingi ambazo humsababisha Mungu kusema “la,” ijapokuwa muumini yeyote anaweza kuomba kwa ujasiri hadi Mungu ajibu. Kila muumini aombe kwa uhodari. Waebrania 4:16 inatuhimiza “kukaribia kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.” Kufahamu U Nani Ujasiri katika maombi ni matokeo ya sababu nyingi, mojawapo ikiwa imani. Kichwa cha somo litakalofuata ni Jinsi ya Kuomba Kwa Imani. Hata muhimu zaidi kuliko kuwa na imani kwa Mungu ni kujua u nani katika Kristo. Kutambulikana na Kristo ndiko kunatupa moyo na ujasiri wa kuomba kwa uhodari mbele ya kiti cha Mungu Matakatifu. Ni mtoto wa Mungu tu anayejua nafasi yake katika Kristo awezaye kutumaini kuomba na mamlaka. Inaonekana kwamba wakristo wachache wa kisasa ndio wanaelewa maana ya kutambulikana na Kristo. Ujasiri katika maombi hutokana na ufahamu wa kweli juu ya Mungu na jinsi anavyokuonoa, kama mtoto wake. Mamlaka ya Muumini Kila mtoto wa Mungu ana “haki kitini pa enzi.” Haki hizi zinatokana na yale Bwana Yesu alifanya msalabani kwa ajili yetu. Haki za muumini kitini pa enzi ndio mamlaka yake katika Yesu Kristo. Mtume Paulo anaeleza mamlaka yetu katika Waefeso 1:18-23: “Ninaomba kwamba macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo: na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo, na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uwezo wake: aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akivitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.” Maandiko haya ni maombi dhahiri. Paulo anaomba kwamba macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, ili mjue ninyi ni akina nani katika Kristo. Ubeti huu ni wa ufasaha unaofunua haki zetu mbele ya kiti cha enzi. Sisi ni warithi katika Kristo. Tuna urithi (Warumi 8:17) ulionunuliwa kwa ajili yetu kupitia kwa kazi iliyomalizika ya Kristo, yaani kifo chake, kuzikwa kwake, kufufuka kwake, na kupaa kwake. Kiti cha Mamlaka Yetu “Aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho” (Waefeso 1:20). Maneno haya yanatuambia kwamba Kristo alifufuka na kukalia kiti cha enzi cha Mungu. Anatawala katika ulimwengu na sayari. Sote tunaelewa hivyo; lakini, Je, wajua kwamba unatawala pamoja naye katika huo ulimwengu wa roho?56 Paulo anathibitisha jambo hili katika ufasaha kwenye maandiko mengine mawili: “akatufufua pamoja naye, katuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu” (Waefeso 2:6); “na ninyi mmetimilika katika yeye aliye kichwa cha enzi yote na mamlaka” (Wakolosai 2:10). Tamko la ajabu hilo! Sisi (waumini wote waliozaliwa mara ya pili) tumeketishwa “pamoja naye” na tunashiriki ushindi wake. Tu warithi pamoja naye katika utawala na nguvu zake. “Tumetimilika” katika yeye. Basi hivyo ni kusema kwamba kweli zote katika ushindi wa Bwana juu ya ulimwengu, mwili, na shetani, ni kweli pia kwa muumini. Kwa wakati huu “tumeketishwa” pamoja naye katika ulimwengu wa roho – si unapokufa, ama Yesu anaporudi tena kuchukua kanisa lake. Uko pale sasa, ukitawala na kungoja pamoja na Kristo juu sana kuliko falme zote, na mamlaka, na nguvu (Waefeso 1:21). Nguvu zote za Mungu alizopewa Kristo zimepewa kanisa pia, “ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika Kristo (Waefeso 1:23). Ukweli Wa Hali Huu ukweli tunauita “ukweli wa hali.” Kwa maneno mengine, Mungu huliona kanisa ambalo limekamilika katika Kristo. Kulingana na Mungu, tumewafanya maadui wetu kuwa chini ya miguu yetu. Mungu anatuona tukiwa mbinguni pamoja naye. Hatusimami mbele ya Mungu Mtakatifu katika hali ya kuhukumiwa au tukiwa kama wenye dhambi na hatia. Bali tunasimama katika hali ya msamaha, kuhimidiwa, na kama warithi pamoja na Kristo. Mungu anatupenda kupitia kwa mwanawe. Tu “ndani ya Kristo” katika kikao chetu kwa Mungu. Kikao na Maombi Huenda ukashangaa kwamba hii ina maana gani katika maombi ya uhodari. Inahusika kabisa. Je, unaweza kukaribia kiti cha enzi cha Mungu Mtakatifu na hatia ya dhambi mbele ya macho yako? Mtume Yohana anaeleza jambo hili vizuri: “Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri katika Mungu” (1 John 3:21). Je, moyo wako mara kwa mara unakuhukumu? Je, hatia, kushindwa, au kukosa ujasiri hukuzuia kuomba na kuuliza” Rafiki, hii ni mbinu ya shetani kuhukumu moyo wako. Anakuweka katika msingi wa “kutenda” badala ya msingi wa kikao mbele ya Mungu. Hakuna anayestahili mbele ya Mungu kwa matendo yake. Hata hivyo, katika Kristo, tunahimizwa kukaribia kiti cha neema kwa ujasiri ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji. Kama watoto wa Mungu tumependwa na kukubaliwa. Sisi si waombaombaji, wanaomwendea Mungu kupitia mlango wa nyuma ili kuomba makombo. Sisi ni tajiri na warithi pamoja na Kristo. Tunaomba na kupokea, kwa sababu ya yale amefanya, na jinsi tulivyo ndani yake. Chanzo Cha Mamlaka Yetu Katika maombi ya Paulo katika Waefeso 1, anatuonyesha urithi huu mkuu na nguvu za kutawala juu ya kila jina litajwalo katika ulimwengu huu au ulimwengu ujao (ulimwengu wa roho), na kwamba uwezo huo tumepewa “sisi tunaoamini” (Waefeso 1:19). Imani yetu, katika ukweli huu uliofunuliwa, ndio ujasiri wetu mbele ya Mungu. Nguvu za Mungu zimeelekezwa kwa wanaoamini. Je, wewe ni muumini? Simaanishi muumini anayefuata mafundisho ya dini, bali muumini katika vitendo. Paulo anaomba kwamba “macho ya mioyo yenu” yafunguliwe – si macho ya akili, bali macho ya moyo wako. Kweli hizi kuhusu sehemu yetu katika Kristo hayafahamiki kwa mawazo ya akili – ila yanatokana na ufunuo wa Roho Mtakatifu kwa roho yako. Ni moyo tu ambayo inaweza kutambua ukweli huu. Ni kwa waaminio. Hii inazidi ufahamu; lakini haizidi imani. Chanzo cha nguvu zetu na mamlaka yetu katika Mungu ni imani. Amekamilisha kazi yake ndani ya Kristo. Ni lazima tuamini kwamba ametukamilishia. Nguvu za Mungu zinaweza kudhihirika katika maombi muumini anapotambua rohoni jinsi alivyo ndani ya Kristo. Wasongezao Milima Yesu alimaanisha maombi haya ya imani aliposema: “Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng’oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu57 hiyo nawaambia, yeyote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu” (Marko 11:23-24). Hii ni ahadi ya ajabu! Je, una “milima” yanayosimama katika njia yako? “Mlima” inamaanisha kizuizi kilichoko katikati yako na mapenzi ya Mungu. Mlima huu unaweza kuwa ni shetani mwenyewe. Yesu anatuambia kwamba tuna uwezo wa kuondoa vizuizi vyo vyote kwa kukiri imani yetu. Tunaongelesha milima, nayo yanasonga! Hayo ni mamlaka, na nguvu kwa hakika. Njia yetu kuelekea kwenye kiti cha enzi ni wazi mno! Musa Na Yoshua Tunaona mfano mzuri wa maombi ya kusongeza milima na maombezi katika matukio ya Musa na Yoshua walipokumbana na Amaleki na kabila la Waamaleki. Mungu alimwambia Musa amiliki nchi ya Kanani. Lakini kulikuwa na pingamizi njiani. Amaleki ni mfalme kafiri, ambaye ni mkali sana. Musa na Yoshua lazima wamng’oe. Musa anafanyaje basi? Ana mipango aina mbili ya vita. Atampigania Mungu kwa jinsi mbili – kwa mwili na kwa roho. Yoshua anaenda kukutana na wanajeshi wa Amaleki. Anapigana vita vya mwili. Musa anakwea juu ya kilima kuomba. Mwanzo 17 inasimulia huu mpango wa ajabu wa vita: “Musa akamwambia Yoshua, Tuchagulie watu ukatoke ukapigane na Waamaleki; kesho nitasimama juu ya kilele kile, na ile fimbo ya Mungu nitakuwa nayo mkononi mwangu. Basi Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia, akapigana na Amaleki; na Musa na Haruni na Huri wakapanda juu ya kile kilima” (Mwanzo 17:9,10). Ningelikuwa jemadari Yoshua, ningejaribiwa kukabiliana na Jenerali Musa kwa jambo hili! Ningelipendekeza Musa aelekee kupigana na Amaleki mwenyewe, nami nikwee mlimani kuomba. Hiyo inaonekana kuwa salama! Ama sivyo? Fimbo Na Panga Vita viwili. Maadui wawili. Silaha aina mbili tofauti. Yoshua alimpiga Amaleki kwa panga na mikuki. Lakini Amaleki hakuwa adui kwa hakika. Shetani ndiye aliyekuwa adui kwa kweli. Amaleki alikuwa mtumishi wa shetani tu. “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika uliwengu wa roho” (Waefeso 6:12). Musa anapigana na adui wa kweli kwa kutumia silaha za rohoni. Anamwombea Yoshua. Mkononi ana fimbo ya Mungu. Hii ilikuwa ni fimbo ya kawaida ya kuchunga kondoo. Baada ya kukutana na Mungu mlimani, fimbo iligeuka kuwa “fimbo ya Mungu.” Fimbo hii ni nguvu ya Mungu iliyowekwa mkononi mwa mtu mwenye imani. Ikiwa mkononi mwa Mungu, fimbo ni nguvu ya Mungu. Kwa hivyo, katika imani, Musa akiwa mlimani anaomba dhidi ya mlima uliosimama dhidi ya wana wa Israeli, yaani Amaleki. Musa anapoinua fimbo na kuomba, Yoshua anamshinda Amaleki. Lakini Musa anapochoka na kurudisha mikono yake chini na fimbo kushushwa, Amaleki anashinda vita dhidi ya Yoshua. Vilikuwa vita vya ajabu kweli! Havikushindaniwa kwa upanga au kwa mikuki. Walishinda, au kushindwa kwa maombi. Hivi ndivyo ilivyo haswa maishani mwetu. Adui wako si Amaleki (au tajiri wako, mume wako, au hata mke wako). Adui wako ni nguvu zinazokukabili kupitia kwa mtu huyo. Mara nyingi tunapigana vita ambavyo havifai, na adui asiyefaa, tukitumia vifaa visivyofaa. Kutumia Fimbo Siku moja nilimsikia mtu moja akisema, “Ningetamani kuwa na fimbo kama ya Musa. Ningempiga Amaleki jinsi Yoshua alivyofanya.” Habari ya ajabu! Unao fimbo kama ya Musa! Kila Mkristo ana fimbo ya Mungu. Ukiwa na fimbo hiyo, unaweza kugawanya maji, kumshinda Amaleki, na kudai nchi ya ahadi.
Una fimbo mbili! “Fimbo zetu mbili za Mungu” ni sehemu yetu katika Kristo, na imani yetu kwa Yesu. Hebu fikiri tena, kazi ya fimbo ya Musa ilikuwa nini? Ilikuwa ni nguvu ya Mungu iliyowekwa kwa mkono wa mtu mwenye imani. Hivi leo, Mungu ametunuku kanisa lake nguvu hizi. Anatupa fimbo mbili: ushirika wetu na Kristo, na jina la Yesu. Kwa sababu ya kikao chetu katika Kristo, Mungu anatuomba tutarajie kusongeza milima. Yesu anasema tuombe “katika jina langu.” Tafsiri ya Wirnams kwa Marko 16:17 inasema, “Ishara hizi zitafuatana na waaminio; kwa kutumia jina langu watafukuza pepo.” Jina la Yesu ni fimbo ya Musa kwa Mkristo. Kwa kutumia jina lake (kwa imani) tunaweza kufukuza pepo. Kila moja wetu ana “pepo” wa aina fulani, ama Amaleki aliye kizuizi. Ni heri tuwaondoe. Tunaweza kufanya kama Musa kwa kutumia fimbo ambalo Mungu ametupa, yaani jina la Yesu Kristo lenye nguvu. Kuungamanishwa naye na imani yetu kwa kuungamanishwa huku kunatupa uwezo dhidi ya ulimwengu, mwili, na shetani. Inatuwezesha pia kumfikia Baba (Warumi 5:2) wakati wowote, usiku au mchana. Michango 1. Sura ya 9, Questions New Christians Ask (Old Tappan, New Jersey: Fleming H. Revell Company, 1979). Pp.93 – 102


JINSI YA KUOMBA KWA IMANI 

Imani si kuamini kwamba Mungu anaweza, ama ataweza, bali imani ya kweli ni kuamini kwamba Mungu ameshatenda. Je, umewahi kumwomba Mungu kitu kikubwa, na ukiisha sema “Amin,” ukawa na tashwishi kama kweli utapata jibu? Labda ulisema, “Hawezi kujibu ombi hili.” Kweli, ishakuwa hivyo kwangu – ni aibu. Mara nyingi Mungu ameniaibisha zaidi kwa kuyajibu maombi yangu, ijapokuwa nilikosa imani. Yeye ni Mungu mkuu! Hata ingawa hivyo, Mungu anaheshimu maombi katika imani. Maombi ni ufunguo wa kufungua mlango wa hazina za mbinguni. Imani humfurahisha Mungu. Hebu sikiliza ahadi ya maandiko kuhusu maombi na imani: Yesu akajibu, akawaambia: “Mwamini Mungu. Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng’oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.” – Marko 11:22-24 Kwa kuwa Mungu ni Baba yetu, anapendezwa tunapomwamini. Anapenda tuamini neno lake. Hakuna kitu kingine kinachompendeza kuliko imani ndogo kama ya mtoto mdogo. Waebrania inasema kwamba, “lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza” (Waebrania 11:6). Hii ni haki kabisa tunapomwendea katika maombi. Bwana wetu alitilia jambo hili mkazo katika Marko 11:22-24. Alituamuru tuwe na imani kwa Mungu. Anatuhimiza tuombe tukiwa na imani ili tupate tayari majibu kwa maombi yetu. Maneno hayo yanatuonyesha Mungu alivyo. Anatamani kuwapa wanawe wanaoamini mahitaji yao! Kuomba, Kupiga kelele, na Kusikitika Yesu anatuambia tumwendee Mungu kwa kuomba, kutafuta, na kubisha (Luka 11:9,10). Je, unaomba ukiwa na imani sawa na ya mtoto anayefahamu upendo na wema wa baba yake? Nafahamu watu wengi ambao wanapoomba, wanaenda mbele ya kiti cha enzi wakiwa na nia ambayo ni kinyume cha imani na kumtegemea Mungu. Mwombaji. Huyu humwendea Mungu kama mwenye kuombaomba. Yeye husihi, huombaomba, hubembeleza, hushurutisha, na kujaribu kumpokonya Mungu baraka alizofungia mkononi. Huyu mtu, ijapokuwa ni Mkristo, hatambui yeye ni nani katika Kristo, na wala hatambui Mungu ni nani. Anahofia Mungu, na kwa hivyo yeye ni mwombaombaji. Nia hii si ile inayofundishwa na Kristo. Pia haina heshima kwa msalaba wa Bwana Wetu Yesu Kristo. Hii humtia Mungu huzuni. Mpiga Kelele. Huyu hufikiri kwamba Mungu ni kiziwi! Paaza sauti, au Mungu hawezi kukusikiliza, ama kukujibu. Umewahi kusikia mtu kama huyu kanisani – akiwa bila chombo cha kupaaza sauti! Katika Yohana 14:14, Yesu alisema, “Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya.” Tazama alivyosema, “Mniombe,” wala si “mnipigie kelele.” Wewe nami hatuhitaji kumpazia Mungu sauti zetu. Anayajua mawazo na shauku ya mioyo yetu. Kwa moyo wa kunyenyekea na kwa imani ndogo, “tunaomba.” Mwenye Kusikitika. Mtakatifu hafifu hudhani kwamba lazima asikitike anapoenda kwa Mungu. Anaomba hivi: “Oh, Mungu, niko hapa tena. Ndio, ni mimi, mimi tu yule niliyekosa!” Huyu huvaa magunia na kujitia mavumbi akienda kanisani. Ana wingu la kulaaniwa kichwani mwake. Huomba60 Hivi, “Ole wangu.” Ni haki kuhisi kuwa na hatia, na ni kitu cha kusikitisha. Kuwa na hatia hutunyang’anya furaha katika Bwana. Katika kitabu changu, Questions New Christians Ask , tumejadili kwamba Mkristo hasimami mbele ya Mungu mtakatifu akiwa na hatia na hukumu. Hata aliyeshindwa, au Mkristo anayeishi kwa kutimiza tamaa za mwili hajafukuzwa kutoka kwa uwepo wa Mungu (labda ametenganishwa na raha Ya Mungu, lakini si uwepo wake). Muumini Hali yetu isiwe ile ya mwenye kuomba omba, mpiga kelele, au mwenye kusikitika tunapomwendea Mungu kwa maombi, bali tuwe waumini walio na ujasiri. Ni kweli, tuna haki ya kuwa katika uwepo wa Mungu. Warumi 5:2 inatueleza vyema: “ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo mnasimama ndani …” Kuna mambo mawili katika kifungu hiki ambayo yananifurahisha. Kwanza ni kuifikia. Hii inamaanisha “kutambulisha,” kama vile kutambulishwa mbele ya mfalme. Ni kama barua ya kitambulisho. Katika Kristo tuna haki kuifikia kiti cha enzi cha Mfalme wa vyote. Kwake tuna cheti cha kututangaza kuwa wenye kufaa kwa sababu ya kununuliwa kwetu kwa damu ili tuwe na uhusiano na Kristo. Paulo pia anasema kwamba “tumeifikia.” Neno ku inaonyesha hali ya kukamilika, kuliko hali ya kisasa kama vile hutumika. Mkazo hapa ni kwamba milele tumewakilishwa kwa Mungu, na hakuna yeyote anayeweza kubadilisha tukio hilo. Kila mara tunasimama kwa neema tukiwa tumependwa na Mungu milele! Huu ni ukweli wa ajabu ya kuishi kwalo! Basi tuendapo kuomba, ni lazima tuamini kwamba tumekaribishwa katika uwepo wake! Unamwendea mfalme, Ukimletea maombi makuu; Neema na nguvu zake ni kwamba, Huwezi kuomba zaidi. Aina tofauti Za Imani Sio Matakwa tu Kwa sababu imani humpendeza Mungu sana na kumruhusu kufanya kazi katika maisha yetu, ni jambo la maana sana kufahamu imani ni nini, na jinsi inavyofanya kazi. Imani ni neno ambalo lina maana tofauti kwa watu mbali mbali. La maana ni kufahamu kile Mungu anachomaanisha anaposema “imani.” Ili kujifunza vyema, ni vizuri kueleza kile ambacho si imani. Imani sio kuwa na matakwa, au kutumaini. Isifananishwe na dhana nzuri. Imani inayoelezwa katika Bibilia si imani ndani ya imani, bali ni imani kwa Mungu. Watu mara kwa mara watasema, “Mungu anaweza kufanya jambo lolote,” na kusema ni imani. Ni kweli Mungu anaweza kufanya lolote. Lakini hatuhitaji imani ili kuamini hayo. Huwezi kuenda mbinguni kwa kutegemea imani kama hiyo. Je, kama yule mwivi aliyekuwa kando ya Yesu msalabani angesema, “Yesu anaweza kuniokoa,” kusema hivyo kungemwokoa? Hasha! Hakuna imani iliyohusishwa, hakuomba ili kupokea. Hata kumtegemea Mungu hakumo. Watu wengine wana imani ya “Mungu ataweza.” Hii ni afadhali kuliko imani ya “Mungu anaweza” kwa sababu mtu huyu anasema, “Mungu atatimiza mahitaji yangu. Mungu ataniokoa siku moja kutoka kwa dhambi zangu.” Hata hivyo, mtu hawezi kwenda mbinguni kwa mawazo ya dhana kama hayo. Kuamini kwamba Mungu atatenda jambo si sawa na kuomba na kudai kwa imani kwamba ametenda tayari. Imani Kibibilia Imani ya kweli ni kwamba “Mungu tayari” ametimiza matakwa yangu. Hi ni imani yenye maana ambayo imeelezwa katika Waebrania 11: “Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana” (Waebrania 11:1).61 Imani si kutumaini, bali ni kuwa nayo. Kiini cha neno “kuwa na hakika” ni halisi, au hali halisi ya kitu, kama vile tunaona katika Waebrania 1:3 kuhusu Kristo kuwa hakika ya Mungu mwenyewe. Nikiwa na imani kwa kitu cha kubainisha, basi kinafanyika kuwa halisi katika maisha yangu. Nikiliamini, basi ninalo! Si ajabu hilo? Ndio, ni kweli. Huyu ni Yesu akifundisha katika Marko 11;24: “Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.” Wakati ule ninapoamini kwa hakika, jibu li njiani, laja. Lugha iliyotumika katika maandiko pale mwanzoni ina uzito mwingi kwamba tafsiri ya New American Standard Bible inakosoa kwa usawa tafsiri iliyokubalika kutoka kwa “mtapokea” hadi “mmepokea.” Kwa hivyo, mara tu unapoamini, tayari umepokea (hali ya kale)! Yesu ndiye aliyesema hayo, si mimi. Imani ni kupokea. Mtu alieleza imani kibibilia hivi, “Imani ni kutenda kama ipo, hata kama haipo, na itakuwepo.” Imani ni kubadilisha bayana kuwa yaliyopo. Imani Na Mapenzi Ya Mungu Yesu alituambia tuwe na “imani kwa Mungu.” Hi inahusu mpango na kusudi la Mungu kwa maisha yako. Yeye ni Mungu Mkuu, mwenye enzi. Imani yote ulimwenguni haiwezi kubadilisha makusudi yake yenye enzi. Watu walio na saratani wameamini kwamba Mungu angeponya magonjwa yao, ijapokuwa walikufa. Waraka wa Kwanza wa Yohana 5:14 inafaa sana inapoeleza kwamba, “tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia.” Kifungu cha 15 kinatuhakikishia kwamba tukiomba (kwa imani) sawasawa na mapenzi yake, “tunazo zile haja tulizomwomba.” Tunapofahamu mapenzi ya Mungu alivyotufunulia katika maandiko, basi tunaweza kudai hayo kama ahadi zake. Mungu tayari hutimiza mahitaji yetu kabla kutuahidi. Tunaweza kuishi au kufa kwa ahadi za Mungu. Maombi ni kubadilisha ahadi za Mungu kuwa riziki kila siku. Siguswi Mimi! Wakati moja nilikaa Romania kwa majuma mawili. Nilifwatwa na maaskari makachero kila nilipoenda. Wachungaji niliokuwa nikifanya kazi nao waliishi kwa kuhofia usalama wao. Nilimuuliza mmoja wa hao wachungaji wajasiri jinsi walivyoweza kulala usiku. Je, alihofia maisha yake? Akiwa na tabasamu kama ya malaika, alinijibu, “Mimi siwezi kuguswa. Ikiwa Mungu angali amenipa kazi ya kufanya, askari hawana uwezo wa kunidhuru.” Nililengwalengwa na machozi. Nilihisi kuwa na aibu na kiburi. Nikakumbuka maneno ya Daudi, “BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? BWANA ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani?” (Zaburi 27:1). Huyu mtu wa Mungu mpendwa alikuwa kama Danieli katika tundu la simba, lakini moyo wake haukuwa na hofu kwa sababu Mungu aliahidi kufunga midoma ya simba. Hebu tukumbuke hayo tunapoomba. Tunahitaji kudai yote ambayo Mungu ameahidi katika neno lake kama riziki. Imani ni kumwamini Mungu kwa neno lake, na kumtarajia kutimiza yale amesema atatimiza. Imani Ni Kutafuta Je, kuna mambo unayoyatumainia, au kutamani, au kuota? Je, utafanyaje ili ndoto yako ikamilike? Kwanza, ondoa yale ambayo si mapenzi ya Mungu, bali ni tamaa yako tu. Pili, amini ahadi rahisi kama vile Wafilipi 4:19; “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachohitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.” Mungu hakuahidi kunipa mahitaji yangu yote; Ameahidi kunijazia kila ninachohitaji. Waebrania inasema kwamba imani ni “bayana ya mambo yasiyoonekana.” Ikiwa unahitaji lililo la haki, utawezaje “kuona” bayana ya hitaji hilo unalolikusudia kutimizwa? Riziki ya Mungu, Kimiujiza Nilikuwa ningali mgeni katika chuo kimoja, ambapo nilianza kuona Mungu akinipa riziki kwa njia ya miujiza. Nilihitajika kulipa kodi katika chumba nilichokuwa nikikaa pamoja na rafiki yangu mmoja. Tulikosa hela ya kulipa kodi kwa muda wa mwezi moja. Je, kodi hii ingetoka wapi? Tuliacha kuangaikia jinsi ya kupata fedha hizo. Tukaanza kuomba, kama jaribio la mwisho. Nilikuwa kijana wa miaka 19 ambaye alikuwa na matarajio ya kuwa mhubiri. Nikaomba Baba yangu aliye mbinguni anipe kodi!62 Wiki hiyo nilipata barua kutoka kwa Huduma Ya Misitu Ya Amerika. Barua hiyo ilikuwa na hundi ya kulipa kodi! Kwa kweli, hundi hiyo haikuwa ya kodi, bali ilikuwa yangu! Mwaka iliyopita, wakati wa kiangazi, niliitwa kuzima moto kule Oregon. Tuling’ang’ana kuzima moto usiku na mchana. Sikufahamu kuwa serikali hulipa watu kwa kuzima moto! Kwa hivyo, miezi mingi baadaye nikapata hundi kupitia posta. Ni juma hilo tu ambalo nilimwomba Mungu anitimizie hitaji ambalo lilikuwa ngumu! Imani ni kuona mahitaji yako yakitimizwa. Tunapomwamini na kumwomba Mungu, atajiheshimu kwa kutimiza neno lake. Rafiki yangu Mkristo, hatupati kwa sababu hatuombi. Amini na kumwomba Mungu ili akutimizie. Tunaweza kupata yote tunayohitaji ikiwa tutaamini kwamba Mungu ameshatutimizia. Kuona Ni Kuamini Kuna vikundi viwili vya watu ambao wana imani aina mbili tofauti. Kikundi cha kwanza ni cha “kuona ni kuamini.” Katika Yohana 20:25 Tomaso alisema, “Mimi nisipoziona…mimi sisadiki.” Ilimlazimu kuona Bwana aliyefufuka kabla kusadiki kwamba Bwana alifufuka. Tomaso alikuwa na imani iliyojengwa kwa hisia. Tunasema, “Bwana nipe ushindi, nami nitasadiki kuwa ninayo ushindi huo.” HIYO SI IMANI! Hiyo ilimsababisha Yesu kusema sadiki kwamba tayari umepokea, ndipo utapata. Yesu hakusema Tomaso alifanya vizuri. Alisema, “wa heri wale wasioona, na hawahitajiki kuona - wakasadiki” (Yohana 20:29, maneno ya mwandishi). Hiyo ni imani iliyo sambamba na maandiko. Tunahitaji kuondoka katika eneo la hisia, na kuingia katika eneo la Bibilia. Hapa ndipo tunagundua kwamba “imani ni kuona yale ninayotumaini.” Nikiwa na hakika kwamba nimepokea yale nimeahidiwa na Mungu, basi NITAONA ninayoyatumaini! Nasema tena, hii ni imani inayookoa. Hukumwona Yesu akifa na kufufuka siku ya tatu; uliamini neno tu. Hiyo ndio hakikisho uliyohitaji. Uliliamini neno, alafu ukamwona Yesu na kupata msamaha wake. Imani ni kufanya kama kwamba imetimika, wakati ambapo haijatimika bado, nayo itatimika! Imani ya Mwenye Ukoma Katika Luka 17, tunaona wenye ukoma 10 waliomwendea Yesu wakipaaza sauti kwa kusema, “Ee Yesu, Bwana Mkubwa uturehemu! Alipowaona aliwaambia, Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani. Ikawa walipokuwa wakienda walitakasika.” Mwenye ukoma aliyetakasika ni lazima ajionyeshe kwa kuhani ili ithibitike kwamba ameponywa kweli. Yesu aliwaambia waende kwa kuhani kabla kuponywa kwao. Je, kama wangalisema, “Bwana, hatuwezi kwenda kwa kuhani, kwani hatujaponywa bado”? Yesu, kwa kweli alisema, “fanya kama kwamba imetimika, ijapokuwa haijatimika bado, nayo itatimika.” Waliamini na kuelekea hekaluni, na “walipokuwa wakienda, walitakasika”…Kisha akawaambia, “imani yako imekuponya.” Ushindi Na Imani Waraka wa Kwanza wa Yohana 5:4 inafananisha ushindi katika maisha na imani kwa Mungu. “Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu.” Kwa hivyo, ushindi umepatikana tayari! Unao ushindi kwa kuamini kwamba Yesu tayari ameshinda (1Yohana 5:5). Labda utasema, “Je, unamaanisha kwamba nina ushindi dhidi ya kila shida kwa kuamini tu kwamba ninao ushindi?” Hiyo ni kweli! Ni kweli kabisa! Unasema, “Siamini hayo!” La, nawe hutapata ushindi kamwe! Amini hayo, nawe utapata ushindi! Imani ni ushindi! Yesu Kristo tayari ameshinda adui wote: yaani ulimwengu, mwili, na shetani (Waebrania 2:14; Wakolosae 2:14,15; 1 Yohana 3:8,4:4). Huna vita vingine vya kushinda. Yesu alishinda vyote miaka 2000 iliyopita. Ukiyaamini hayo, kuyasimamia imara, na kuyadai, basi ushindi wake utakuwa wako! Imani hii ya “Mungu ameshashinda vita” hutupa wokovu. Ni lazima uamini kwamba Mungu ameshatupatia wokovu ndani ya, na kupitia kwa Yesu Kristo. Aliyepotea dhambini lazima amjie Mungu na kupokea yale Mungu ametenda kwa kutubu dhambi, na kusema “Ahsante Yesu, ishatendeka.” Jinsi ulivyopata wokovu ndivyo utakavyopata ushindi na mwongozo wa kila siku. Ukiwa na imani, basi una bayana. Kwa hitaji lolote, amini kwamba ni yako, nawe utapata.63 Mungu akuzidishie katika maombi na kuamini kwako. “Bwana, tufundishe kuomba kwa imani, tukidai yaliyo yetu katika Kristo.” Michango 1. Tazama Luka 11:9-13 2. Sura ya 4, “Can a Christian Lose His Salvation?” inaongea kuhusua kuwa na hatia na msamaha kwa kinaganaga.



MBONA TUNAOMBA KATIKA JINA LA YESU?

 Kuomba katika jina la Yesu, kwa Muumini, ni njia ya kumfikia Mungu Baba. Imani yetu katika hilo jina takatif u hutuwezesha kuifikilia chumba cha enzi. Nilipokuwa kijana mdogo, wazazi wangu walianza kunifundisha dini kwa kuniorodhesha katika shule ya Wakatoliki wa Kirumi. Miaka yangu mitatu katika masomo yalitokana na msingi huo wa elimu. Ombi la kwanza ambalo nakumbuka kuomba ni ombi la kukariri “neema” wakati wa chakula nikiwa katika shule hiyo. Watoto wengi Wakatoliki hukariri ombi hili fupi kwa Mungu wakatika wa kwenda kulala, wakisema, “Tubariki, Ee Bwana, kwa vipawa hivi ambavyo tuko tayari kupokea kutoka kwa utajiri wako, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Amin.” Hilo ndilo lilikuwa ombi langu la kwanza. Ombi hili si mbaya. Sehemu ya mwisho katika ombi hilo ilinifurahisha sana, “kwa Yesu Kristo Bwana wetu.” Nilipoendelea kuwa mkubwa, nilianza kusikia wengine wakimaliza maombi kwa kusema “Katika jina la Yesu. Amin.” Nikaanza kuwaza na kuwazua “kwa nini” wanaomba “katika jina la Yesu.” Nikawa mtu mzima kabla moyo wangu kukubali ukweli wa maneno hayo. Ombi Rahisi Yesu alikuwa akiwapa wanafunzi wake funzo kamili kuhusu utiifu, Roho Mtakatifu na maombi katika Yohana 1:16. Katikati ya mafundisho hayo, mara tatu Yesu aliwaambia wanafunzi wake kuomba Mungu “katika jina langu”: “Amin, amin, nawaambia, mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu. Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu” (Yohana 16:23,24). Kristo tayari ameshawishi jambo hili katika sura ya 14, na akarudia katika sura ya 15 (Yohana 14:13,14 na Yohana 15:16). Kurudia huku kulimaanisha kutilia mkazo kanuni hii rahisi: kukaribia moyo wa Mungu ni kupitia kwa jina la Mwanawe. Kukosa Kuomba ni Kukosa kupokea Fundisho hili lilikuwa la kipekee, na geni kwa wanafunzi wa Kiyahudi. Katika historia yao, hawakuwahi kumwomba Yehovah Mungu katika jina la mtu! Ndio sababu Yesu alisema, “Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu” (Yohana 16:23). Hili ni fundisho linalobadilisha. Ni kiini cha theologia ya Kikristo. Yesu anasema kwamba kuna njia jipya ya kufika kitini pa enzi kwa Mungu, ambalo halijapitiwa na mtu mwingine awaye yote. Kuna nambari ya siri ya simu mpya isiyojulikana na yeyote, ya kwenda kwa kiti cha enzi cha Mungu. Hebu piga simu hiyo! “Hata sasa, hamjamwendea Baba kwa jina langu. Sasa fanya hivyo naye Baba yangu atakupa kila hitaji lako,” asema Bwana Yesu. Hili laonekana kuwa kinyume, lakini sivyo kamwe! Hadi wakati huo, hakuna aliyewahi kumwomba Mungu “kwa jina la Yesu.” Labda hii haikufanywa na wafuasi wa kwanza wa Kristo hadi baada ya Pentekote. Iligharimu uchochezi wa Roho Mtakatifu, aliyekuwa akiishi ndani yao, kuwafanya kuomba katika jina la Yesu. Hivi sasa watu wengi wanaomba maombi kila siku, yakiwa maombi ya kukaririwa, na kuyamaliza kwa “jina la Yesu” bila kumaanisha. Kanisa likifahamu uwezo na nguvu iliyoko katika jina la Yesu, basi maombi yetu yataleta Pentekote mara nyingine. Kanisa la kwanza lilichochewa na imani katika hilo jina la Yesu. Jina hilo litaweza kuwasha imani na moto katika moyo wako ikiwa utatambua kwa nini Mungu anaheshimu jina la Yesu.66 Katika Jina Langu Mbona uombe katika jina la Yesu? Mbona si Budha, au Allah, au mwalimu mwingine shupavu wa dini, au nabii? Kuomba katika jina la Yesu ni kukubali malipo ya dhambi zetu ambazo Kristo alilipa pale msalabani ili tuweze kuifikia uwepo wa Mungu. Kama vile Wayahudi hawangeingia Patakatifu bila gharama ya damu (kwa Yom Kippur), ndivyo mwenye dhambi hawezi kuingia katika uwepo wa Mungu bila damu iliyomwagika ya Yesu Kristo. Ni kupitia kwa kifo chake, kuzikwa kwake, kufufuka kwake, na kupaa kwake mbinguni ndipo tunaweza kuwa na uhusiano wa Baba-Mwana pamoja na Mungu. Mwenye dhambi asiyekuwa na mwokozi hana tumaini la msamaha wa dhambi. “… Vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo…kwa sababu Kristo hakuingia patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu” (Waebrania 9:22,24), na “Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu” (Waebrania 10:19). Hiyo ndio sababu tunasogelea kiti cha enzi cha Mungu katika jina la Yesu. Tunaomba kwa kuwa yeye ni mwadilifu. Ni kama kumwambia Mungu, “Mungu, siombi kwa sababu ya jinsi nilivyo ama kwa ajili ya uzuri wangu. Naomba kwa sababu Yesu alisema nije kwako na kukuambia amenituma. Alisema utajibu maombi yangu kwa ajili yake, wala si kwa ajili yangu.” Ghala La Baba Ukienda sokoni na kununua vyakula vyote unavyohitaji nyumbani mwako, na mahitaji mengine. Ukaenda kulipa ukiwa na vikapu kumi vilivyojaa vyakula, na vitu vingine ulivyonunua. Muuzaji akahesabu gharama ya vitu vyote ulivyonunua. Unagundua kwamba vimegharimu pesa kiasi kikubwa. Muuzaji anakuangalia kwa mshangao na kukosa kukuamini. Tuseme labda kiasi cha pesa unazohitajika kulipa ni $5000. Kisha unamwambia huyu muuzaji, “Hebu nipe cheti hicho niweke sahihi.” Anapigwa butwaa na kukuuliza, “Uweke sahihi? Kwani unafikiri wewe ni nani, mwenye soko?” Alafu unamjibu, “La hasha, kwa hakika mimi si mwenyewe, lakini baba yangu ndiye mwenye soko. Mimi ni mwanawe wa pekee. Nitaurithi mali yake yote.” Yesu alimaanisha hivyo alipotuambia tuombe kwa jina lake. Yote ya Mungu Baba pia ni ya Mwanawe wa pekee. Yesu ndiye mwenye soko, akiwa pamoja na Baba yake. Amemwambia Baba yake kwamba tunaweza kuweka sahihi cheti katika jina lake. Baba anaheshimika kujibu maombi yako katika jina la Yesu, kama vile Kristo mwenyewe angeweza kuomba. Muumini ameshikamanishwa na Kristo kiasi cha kwamba kuomba kwetu ni kuomba kupitia kwa Roho wake aliye ndani yetu. Huu ni ukweli wa ajabu! Kutumia Fimbo Ya Mungu Tumetazama Mwanzo 17, na “fimbo ya Musa ya Mungu.” Tumeona kwamba fimbo yetu ni imani katika jina la Yesu. Katika Marko 16:17, Yesu ametuambia tutumie jina lake hata kwa kuwatorosha mapepo. Inasisimua kuona wanafunzi wa Yesu wakitenda yale Yesu alihubiri. Baada ya Pentekote, Petero na Yohana walienda hekaluni kuomba. Yesu amerudi kwa Baba, lakini Roho Wake sasa anakaa ndani yao. Wakiwa nje ya hekalu, Petero na Yohana walikutana na kilema ambaye alikuwa akiomba pesa kutoka kwa wale waliokuwa wakienda hekaluni kusali. Petero aliwaza akiwa ameshurutishwa na Roho wa Yesu aliyekuwa ndani yake: “Petero, tumia fimbo yako. Tumia jina langu. Mwombe Baba. Ona muujiza.” Petero, kwa msukumo, akamwambia yule kilema, “Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende.” (Tazama Matendo 3:1) Kwa hivyo, kwa mara ya kwanza mmoja wa wanafunzi kumi na wawili wa Yesu alifanya kitu. Waliamini maneno ya Yesu na kutumia jina lake. Walisogelea eneo la miujiza. Baadaye Petero na Yohana walipoulizwa na viongozi wa Wayahudi jinsi huyu kilema alivyoponywa, kwa furaha walijibu, “na imani67 ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele yenu ninyi nyote” (Matendo 3:16). Iweke imani yako katika jina la Yesu na Mungu ataweka jina lake, na nguvu zake, katika imani hiyo.


VITA VYA KIROHO NI NINI? “

Shetani ana nguvu za kushikilia jibu kwa muda fulani ili kuchelewesha matokeo. Hana nguvu za kuzuia matokeo kabisa, ikiwa mtu ataelewa na kuomba kwa uthabiti pasipo kukoma. Maombi mazito yanastahili kuelekezwa dhidi ya shetani.” S.D. Gordon, Quiet Talks on Prayer Maisha ya Kikristo ni maisha ya vita. Mkristo ni sehemu ya mng’ang’ano wa milele kati ya mema na mabaya. Kuwa mwana wa Mungu ni kupigana dhidi ya nguvu za giza siku zote za maisha yako. Ni watu wachache sana ambao wanafahamu mgongano huu wa kiroho. Washirika wengi wa kanisa hukaa kana kwamba adui amekufa na wao hatimaye wamefika Sayuni. Mtu mmoja alisema kuwa meli ya zamani ya Sayuni si merikebu ya kustarehe ambapo tunasafiri kwa furaha hadi ufuoni mwa mbinguni, bali ni merikebu ya vita ambapo tunamkabili adui Shetani kila siku. Vita hivi vya kiroho ni nini basi? Adui ni nani ? Silaha zetu ni zipi? Vita hivi hupiganwa vipi? Tutatafuta majibu kwa hayo maswali kutoka kwa neno la Mungu. Adui Paulo, akiandikia waumini wa Efeso, anaongea kuhusu vita vya kiroho, na asili ya adui: “ Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka; juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho” (Waefeso 6:10-12). Shetani ndiye adui wetu mkubwa. Yeye ni malaika mkuu aliyeanguka ambaye moyo wake umejaa chuki dhidhi ya Bwana Yesu na ufalme wake. Shetani ni mtawala wa roho katika ufalme wa giza. Anaongoza “nguvu za uovu wa kiroho ulimwenguni.” Kuamini, au kutokuamini kwako kwa shetani au nguvu za pepo ina mwelekeo katika ushindi wako, au kushindwa kwako katika pambano. Kujifanya kwamba hakuna adui ni kuhakikisha kushindwa kwako. Watu wasioamini kwamba shetani yuko wana Shetani ndani yao kuliko mtu yeyote mwingine! Vita vya “Roho” Tazama kwamba maandiko yanaeleza asili ya vita hivi kuwa vya “kiroho.” Hatupigani katika ulimwmengu wa mwili - “kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama.” Hivi ni vita visivyoonekana dhidi ya maadui wasioonekana - Shetani na mapepo, au washirika wake. Waumini wengi wanapoteza vita hivi kimakosa kwa sababu hawajajitokeza kwa vita. Shetani anashinda bila kupingwa kwa sababu wakristo wanakataa kupigana katika hivi vita vya “roho.” Tilia mkazo maneno haya: hivi vita ni vya roho, wala si vita vya mwili. Majengo na makisio ya makanisa hayawezi kushinda vita hivi. Kamati na fadhili za kanisa haziwezi kushinda “uovu wa kiroho katika ulimwengu wa roho.” Jambo ambalo lazima tuelewe ni kwamba matatizo yetu hayana asili kwa yale tunayoyaona, ijapo yanaonekana kuwa hivyo. Kuna shida ya ndani kwa roho katika kila tatizo la mwili. Mwili ni chombo tu kinachotumiwa na roho. Mathayo 16: 21-23 inatuonyesha ukweli huu. Baada ya Yesu kutabiri juu ya kifo chake kule Yerusalemu, Simoni Petero alimwambia, “Hasha Bwana, hayo hayatakupata” (tazama kifungu cha 22). Hebu tazama jinsi Yesu alivyomkemea “nenda nyuma yangu Shetani…” Bwana wetu hamkemei Petero, bali anakemea nguvu za pepo zilizoko nyuma ya maneno ya Petero. Shetani alizumgumza kupitia kwa mawazo na sauti ya Petero. Tatizo halikuwa Petero, bali nguvu zilizokuwa nyuma yake, yaani shetani. Kila mara tatizo haliko katika yale yanayoonekana, bali katika nguvu za roho zitendazo kazi nyuma ya matendo yanayoonekana katika mwili.70 Kila siku tunapigana vita vya roho, ambavyo havionekani. Katika Waefeso, Paulo anaeleza “kushindana” kwetu. Tafsiri ya mfalme Yakobo (The King James Version) inatafsiri hili neno kama “mweleka,” ambalo lina maana ya kupigana mkono kwa mkono. Vita hivi ni vita vyako binafsi. Kuokolewa ni kujihushisha katika kushindana dhidi ya nguvu za ulimwengu wa giza. Kama Mkristo unahusika; upende, usipende. Ni jambo la kuhuzunisha kwamba wakristo wachache wana habari juu ya vita hivi. Shetani ana juhudi kumshinda kila Mkristo. Ni asili yake kumshinda Mkristo pasipo Mkristo kutambua uwepo wake. Silaha za roho Ikiwa tutapigana vita vya roho, basi tutahitaji silaha za kiroho. Silaha zetu lazima ziwe na uwezo wa kukabiliana na adui wetu pamoja na mbinu zake . Paulo anaeleza juu ya silaha za Mkristo anaposema: “Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kishindana siku za uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. Basi simameni hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tapatao kwa injili ya amani: zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote ya moto wa yule mwovu. Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa roho ambao ni neno la Mungu (Waefeso 6:13-17). Hii ni picha ambayo ni mfano unaotuhusu; wewe na mimi. Tumevalishwa mavazi ya vita, pamoja na silaha kamili tukiwa tayari kabisa kwa vita. Mshipi wa kweli, dirii ya haki, viatu vya vita, ngao ya imani, chepeo ya wokovu, na upanga wa roho ndizo silaha zako. Mavazi ya silaha za ajabu! Umeimarishwa kwa vita vya mkono kwa mkono na Shetani mwenyewe. U tayari; nionyeshe vita, na kunipeleka katika msitari wa mbele. Hebu tuvianze vita basi! Sawa. Hapa kuna vita. Sikiliza maneno ya Paulo katika aya inayofuata: “kwa sala zote na maombi; mkisali kila wakati katika roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote” (Waefeso 6:18). Maombi ndio vita Sasa, je waweza kuzidisha hayo? Umevalishwa, na kutayarishwa kupigana vita. Naye Paulo anakuambia uombe! Omba? Sawa kabia, omba. Hata ingawa inavunja moyo, maombi ndio vita. Silaha ni maandalizi tu ya maombi. Mwanajeshi Mkristo ni mwanajeshi wa maombi. Vita hivi vya roho hupiganwa na jeshi liendalo kwa magoti. Adui wetu ni wa rohoni. Hivyo basi ni lazima tutumie silaha kuu za roho dhidi yake. Maombi ndio njia ya kuwa katika pambano la kiroho. Hapa ndipo makanisa mengi na viongozi Wakristo wanakosa wakiwa vitani. Tumedhani kwamba matatizo yetu yanatokana na ukosefu wa fedha, rasilmali, au utaratibu. Kama kanisa letu lingekuwa na hili au lile, basi tungelimfanyia Mungu mambo makuu. Mungu utusaidie! Hatuwezi kumshinda shetani kwa majengo, makadirio, au makombora. Tunaweza tu kumshinda mwovu kwa nguvu za maombi pekee. Mungu ametumia mbinu hiyo wakati wote. Mweneza Injili na Uamsho Mimi ni mweneza injili. Nimehubiri katika mamia ya makanisa, nikizunguka ulimwenguni. Ni mara chache sana ambapo kanisa limeamini kwamba maombi ndio vita. Ili kujiandaa kwa ajili ya kuhubiri juma nzima, mchungaji wa kadiri huweka matangazo kwa karatasi, kwa runinga, na mabango katika sehemu za biashara, akitangaza mkutano wa hadhara wa injili ujao. Atatumia sarakasi na vifaa mbalimbali kuvuta watu wahudhurie mkutano huo wa injili. Haya yote ni mema na sawa, bali ni juhudi za mwili. Lakini vita, kwa kweli, ni vya roho! Ni mara chache sana ambapo kanisa limevaa silaha na kwenda vitani katika maombi. Naongea juu ya maombezi ya kweli. Aina hii ya maombi hutufanya “kuingia kwa mapango” na “mweleka” wa mkono kwa mkono mpaka ushindi upatikane. Ni rahisi kwenda kumsikiliza mwinjilisti akihubiri. Lakini ni vigumu sana kudumu katika maombi, ukiamini. Tunashangaa kwa nini Mungu hatembei kwa jinsi ya ajabu miongoni mwa watu kupitia kwa Roho wake, hali tumeiacha hatua hii muhimu ya kwanza. Miaka kadhaa zilizopita nilihubiri katika nchi ya Rumania, ambayo ni nchi ya kikomunisti. Tulihubiria umati upatao watu kati ya elfu tatu na elfu nne kila usiku kwenye jumba ambalo linaweza kukaliwa na watu mia nane tu. Hakukuwa na matangazo kwenye magazeti, runinga, na mabango. Mkutano hao ulikosa kuchochewa, kwa sababu ni hatia katika nchi ya kikomunisti kuchochea dini kwa kuutilia mkazo. Kwa hakika ilikuwa baraka isiyo na kifani! Nilikuwa karibu kutamani dini iwe hatia katika nchi za magharibi. Basi pengine hatungeegemea mwili, bali tungelazimika kumtegemea Bwana. Katika Rumania, waumini hukutana na mfalme wa giza kila71 siku. Lazima wang’ang’ane ili waishi. Maombi ndio njia moja wanayotumia kama silaha kuu ya kurarua ngome za shetani. Maelfu wanamgeukia Kristo licha ya upinzani mkubwa na mateso. Maombi ndio vita. Tunapokosa kuomba, tunapoteza ushindi kimakosa. Maombi na Uinjilisti Uinjilisti ni vita vya kiroho vinavyoshindwa kwa maombezi. Mwenye dhambi anapozaliwa katika ufalme wa Mungu, hakika ni kwamba mtu mwingine alimwombea. Mtu alisimama “katika pengo” kwa ajili ya nafsi hiyo iliyokuwa imepotea. Ni kwa kumfukuza adui kutoka kwa uwanja wa vita wa moyo wa mwanadamu ndipo hutokea uhuru kwa mwenye dhambi kuitikia neema ya Mungu. Kuhubiri, kushuhudia, ratiba, na kazi zote za kanisa zinafaa na kuhitajika; lakini hivi si vita vyenyewe. Shetani hutuogopa sana tuchukuapo silaha za roho na kuzitumia dhidi yake katika maombi. Hapo mapema tulitaja mfano wa Musa na Yoshua wakipigana na Amaleki. Vita hivi vimeandikwa katika kitabu cha Kutoka 17: 9-16. Yoshua alipokuwa akipigana vita kule nyikani, Musa alikuwa akimwombea kule mlimani. Musa allikuwa akipigana vita vya kweli dhidi ya nguvu za roho za uovu, ambazo zilimtia nguvu mfalme wa Amaleki, aliyekuwa mwabudu sanamu. Musa anamwombea Yushua, ambaye anazidi kushinda dhidi ya Amaleki. Kwa kupigana vita vya roho, Musa alirahisisha ushindi wa Yoshua dhidi ya Amaleki (Kutoka 17:13). Shetani hupinga Maombi yetu Mwana wa Mungu aliyejazwa na roho anapoanza kuomba kwa thati, shetani hutetemeka. Anajua maombi kama hayo yanatokana na Mungu, wala si ya kawaida. Yanamuusisha Mungu katika pigano. Shetani hawezi kushinda dhidi ya silaha kama hiyo. Hii ndio sababu Shetani atapinga vikali maisha yako ya maombi. Je umewahi kugundua jinsi ilivyo vigumu kutumia muda wako katika maombi? Tunapata muda wa kuhusika kwa ratiba nyingine za “dini,” kama vile kuhudhuria kanisa, kuhudhuria darasa la Bibilia, na kushuhudia mara kwa mara. Lakini tunapata pingamizi katika kukutana na Mungu kwa maombi. Hii ni kazi ya Shetani. Akiweza, atazuia maisha yako ya maombi. Elewa kwamba maombi ni vita! Daktari Stephan Alford alikuwa mchungaji wa kanisa la Calvary Baptist katika jiji la New York kwa miaka mingi. Wakati moja nilimsikia akieleza jinsi Shetani alivyompinga katika maisha yake ya maombi. Alisema kwamba kwa miaka mingi hangeweza kuelewa kwa nini mawazo yake yalitangatanga ovyo ovyo wakati wa kuomba. Kila mara alipata mawazo maovu ya chuki au tamaa yakipenya katika maombi yake. Mwishowe alitambua kuwa ilikuwa ni vita. Alitambua kwamba mawazo haya yalikuwa “mishale ya moto” iliyolengwa kutoka kwa uta wa Shetani ili kuharibu mombezi na maombi yake. Kuomba ni zaidi ya kukutana na Mungu. Ni wakati wa kumkabili adui. Haimaanishi kwamba katika maombi tunaongea na Shetani. Mungu asituruhusu kamwe! Yupo kutupinga, na ni lazima tukabiliane naye. Katika sura lingine, tunazungumzia hili swala la kukabiliana na Shetani kwa “kufunga na kufungua,” kama iliyotajwa katika Mathayo 18:18. Hebu sasa tufahamu kwamba Shetani hupinga maombi yetu. Anaweza hata kuchelewesha majibu kwa maombi yetu. Mfano dhahiri inayoonyesha kwamba maombi ni vita vya kiroho iko katika Agano la Kale. Danieli 10:13 inasimulia kijana nabii Danieli akichukua majuma matatu katika kufunga na kuomba. Baada ya muda huu wa makabiliano makali ya kiroho, Malaika anatokea, akiwa ametumwa kama majibu kwa maombi yake. Mungu hajawahi kutuma Malaika ninayeweza kumwona akiwa na majibu kwa mojawapo ya maombi yangu. Hata hivyo sijawahi kuomba na kufunga kwa dhati kama alivyofanya Danieli. Malaika alimwambia Danieli jambo la kupendeza, akisema, “Usiogope Danieli kwa maana tangu siku ile ya kwanza ulipotia moyo wako ufahamu, na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, maneno yako yalisikiwa, nami nimekuja kwa ajili ya maneno yako” (Danieli 10:12). Fahamu hili andiko “tangu siku ile ya kwanza.” Malaika alianza kumwendea Danieli tangu siku ya kwanza alipoanza kuomba. Kwa nini ilimchukua majuma matatu kumfikia? Malaika anaeleza maana ya kuchelewa kwake katika aya inayofuata: “Lakini mkuu wa ufalme wa Uajemi alinipinga siku ishirini na moja, bali, tazama huyo Mikaeli, mmoja wa hao wakuu wa mbele, akaja kunisaidia…” Hili ni jambo linalotatanisha! Danieli anaomba. Lakini katika ulimwengu usioonekana, vita vinaanza. Mungu anatuma Malaika (mjumbe) kumjibu Danieli, bali mkuu wa Uajemi (jina lililopewa Shetani hapo72 kale), anampinga. Kwa siku ishirini Malaika alipigana na Shetani mwenyewe, kwa sababu Danieli alikuwa akiomba na kufunga! Malaika hakuwa na nguvu kumzidi Shetani. Mungu akawajibika kumtuma Mikaeli, ambaye ni malaika mkuu, kumaliza mapigano. Ushindi ukapatikana. Shetani alikuwa akizuia jibu kwa maombi ya Danieli. Ama uchukue maandiko haya kuwa mfano tu, au ukweli, jambo moja li wazi kwamba kuomba hutuweka katika ulimwengu wa roho ambapo vita kamili vipo. Maombi ni vita, na kwa hivyo, Mungu anaitilia maanani hata kumhusisha malaika. Maombi yako yanaweza kuchochea jeshi la mbinguni yakiombwa kwa imani na uwazi. Maandiko yanatuambia Malaika wa Mungu ni Roho watumishi wanaotumwa kuwahudumia wale wanaogusa yasiyo ya kawaida katika maombi yao (Waebrania 13-14). Mwito wa kujiami Kiini cha huduma ya kanisa ni maombi halisi. Kuomba ni zaidi ya kushukuru Mungu, au kumuuliza vitu. Maombi ni mwito wa kujiami. Ni jambo zito. Kupitia kwa maombi, tunagusa mbingu na kushambulia kuzimu. Waliodhaifu moyoni, au katika imani hawawezani nalo. Mambo yaliyosalia katika kitabu hiki yanahusika na “mambo ya ndani” ya maombezi na vita. Waweza kufikiri tayari tuko ndani sana katika masomo haya, lakini bado. Tujiunge tena na Paulo katika ombi lake kwamba “macho ya moyo wako yatiwe nuru.” Bwana, tufundishe kuomba.73 KUWA SHUJAA WA MAOMBI Kuna upungufu mkubwa sana kwa utumikaji wa maisha iliyojazwa na roho mtakatifu ikiwa maisha hayo hayatoi ujuzi muhimu katika kiwango cha maombi. --Arthur Wallis, Pray in the Spirit Kila Mkristo ana haki na uwezo wa kuomba. Ingawa hivyo, kila Mkristo hajajiandaa kuingia katila vita vya roho. Mambo ya ndani ya uombezi na maombi yametengewa walio na ujuzi katika mambo ya roho. Kama vile mwanajeshi mchanga anavyoenda kujiunga na kikosi kwa mafunzo, mkristo ni lazima “avae silaha zote za Mungu” kabla ya “kuwa hodari katika Bwana na nguvu za ukuu wake” (Waefeso 6:11,10). Kikosi Cha Mafunzo cha Maombi Silaha ambazo Paulo anazungumzia katika Waefeso 6: 1-17 kwa hakika ni maandalizi ya maombi. Kwa sababu maombi ni mahali ambapo tunakutana na Mungu na pia kukabiliana na Shetani, lazima tujiandae kwa kuvaa silaha zote za Mungu. Mtume Paulo anatupa shauri la kweli kwa kujiandaa kwa huduma ya maombi, kwa: “Kusimama imara.” Kutumia “upanga wa roho.” Kuomba “katika roho.” Omba Ukisimama Imara Tunahimizwa kusimama imara dhidi ya “mbinu za shetani” (Waefeso 6:11) kwa kuvaa silaha zote za Mungu. Kile Paulo anamaanisha ni kwamba msingi wetu wa maombi lazima uwe kazi iliyomalizika ya Kristo. Ushindi wetu ni ule ambao Yesu alipata msalabani. Pia, ni lazima tuishi maisha ya utakatifu na utiifu mbele za Mungu. Tumevalishwa dirii ya haki na viatu vya kuonyesha utiifu wetu, ya kuenda anapotuamuru kuenda. Kwa hivyo tunaomba tuwe katika hali itupayo nguvu. Tunaweza kuomba kwa ujasiri. Katika sura itakayofuata tutaona mengi kuhusu ushindi wetu juu ya adui tutakapozungumza juu ya silaha za vita vyetu. Omba Ukiwa na Upanga wa Roho “Tena ipokeeni… upanga wa roho, ambao ni neno la Mungu” (Waefeso 6:17). Shujaa wa maombi anayefaa hutumia silaha yake ya neno la Mungu. Katika maisha ya maombi ya Mkristo, upanga wa roho ni silaha ya kushambulia adui. Watu wanaoomba kwa ukamilifu hutumia Bibilia katika maisha yao ya maombi. Nguvu katika maombi huambatana na ufahamu wa Bibilia. Je unafahamu jinsi ya kutumia neno katika maisha yako ya maombi? Mtajie Bwana Neno lake Katika Maombi Tumia neno unapozungumza na Mungu. Kumbuka Bibilia ni kitabu cha ahadi ya Baba kwa watoto wake. Tumtarajie Mungu kutimiza neno lake. Mkumbushe katika imani, na kumtajia katika maombi. Kila ninapoomba, maandiko huchukua nafasi kubwa. Mara nyingine naanza muda wangu na Mungu kwa kumsomea neno lake. Napenda sana kusoma kitabu cha Zaburi kwa sauti katka kuomba kwangu. Thamani ya kushikilia na kutaja neno hadi kwenye kiti cha enzi ni kwamba ahadi za Bibilia ni kama “deni” kutoka kwa Mungu hadi kwetu. Sisi ni warithi pamoja na Kristo. Kwa hivyo chochote ambacho ni cha Kristo, ni chetu pia. Kuomba na upanga ni kudai haki za uzaliwa wako upya. Muumini huja kwa kiti cha enzi cha Mungu na kusema “Baba, mimi mtoto wako. Ulisema utakutana na mahitaji yangu yote (Wafilipi 4:19), na nitakudai kwa neno lako leo.”74 Taja Neno Dhidi ya Shetani Unapoomba, tumia upanga wa roho dhidi ya adui. Shetani huchukia na kuogopa ukweli wa neno la Mungu. Litumie dhidi yake. Neno humkata kwa vipande vipande! Upanga wa neno una uwezo wa kumtorosha Shetani kutoka vitani. Kuna nyakati katika maombi ambapo Shetani atakushambulia kwa mawazo maovu, tamaa, au uharibifu. Atafanya vyo vyote katika nguvu zake kuzuia wakati wako wa maombi. Tumia neno dhidi yake. Isaya 54:17 inasema, “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa…” Shetani anajua yeye ni adui aliyeshindwa, bali wakati mwingi yeye hujigamba. Lazima umjulishe kwamba unafahamu kushindwa kwake. Mtajie neno. Mara kwa mara namkemea usoni kwa kusema: “Shetani, wewe ni mwongo.” Bibilia inasema “... Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za ibilisi.” Shetani hawezi kuvumilia ukweli wa neno la Mungu. Atatoroka. Taja Neno ili Kuinua Nafsi Kuna nyakati ambapo utaona ugumu kuomba. Taja neno kwa sauti, kwako na kwa Mungu. Kila mara Roho Mtakatifu atatumia maandiko kuinua nafsi yako juu, ili kutayarisha moyo wako kwa maombi na uombezi. Omba Katika Roho Paulo, hatimaye, anatuambia tuingie katika vita vya roho kwa “kuomba wakati wote katika Roho.” Wewe na mimi hatuwezi kuwa mashujaa wa maombi bila maandalizi haya matatu. Tunajifunza kuomba tukisimama imara kwa kazi iliyomalizika ya Kristo, tukiomba na neno la Mungu kama silaha yetu ya kushambulia, na kuomba katika nguvu na ujazo wa Roho Mtakatifu. Maombi ya kweli ni yale yaliyojawa na uwepo wa Roho Mtakatifu. Ni maombi yaliyojazwa na kudumishwa na pumzi ya Mungu. Tunaponyenyekea chini ya uwepo wa Roho Mtakatifu ndipo tutakapoweza kuwa na tumaini ya kuwa mashujaa watakatifu wa maombi. Tumetaja upanga wa neno la Mungu kuwa silaha katika maombi. Lakini sasa ningependa tuangalie silaha zingine mbili za ajabu katika maombi, ambazo ni Msalaba, na kutambulishwa na Kristo.75


KUTUMIA SILAHA ZA VITA VYA ROHO 

Kutoka kwa nguvu hadi nguvu endelea: Ng’ang’ana, pigana, na uombe; Kanyagia chini nguvu za giza, Na ushinde katika siku iliyopiganwa vema. - Charles Wesley. Kuomba kunaweza kuchuchukua mitindo mingi, kama vile kuabudu, ambapo tunawasilisha sifa kwa Mungu. Maombi yanaweza kuwa kazi! Ombi ambalo ni gumu ni lile la uombezi kwa ajili ya watu wengine. Maombi pia yanaweza kuwa vita. Maombi yatamkabili adui Shetani yakiombwa kwa Roho kutoka moyoni. Kwa sababu kuna nyakati ambapo maombi ni vita vya roho, tutahitaji silaha za roho ili kushinda “uovu wa roho katika ulimwengu wa roho” tukikabiliana nazo. Mpango Wa Vita Kila Mkristo anahitaji ufahamu wa msingi kuhusu jinsi ya kupigana vita vya roho, na silaha zinazohitajika ili kumshinda adui. Wakati moja wanafunzi wa Yesu walikutana na kijana aliyepagawa na pepo lakini wakashindwa kukemea pepo hilo. Baba yake akamleta kwa Yesu. Mara moja Yesu alikemea yule roho mchafu. Baadaye wanafunzi walipomuuliza kwa nini hawakuweza kukemea pepo huyo, Yesu alijibu kwa kusema: “Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amini, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. (Alafu maandiko mengine huongeza maneno yafuatayo: Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga) (Mathayo 17:20-21). Tumefananishwa sana na hao wanafunzi wa kwanza. Tumekosa nguvu dhidi ya nguvu za mapepo zinazotukabili kila siku. Tuna vifaa vinavyotuwezesha kusongeza hayo milima, kama tungekuwa na imani na ufahamu wa jinsi ya kutumia vifaa hivyo. Hebu tuangalie silaha za Mungu alizotupatia ili tuweze kuishi katika ushindi, na kuomba kwa nguvu. Silaha Za Msalaba Katika Waefeso 6:11-14, Paulo anatuambia kwa kurudiarudia, “simama imara.” Kwa maneno mengine, anasema “shikilia ushindi wako.” Kwa kusema “ushindi” alikuwa akimaanisha ushindi ambao Yesu alitushindia alipokufa na kufufuka tena. Kalivari ilikuwa uwanja wa vita vya roho ambapo Yesu alimshinda adui na kumtekea Mungu na ulimwengu uliopotea eneo ambalo Shetani alikuwa amemiliki. Ushindi wake alipata dhidi ya ulimwengu, mwili, na Shetani. Katika kitabu cha Wakolosai 2:13-15, tunaona mifano miwili ya ajabu yanayoeleza ushindi wa Yesu msalabani, na kaburi lililo tupu. Paulo anasema, “Na ninyi mlipokuwa mmekufa kwa sababu ya makosa yenu na kutokutahiriwa kwa mwili wenu, aliwafanya hai pamoja naye, akiisha kutusamehe makosa yote; akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa uadui kwetu: akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo. “Hati ya makosa” ambayo Paulo anamaanisha ilitokana na sheria ya Warumi katika siku za Paulo. Yesu alipoangikwa msalabani, askari waligongomea juu ya kichwa chake maneno yaliyosema “mfalme wa76 Wayaudi.” Haya maandishi yalikuwa hati ya deni ambayo Yesu alishtakiwa kisheria na wale waliomshtaki. Katika enzi za Warumi, ilikuwa kawaida hukumu ya sheria kuletwa mbele ya hakimu. Hakimu alitoa hukumu ya kuwa na hatia, ama kutokuwa na hatia. Kama mshtakiwa alipatikana na makosa, alipewa hati ya deni ambayo ilipachikwa kwenye mlango wa kijumba cha gereza alimowekwa, ama hati hiyo ingegongomewa msalabani jinsi walivyomfanya Yesu. Kwa hivyo wote wangeona na kujua hukumu ya sheria kwa mshtakiwa. Yesu alishtakiwa kwa kuhujumu serikali ya Kirumi, na kujionyesha kama mfalme wa Wayahudi. Hiyo ilisababisha kuwekwa kwa maandishi hayo juu ya kichwa chake. Paulo anasema katika Wakolosai 2:14 kwamba Yesu alikufa na akaifuta ile “hati ya makosa … iliyokuwa ya uhasama kwetu.” Fahamu kwamba hii hukumu, au hati hii ya deni ilikuwa “dhidi yetu,” wala si dhidi ya Kristo. Ni deni tuliokuwa nalo ambalo Yesu alilipa kwa kifo chake. Shetani ni mshtaki wetu. Ana orodha ya dhambi ya kila mwenye dhambi. Analeta mashtaka yake dhidi ya mwenye dhambi mbele ya kiti cha enzi cha Mungu. Shetani hutoa hati yake ya makosa mbele ya Mungu. Sisi wenye dhambi tumehukumiwa kuwa na hatia, na “mshahara wa dhambi ni mauti” (Warumi 6:23). Sasa ni kitu gani ambacho Mungu alitufanyia? Alichukua hati ya dhambi na kuuweka msalabani. Kisha akaifutilia mbali na damu ya mwanawe wa pekee, Yesu Kristo. Mungu alimaliza kesi yetu nje ya mahakama, kwa msalaba. Silaha Pekee ya Shetani Ukweli tunayoweza kutumia ni kwamba silaha ya pekee ambayo Shetani anatumia dhidi yetu ni dhambi zetu. Yesu alifuta, na kuziondoa kabisa dhambi zetu. Shetani hana la kudai kwetu kisheria. Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi za ulimwengu wote (1 Yohana 2:2). Hivyo basi alimshinda Shetani kwa kifo chake msalabani. Huo ndio mfano wa kwanza kutumiwa na Paulo katika Wakolosai 2. Wakolosai 2:15 Mfano wa pili unatokana na ushindi wa jeshi la Kirumi. Yesu “alimwaibisha” Shetani wazi wazi kupitia kwa msalaba wake. Hii “aibu ya wazi” ilitumiwa na Kaisari katika ushindi wake vitani. Warumi waliposhinda jeshi lolote, waliwatia aibu kwa kuvua mavazi ya mfalme, au jemadari wake. Kisha walilazimisha mfalme huyo, au jemadari pamoja na jeshi lake lote, kufuata gari la vita la Kaisari (ama Jemadari wa Kirumi) wakiwa wamefungwa minyororo, bila silaha zezote. Warumi waliporudi Roma pamoja na mateka wao waliokuwa wamefungwa kwa pingu, mateka walidhihakiwa na watu wakitembea huku wamechoka. Walitembea nyuma ya Kaisari aliyekuwa akionyesha ushindi mkuu. Yesu alimwaibisha Shetani lini? Msalabani! Yesu alimweka aibu wazi wazi lini? Alipofufuka kutoka kaburini! Yesu aliposhinda kifo, “aliivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo” (Wakolosai 2:15). Shetani hana silaha za kutumia dhidi ya Mwana wa Mungu aliyenunuliwa kwa damu. Kutumia Msalaba Kama Silaha Hii inahusiana vipi na vita vya roho? Vita hivi vilipangwa katika kila njia. Tumeshinda tayari. Vita vinakamilika tunapoomba! Shetani hana dai kwetu wala kwa wale tunaowaombea. Tunapoomba kwa imani katika kazi ambayo Kristo alimaliza, tunaleta ushindi wa Kalivari katika hali zetu! Katika kuwaombea waliopotea, mimi humkumbusha Ibilisi kwamba Yesu tayari amemkomboa huyo rafiki yangu aliyepotea. Namwamrisha Shetani amwachilie huyo mtu ambaye Yesu Kristo alimfilia. “Nakiri damu” ya Kristo juu yake. Ufunuo 12:11 Inasema, “wakamshinda Shetani kwa damu ya mwana kondoo, na neno la ushuhuda.” Tunaweza kumshinda kwa njia iyo hiyo. Maneno ya wimbo maarufu wa Martin Luther yanakuja kwa mawazo: “…hatutetemeki kwa ajili yake: … neno moja ndogo litamwangusha.” Ushindi Wake Ni Ushindi Wetu Ningependa kutilia mkazo jambo hili la asili la kujitambulisha kabisa na Kristo. Ushindi wake ulikuwa kwa manufaa yetu. Tunashiriki katika ushindi huo. Tumo “ndani yake,” naye yumo ndani yetu. Kwa hivyo, lililo kweli kihistoria linaweza kuwa kweli hata katika maisha yetu ya kila siku.77 Kuishi katika ushindi kama Mkristo si vigumu kamwe. Ni kupumzika tu katika ushindi wa msalaba. Ni kuleta kalivari kikamilifu katika maisha yetu, kwa imani. Wakati fulani nilimwandikia mchungaji mmoja rafiki yangu ambaye alikuwa na mashtaka huko Romania. Mashtaka juu yake yalikuwa ya uongo, na yasiyothibitika. Alihukumiwa kifungo cha miaka miwili. Niliporudi nyumbani kutoka Romania, niliwajulisha rafiki zangu wengi wamwombee ili apate kuachiliwa huru. Tulituma barua na simu nyingi kuwajulisha viongozi kwamba huyu mchungaji alikuwa na marafiki katika nchi za magharibi. Hatimaye tuliona silaha bora kuwa maombi. Mimi binafsi nilimweka katika ulinzi wa Mungu. Na pia nilimkemea Shetani na kumuamrisha “kuacha na kukoma” kumhangaisha huyu ndugu Mrumi. Nilihusisha msalaba wa Yesu kwenye vita. Baada ya kitambo kidogo tulifahamishwa kwamba mashtaka dhidi yake yalifutiliwa mbali na kesi hiyo kutupiliwa mbali. Bwana asifiwe! Tusimruhusu Shetani kutuchezea, kuturusha mrungula, au kutupotosha kwa vyo vyote vile. Tukiwa ndani ya Kristo tu washindi kila siku, na wakati wote. Tuamini, tutende, na kuomba kikamilifu. Ijapokuwa tuko mwilini, hatupigani vita vay mwili, maana silaha za vita vyetu si vya mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome. Tunaangamiza mawazo na kila kitu kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na kuteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo (2 Kori.10:3-5). Silaha Za Maombi Hivi vifungu vinatuonyesha jinsi tunavyoweza kutumia silaha zetu za maombi. Zina “uwezo katika Mungu kuangusha ngome” (kifungu cha 4). Ngome hizi ambazo tunastahili kuangusha kwa silaha zetu za maombi ni zipi? Matamshi haya labda yanamaanisha maeneo ya ufungwa (tabia ya dhambi) katika maisha ya watu. Watu wengi wana ngome za Shetani za hatia, shaka, hofu, uasi na dhambi ya wazi. Ngome hizi za kishetani zinatokana na miaka mingi ya mazoea ya dhambi. Haya maeneo ya ufungwa huteka watu nyara ili kufanya mapenzi ya Shetani. Tutaweza kuweka huru waliotekwa nyara kupitia ka uombezi. Iwapo una rafiki aliye katika tabia ya utumwa wa dhambi kama vile kutumia madawa za kulevya, au kunywa pombe, basi mama shujaa wa maombi, una jukumu la kupigana vita kwa niaba yake. Katika maombi unaweza kuangusha hizo ngome kwa kutomruhusu Shetani kumhangaisha, kumfurahisha, au kumjaribu huyo mtu. Amrisha Shetani katika jina la Yesu aondoe makucha yake kutoka kwa nia, mawazo, au mwili wake. Maombi ya thati yanaweza kuwa huduma ya ajabu! Neno La Mwisho Katika maombi tunatumia silaha zote. Kwanza, kutokana na kikao chetu katika Kristo tunaweza kumwendea Mungu kwa ujasiri tukidai ahadi zake. Kisha tuna silaha za damu, msalaba, Neno, na jina kuu la Yesu Kristo, ambayo yanatuwezesha kuwa waombezi kwa niaba ya wengine. Silaha hizi zinaweza kuwa za ajabu zikitumiwa na muumini aliyejazwa na Roho; na kutembea katika imani na utiifu. Katika sura itakayofuata, tutaangalia zaidi mamlaka ambayo muumini anayo anapotumia kikamilifu silaha zake za maombi. Michango 1. Tafsiri ya Mfalme Yakobo inatafsiri hivi “maandiko ya sheria”. 2. “Bwana Yesu Kwetu Ngome Nzuri,” na Martin Luther.7879 FUNGUO ZA UFALME NI ZIPI? “Amini nawaambieni, yoyote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yoyote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao. Mathayo 18:18-20 Niliwahi kuongoza kongamano la Bibilia kwa wanafunzi wa chuo cha Bibilia. Msichana mmoja kijana katika kongamano hilo aliuliza swali la kuchochea fikira, akisema: “Yesu alimaanisha nini kwa matamshi yake katika Mathayo 16:19, alipomwambia Simoni Petero: ‘Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lolote utakalolifunga duniani, litafungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni’?” Swali lake lilikuwa na pande mbili. “Funguo” za ufalme wa mbinguni ni zipi? Pili, maana yake nini “kufunga na kufungua” katika matamshi haya? Haya ni maswali mazuri. Majibu yake si rahisi kwa sababu kuna maswala yanayotatanisha. Nimetaja mambo mawili. Jambo la kwanza linapatikana katika utangulizi, na lingine liko katika swali la mwanafunzi yule. Yote yanahusika na kufunga na kufungua. Yesu alieleza jambo hili la asili katika nyakati mbili tofauti, ambapo Mathayo aliyakumbuka na kuyaandika. Katika Mathayo 18:18, matamshi haya yameandikwa kama nidhamu na maombi ya kanisa. Bali katika Mathayo 16:19, tunaona yakielezewa Simoni Petero, akiwa na wanafunzi wengine kule Kaisaria Filipi katika pembe za kaskazini mwa Galilaya. Alichomaanisha Yesu katika mafundisho haya yana manufaa kwetu sana leo kwa maombi yetu, hasa katika kuombea watu wengine. Ingawa hivyo, waumini wachache sana leo wanaelewa maana ya maneno hayo. Mafundisho ya Wakatolika Wa Roma Mafunzo yangu ya kwanza kanisani nilipata katika kanisa la Kikatolika la Roma. Hivi vifungu katika Mathayo 16:18-19 ni sehemu muhimu ya mafunzo ya kidini kwa Warumi. Wanathiologia wa kikatoliki huchukua kifungu cha 18 na kukitumia kuonyesha kwamba Petero ndiye mwamba wa msingi ambaye Kristo alijenge kanisa juu yake. Wanaposema haya maneno ya Yesu wanamaanisha kwamba Kristo alimpa Petero funguo za ufalme wa Mbinguni. Zilikuwa funguo zenye uwezo wa kusamehe dhambi, na kwa hivyo Petero na msururu wa Baba Watakatifu waliofuata wana uwezo wa kuamuru mbingu kusamehe watu fulani, na kutowasamehe wengine. Ili uthibitishe maneno haya, unaweza kutembelea jiji la Vatican, kule Roma. Katika kanisa la Mtakatifu Petero kuna sanamu iliyochongwa kwa marmar inayotoshana na mtu aliye hai. Sanamu hiyo imepiga magoti mbele ya Kristo. Kando ya sanamu hiyo kuna maandishi yaliyochongwa kwa mawe, ambayo yanasema: “Nami nitakupa (yaani Petero) funguo za ufalme wa mbinguni; na lolote utakalolifungua duniani litafunguliwa mbiguni.” Hivyo basi, mafunzo ya dini ya Kirumi yanatumia kufungu hiki kufundisha kwamba Petero ameinuliwa, na ana uwezo wa kusamehe dhambi. Sioni tafsiri hii kuwa sahihi. Sina ugomvi na kanisa la Katoliki la Warumi, isipokuwa tafsiri ya namna hii kuhusu maneno ya Yesu yanapotosha. Ni rahisi mwanafunzi mwema wa Bibilia kugundua hivyo. Hata hivyo, kuna makosa aina tatu ambayo yamehusishwa.80 Kwanza kabisa, ni nani aliyeambiwa maneno hayo? Petero peke yake, au kanisa kwa ujumla? Watu wanaosema Yesu alimpa Petero funguo wanakabiliana na tatizo katika kuelewa hayo maandiko. Hii ni kweli kwa sababu mbili. Kwamza, Petero siye “mwamba” wa msingi ambaye Yesu alijenga kanisa lake juu yake. Yesu mwenyewe ndiye msingi wa kanisa lake. Petero kwa Kiyunani ni Petros, ambayo maana yake ni “jiwe, au mwamba mdogo.” Neno ambalo limetafsiriwa “mwamba,” katika kifungu hicho (Mathayo 16:18) lina maana lingine kwa Kiyunani la petra, ambalo ni “utanda wa chini wa mwamba,” mwamba mkubwa, au mwamba wa msingi. Petero ni Petros, kipandu tu cha Petra yenyewe. Lugha ya Kiyunani iliyotumiwa hapa ni ya wazi, na ya kubainisha. Wasomi wengi wa kisasa wanakubaliana kwamba “Mwamba” wa msingi ambalo Kristo amekuwa akijenga kanisa juu yake ni ufunuo tukufu ambao Simoni alifunuliwa katika kifungu cha 16, kwamba Yesu ndiye Kristo. Funuo hili tukufu humjia kila muumini wa kweli. Roho Mtakatifu anapomtambulisha Kristo katika moyo wa binadamu, itamlazimu kufanya vile Simoni alivyofanya, yaani kukiri alivyofunuliwa na Kristo. Hivyo ndivyo watu wanavyozaliwa mara ya pili katika kanisa la kweli. Hivyo ndivyo kila mmoja wetu anavyokuwa “sehemu ya mwamba.” Kila muumini ni Petros, sehemu ya Petra. Petero, Ama Kanisa Sababu ya pili ya kukataa wazo kwamba Yesu alimpa Petero (na hatimaye, Baba Watakatifu waliokuja baadaye) uwezo wa kiungu wa kusamehe dhambi halina utatanishi sana. Bwana Yesu anarudia maneno haya juu ya uwezo wa kufunga na kufungua katika Mathayo 18. Hapa anatumia hili neno kwa jinsi tofauti sana, kwani hamtaji tena Petero. Haya maneno yameambatanishwa na maombi. Yesu anasema kwamba “wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye Mbinguni” (Mathayo 18:19). Tazama, “ikiwa wawili wenu watapatana,” wanaweza kuomba na kupokea. Anawezaje kusema kwa ujumla “wawili wenu”? Kwa hivyo, watu wowote wawili wanaweza kufunga na kufungua hapa duniani. Kristo analiambia kanisa kwa jumla maneno haya. Vifungu vya kutangulia vinaeleza juu ya washiriki kupewa nidhamu na kanisa. Yesu anatuambia jinsi ya kumrudi ndugu “aliyepatwa” katika dhambi. Kwa kumaliza, matamshi yake yanatuvumbulia silaha yetu kuu, kwamba ikiwa wakristo wawili tu watapatana kwa mapenzi ya Mungu katika maombi, wanaweza “kufunga na kufungua.” Hii ni muhimu zaidi. Mathayo 18 inatufundisha uwezo huu wa “kufunga na kufungua” kuwa silaha ya maombi ya kutumiwa na kanisa. Si uwezo maalum ambayo imepewa kikundi kilichochaguliwa cha maaskofu ambao kwa njia nyingine ya siri ni wazao wa Simoni Petero. Kufunga na Kufungua ni Nini? Kosa la tatu ni kuhusu maneno ya Yesu, “utafunga duniani” na “kufungua duniani.” Je, Yesu kweli alimaanisha kwamba Petero, ama mwingine yeyote yule, ana uwezo wa kusamehe dhambi kwa hakika? Nafikiri sivyo. Baba Mtakatifu au kuhani hana uwezo huo. Ni Mungu pekee anayeweza kusamehe dhambi. Ni rahisi kuona ukweli huo. Ukitazama kwa makini Mathayo 16:19 na Mathayo 18:18 utaona ukweli huu. Agano Jipya katika The King James Version linalojulikana kama andiko lenye “mamlaka” kwa miaka 350, linatafsiri hivi vifungu kwamba “… lolote mtakalolifunga duniani litafungwa mbinguni: na lolote mtakalolifungua duniani litafunguliwa mbinguni.” Tafsiri ya maneno yaliyotumika hapa yanahusu vitendo vijavyo. Kama hili lingekuwa sawa, basi tafsiri nalo lingekuwa sawa. Tafsiri kamili basi lingekuwa kwamba “mbingu” linangoja “dunia” liliambie la kufanya, yaani mbingu litapata mashauri kutoka duniani. Hivyo ni kusema kwamba nikipiga jambo lolote marufuku, au nikiruhusu jambo lolote, basi Mungu lazima atii uamuzi wangu. Haya ni mafundisho yanayopatikana kutoka kwa wale wanaofundisha kwamba mwanadamu anaweza kusamehe dhambi. Kosa hili limetokana na kutotafsiri vyema maneno yaliyotumika. Maneno hayo hayahusiani na vitendo vijavyo, bali yanaonyesha mchanganyiko wa habari yenye maneno ya kutendwa, na mafumbo ya maneno. Hakika katika vifungu vyote viwili, neno la kwamza linaonyesha tendo lililotendeka, na la pili linaonyesha ukosefu wa tendo. Kwa hakika, maneno yote mawili hayaonyeshi81 matendo yajayo. Interlinear Greek-English New Testament, katika Kiyunani, inatafsiri kwamba “likiisha kufungwa” (au kufunguliwa). Tafsiria ya Bibilia liitwalo The American Standard Bible, linaonyesha kwa usahihi maana ya maneno haya kwa kutafsiri kwamba “lolote mtakalolifunga duniani tayari litakuwa limefungwa mbinguni; na lolote mtakalolifungua duniani tayari litakuwa limefunguliwa mbinguni.” Tilia mkazo maneno “tayari litakuwa.” Hii ni ukweli wa maandiko haya, kwamba yale ambayo Yesu alisema ni kinyume na jinsi yalivyoandikwa katika Bibilia ya The King James Version. Dunia haina uwezo wa kuamrisha mbingu! Haiwezekani kabisa! Dunia ndio huamrishwa na mbinguni. Tunaweza tu kufunga na kufungua kile ambacho tayari kimefungwa au kufunguliwa. Tunaweza kudai kitu ambacho tayari kimefungwa, au kufunguliwa, katika maombi. Huku kufunga na kufungua ndio mamlaka yetu katika Kristo. Hatuhusiki katika kusamehe dhambi, bali katika uombezi tunachukua mamlaka juu ya adui. Kufunga na kufungua ndio silaha ya maombi. Mfunge Shetani Kabisa Je, umewahi kutaka kumfunga Shetani kabisa hata kwa siku moja? Je, hutapendezwa kumwamuru kukuacha, au kuachana na wapendwa wako? Kuna kanuni moyoni mwa Yesu katika mafundisho yake kuhusu kufunga na kufungua. Kanuni hiyo ni kwamba tuna nguvu dhidi ya yule mwovu! Kwa sababu Yesu tayari alimpokonya Shetani nguvu (Waebrania 2:14), tumeshirikishwa katika huo ushindi. Tunatazama mbinguni na kuona ushindi wa Bwana. Kisha kwa imani, tunatumia “funguo” zetu kuamrisha Shetani kufungua rafiki zetu waliopotea. Pia tunaweza kumuamuru kufungwa ili asinyanyase rafiki zetu. Kila siku katika maombi tunaweza kukataza, au kuruhusu kufunga na kufungua. Hizi “funguo” ni silaha zetu kuu za kuangusha ngome zinazotajwa katika 2 Wakorintho 10:4. Kuweka Waliotekwa Huru Asili ya uombezi ni kanuni ajabu ya “kuweka waliotekwa huru” ambao ni kiini katika uombezi. Tuliona hapo mbeleni katika kitabu kingine jinsi ya kuombea waliopotea. Katika somo hilo, kuna sisitizo kwamba aliyepotea dhambini ni mateka wa Shetani. Amefungwa kwa minyororo ya kiroho. Amepofushwa na muovu ili asiweze kuona ukweli wa injili. Shetani amempofusha na kumfunga. Anahitaji kutolewa kutoka utumwani na kuwekwa huru. Ni jukumu la kanisa linaloamini kuomba ili awekwe huru. Tunapomwondosha Shetani kutoka kwa uwanja wa vita wa mwanadamu, basi mtu huyo ambaye hajaokoka atakuwa huru kufanya maamuzi ya busara kuhusu kumfuata Yesus Kristo. Unapokutana na mwenye dhambi asiye na Mungu, lazima umuhurumie. Yuko mtegoni mwa yule mwovu (2 Timotheo 2:26). Tuwe vitani kwa niaba yake, kwani amepotea na kukosa tumaini. Bali tukifanya maombezi kwa ajili yake, Shetani atamfungua, na ataweza kuamua kunfuata Kristo kwa hiari yake mwenyewe. Hii haimaanishi kwamba kila mtu tutakayemwombea ataokoka, bali wengi wataokolewa ikiwa kanisa litaamini na kuchukua mamlaka juu ya adui. Yesu ametupa funguo za Ufalme wa mbinguni – ila tu tujifunze kuzitumia! Malango ya kuzimu hayawezi kusimama dhidi ya kanisa liombalo. Michango 1. A.T. Robertson, Word Studies In The New Testament, vol.1 (Nashville, Tennessee: Broadman Press, 1930), ukurasa 149. 2. The International Greek - English New Testament (London: Samuel Bagster and Sons, 1964). 3. Chapter 16 in Questions Non Christian ASK (Old Tappan, New Jersey: Fleming H. Revel Company, 1977), ukurasa 145-53.



MAOMBI YA UOMBEZI NI NINI? 

Kutumia muda mwingi kwa Mungu ndio siri ya maombi yanayofaulu. Maombi yanayohisiwa kuwa ya nguvu yanatokana na muda unaotumiwa kwa Mungu. Maombi mafupi yana maana na uhodari kutokana na maombi marefu yaliotangulia. E. M. Bounds, Power through Prayer Hapo awali tulitumia neno “uombezi.” Watu wengine wanaona hii kuwa ufahamu mpya. Hebu tufafanue. Kurasa nyingi zilizobaki katika kitabu hiki zinaongea juu ya huduma ya uombezi. Uombezi ni nini? Tunaambiwa katika Agano La Kale kwamba Masihi akija atafanya uombezi kwa niaba ya wakosaji (tazama Isaya 53:12). Yesu alikuwa, na bado angali, Mwombezi mkuu. Wahebrania 7:25 inatuambia kwamba Yesu yu hai, ili atuombee mbele ya kiti cha enzi cha Mungu. Neno uombezi linatokana na neno la zamani la Kiyunani ambalo lilikuwa neno lililotumika kwa wale waliomwendea mfalme. Lilitumika kueleza maombi kama kumwendea Mungu. Neno la Kingereza la intrude (kuingilia kati bila kukaribishwa) lilitokana na neno hilo la Kiyunani. Kufanya uombezi ni kuingilia kati bila kukaribishwa, kwa niaba ya mwingine. Mwombezi ni “mshenga” anayeombea kesi ya mwingine. Kuwa mwombezi ni kuwa mpatanishi. Aina Maalum Ya Maombi Kuna mitindo mingi ya maombi, lakini maombi yanayomfurahisha Mungu ni maombi ya uombezi kwa dhati. Ni maombi yasiyo na ubinafsi, bali kujitolea mhanga. Maombi ya uombezi yanaweza kuwa silaha yenye nguvu milele. Yanaweza kuwa silaha ya siri kwa kanisa. Wakati moja nilisikia maombi ya uombezi yakielezwa kuwa kombora la kimataifa la Mungu lenye masafa marefu, ambalo linaweza kulengwa au kuelekezwa popote duniani. Linapiga shabaha lake, likienda mwendo wa kasi ya wazo. Wakati mwingine laweza hata kuchelewa kulipuka ili liweze kujibiwa miaka mingi baada ya kutumwa. Karibu miaka elfu mbili iliyopita, Yesu alianzisha kombora lililo na jina lako, alipoomba katika Yohana 17:20 akisema “wala si hao tu ninaowaombea, lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao.” Siku ile uliokoka, Mungu alijibu maombi ambayo Yesu alikuombea zamani. Maombi ya uombezi ni maombi ya ajabu! Naamini kwamba mtu anapozaliwa mara ya pili, Mungu huwa amejibu maombi ya Yesu tena. Kila mara mtu anapookaka, juhudi za mwombezi hujibiwa. Wazazi wana silaha ya siri ya kutumia kwa ulinzi ya watoto wao. Unapowaombea watoto wako unahifadhi historia kwa ajili ya huyo mtoto. Tayari nimewasilisha maombi juu ya watoto wangu kwa miaka zijazo. Walipokuwa wachanga, niliwaombea kuhusu miaka ya ujana wao. Kwa kumhusisha Mungu katika maisha yao ya baadaye, unawapangia maisha yao ya siku za usoni. Miaka mingi baadaye, Mungu atayajibu maombi hayo. Kinachoshangaza ni kwamba Shetani hana silaha dhidi ya “neema hii iliyohifadhiwa.” Hii pia ni kweli tunapomwombea mtu aliyepotea. Mtu aliyepotea huenda asikusikilize unapomshuhudia kuhusu Mungu. Huenda hataenda nawe kanisani, au kusoma Bibilia uliyomnunulia. Hata hivyo, unapomwombea na kumwuliza Roho Mtakatifu wa Yesu agonge katika mlango wa moyo wake, Shetani hawezi kuwa na silaha au kizuizi dhidi ya maombi yako. Yesu atamwendea huyo mtu na kuzungumza naye. Tukijua hivi basi, mbona tusitume makombora yetu kila siku? Nina hofu kwamba dhambi kubwa ya kanisa la kisasa ni ukosefu wa maombezi. Tunahitaji moyo wa nabii Samweli aliyepaza sauti akisema, “Walakini mimi, hasha! Nisimtende BWANA dhambi kwa kuwacha kuwaombea ninyi” (1 Samweli 12:23).84 Fumbo Juu Ya Uombezi Yesu alisimulia hadithi nyingi za ajabu. Lakini hakuna hadithi iliyokuwa rahisi na yenye kuvutia kama ile ya mtu aliyembishia jirani yake mlango usiku wa manane. Yesu alisimulia hadithi hii ili kuonyesha Mungu anavyohisi kuhusu uombezi. Akawaambia, “ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, Rafiki yangu, nikopeshe mikate mitatu, kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, nami sina kitu cha kuweka mbele yake; na yule wa ndani amjibu akisema, Usinitaabishe; mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe? Nawaambia ya kwamba, ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake. Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa” (Luka 11:5-10). Kuomba Kwa Ujasiri Kama kuna funzo maalum kutoka kwa hadithi hii, basi ni kanuni ya ujasiri, kuthubutu, na kuwa na mamlaka. Hapa tunaona mtu jeuri, akigonga mlango wa jirani usiku wa manane. Hawezi kuacha kubisha mpaka mwenye nyumba aende kumfungulia na kumpa haja yake. Tazama alivyo jeuri, anavyosisitiza, na mwenye uthabiti. Wanafunzi wa Bwana wetu walikuwa wamemuuliza awafundishe kuomba (Luka 11:1). Katika hadithi hii, Yesu anasema wazi wazi, “Njoo kwenye kiti cha enzi kwa ujasiri. Uwe thabiti katika maombi yako.” Huwezi Kuomba Kupita Kiasi Uombezi wetu lazima uwe thabiti kulingana na maombi yetu. Hebu mwone huyu mtu anavyoomba mikate mitatu, badala ya mkate mmoja. Nyakati hizo mkate moja ilikuwa chakula cha siku nzima! Ni ajabu, sivyo? Hivyo ndivyo tunavyostahili kumwendea Mungu. Nimehuzunishwa sana kusikia watu wengine wakisema tusimsumbue Mungu kwa kumwomba “vitu.” Hata hivyo, Mungu ana shughuli nyingi, na hawezi kusumbukia shida zetu za kila siku! Si hivyo ndivyo ilivyo kiroho, jamani? Inaweza kuonekana kuwa takatifu, lakini haiambatani na mafundisho ya Bibilia. Nashukuru kwamba Mungu wetu si wa namna hiyo. Anataka tuombe maombi makuu. Nilitaja mambo hayo awali katika kitabu hiki, lakini ni vyema tuyataje tena. Wewe unakuja kwa Mfalme, Maombi makubwa kwa ewe mfalme, Neema yake yatosha na uwezo wake watosha, Huwezi kuuliza zaidi kupita kiasi. Lililo na maana kwako lina maana kwa Mungu. Anataka kukupa mahitaji yako yote. Rafiki anayekuja kubisha mlango usiku si mjasiri tu wa kuomba mikate mitatu, bali ni msumbufu pia. Hatachoka. Katika kifungu cha 7, Yesu alisema mwenye nyumba hangefungua mlango isipokuwa tu kwa usumbufu wa yule jirani. “Nawaambia ya kwamba ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka, na kumpa kadiri ya haja yake.” Kwa nini alimpa kiwango alichohitaji? Hii haina uhusiano na urafiki, kwa sababu tafsiria ya The King James Version imetumia neno ambalo kwa Kiswahili ni maombi ambayo ni sumbufu (yenye udhia). Mombi iliyo sumbufu ni maombi gani? Neno hili halitumiki sana, lakini ni tafsiri kutoka kwa lugha ya Kiyunani ambalo lilikuwa na maana ya kutokuwa na aibu. Tafsiri ya The New American Bible linawasilisha neno hilo sawa kwamba “aliendelea kubisha bila aibu,” na mwishowe, kwa sababu ya jitihada zake, mwenye nyumba aliamka na kumpa hitaji lake. Hivi ndivyo tunavostahili kwenda mbele ya kiti cha enzi cha Mungu katika maombezi. Tunapoombea wokovu, ulinzi, afya, mali, ama lolote lile, kwa ajili ya85 watu wengine, Yesu alisema tunahitaji kuendelea kuomba, kutafuta, na kubisha. Hatimaye Mungu atatupa hitaji letu. Kuomba Mungu Anayesita? Swali la kawaida lazuka hapa. Je tunajaribu “kumpokonya” Mungu, ambaye ni wa kusita, kitu alichofungia mkononi? La, hasha. Lazima tukumbuke kwamba tunazumza juu ya aina maalum ya maombi. Katika maombi haya, tunawaombea wengine mpaka Mungu ajibu kwa njia moja au nyingine. Mara nyingine Mungu hukawia kujibu ili tuweze kukua kiroho katika maombi. Kumbuka Yakobo alivyopigana mweleka na malaika wa Bwana katika kijito cha Yabbok (Mwanzo 32:2-29). Yakobo alipigana na huyu malaika usiku kucha hadi alfajiri. Malaika alimsihi amwache, lakini Yakobo akadai mgeni huyo ambariki ndipo amwachilie. Katika hali ya kusita, malaika huyo alimbariki. Yakobo akamwachilia. Labda inaonekana kwamba kuna kitu ambacho si sahihi kuhusu pigano hili. Swali ni kwamba tangu lini mwanadamu kama Yakobo akawahi kupigana na malaika shupavu wa Mungu mweleka na kumweka chini, kisha akaitisha baraka kutoka kwake? Naona kwamba vita hivyo vilikuwa vimepangwa mbeleni. Naamini kwamba huyo malaika alikuwa akifurahia vita hivyo. Hakuwa na haraka ya kuachiliwa. Picha ile ni kama ya Baba anayemenyana na mwanawe mdogo wa kiume. Ni kama malaika alikuwa akizungumza kimoyomoyo akisema “Usikate tamaa Yakobo, nitakubariki ikiwa tu utang’ang’ana zaidi kidogo.” Mungu ana mengi ya kutufundisha tunapotafuta, tunapoomba, na tunapobisha. Imani yetu inapanuliwa, na tabia yetu inaundwa na kufanywa imara katika bidii. Tunachojifunza katika uombezi kila mara ni ya thamani kuliko jibu yenyewe. Kuwaombea wengine hujenga unyenyekevu na upendo usio kuwa na choyo ndani yetu. Uombezi Unahitaji Kujitolea Kanuni nyingine muhimu katika hadithi hiyo ni kwamba yule bwana alijitolea kabisa. Usiku wa manane, alienda nje kutafuta chakula ampe rafiki yake. Rafiki yake alikuwa na njaa, lakini hakuwa na njia ya kumlisha. Hivyo ilimbidi kutambua kwamba rafiki yake kweli alikuwa na njaa. Angesema, “Ikiwa una njaa sana, basi nenda ukawaamshe majirani ili wakasirike nawe.” Lakini hakufanya hivyo. Badala ya kufanya hivyo alitambua njaa ya rafiki yake, na kuifanya kuwa shida yake. Huo ndio moyo wa mwombezi. Moyo wa mwombezi ni kujitambulisha na hali ya wengine. Je umewahi kuhisi hivyo kwa sababu ya rafiki yako ambaye hajaokoka? Je upotevu wake umewahi kukumeza mpaka ukauonna kuwa mzigo wako? Itakubidi kujiweka katika nafasi ya huyo mwenye dhambi aliyepotea na kuanza kubeba upotevu wake katika moyo wako. Hitaji lake litakuwa hitaji lako. Mwongozi mkuu, John Knox wa Scotland, alipaza sauti mbele ya Malkia wa Scotland akisema, “Nipe Scotland, au nife.” Namwona kijana Daudi Brainerd akipiga magoti katika theluji nje ya kijiji cha Wahindi akimsihi Mungu kuwaokowa hao makatili, waliokuwa katika misitu ya New England katika miaka ya 1743-1747. Kijana Brainerd aliwaombea hao wahindi hadi akazirai kutokana na kukaa kwenye baridi kwa muda mrefu, na kuchoka. Ilichukua miaka mingi ya maombi na kushuhudia, lakini mwishowe Mungu alifungulia Brainerd milango ya uinjilisti. Kujitoa kwake kuliathiri afya yake na kumgharimu maisha yake. Lakini David Brainerd akawa mmisheni wa kwanza kabisa katika eneo hilo. Maisha yake ilivutia maelfu ya watu katika huduma ya maoambezi na kushuhudia.Maisha ya uombezi yanahitaji kujitolea katika muda, vipawa, na hata uhai. Tunakuwa waombezi kwa watu wengine katika kujitambulisha na mahitaji na machungu yao. Tunapotokwa na damu, tunabariki. Hakuna njia nyingine. Mungu atupe kujali kama vile Musa aliyeomba kwamba: “Aa! Watu hawa wametenda dhambi kuu, wamejifanyia miungu ya dhahabu. Walakini sasa, utawasamehe dhambi yao - na kama sivyo, unifute, nakusihi, katika kitabu chako ulichokiandika” (Kutoka 32:31-32).86 Hiyo ndiyo roho ya kujitambulisha na kujitoa. Maombi Yenye Haja Tukisoma zaidi somo la uombezi, tutaona mara kwa mara kwamba shujaa wa maombi wa kweli ana juhudi. Shujaa wa maombi mara nyingi ni mtu mjasiri aliye tayari kufanya lolote. Mfano ambao tumeonyeshwa katika masomo haya unaonyesha hali ya dharura. Mtu huyu alienda usiku wa manane kutafuta msaada kwa sababu alihitaji msaada huo kwa dharura. Alisema, “Rafiki yangu amefika kwangu … na sina kitu cha kuweka mbele yake” (Luke 11:6). Mtu huyo aliona kuwa ni jukumu lake kumwendea jirani yake kutafuta msaada akiwa na ujasiri. Ningeomba Wakristo wengi wachukue jukumu katika kazi ambayo Mungu amempa kila moja wetu. Kanisa haliwezi kukutunzia watoto wako. Hilo ni jukumu lako kuwatunza. Kazi yako muhimu kila siku ni kuwaombea. Mungu anapendezwa sana anaposikia wazazi wakiombea watoto wao. Hatari iliyoko ni kwamba mara nyingi tunangoja hadi tupate shida, ndipo tunaomba. Tukingoja hivyo basi huwa tumechelewa. Hatuwezi kuomba maombi ya dharura hadi tuwe katika hali ya kutokuwa na uwezo. Mtu huyu alikuwa katika hali mbaya kwa sababu hakuwa na chakula cha kumpa mgeni wake. Mara nyingi hatuombi kwa uaminifu kwa sababu tunafikiri tumetosheka ndani yetu. Tunakosa kumtegemea Mungu tunapokuwa na afya njema, fedha, kazi, au hata mali. Vitu tunavovitegema vikiisha, basi tutatambua kwamba hatuwezi kukabiliana na maisha. Hii ni hakika pia katika mambo ya kiroho. Tunapokumbana na shida ambazo haziwezi kusuluhishwa na fedha au mali, ndipo tunakuwa tayari kuomba. Mwombezi wa kweli anajua kwamba ni Mungu tu anayeweza kukutana na mahitaji ya maisha yetu. Anajua “sina kitu.” Kisha humwendea Baba wa Mbinguni, aliye na kila kitu. Huduma ya Uombezi Pengine hitaji kubwa katika ulimwengu wa leo ni kupata waombezi wa kweli. Watu kama hao wanamwamini Mungu anayejibu maombi. Wako tayari kujitambulisha na ulimwengu unaoumia na kufa. Hawawezi kumwachilia Mungu hadi awabariki. Katika kurasa zitakazofuata, tutaangalia kwa undani huduma hii ya uombezi ambayo inahitajika sana. Michango 1. “Endelea” kuomba, kubisha, na kutafuta inaeleza vitendo hivi katika hali ya sasa.87


JE, KUKOSA KUTII 
KUNAWEZA KUZUIA MAOMBI YAKO? 

Maombi ni kama zana hatari zenye uwezo wa kupiga bara lingine zikirushwa kutoka kwa jukwaa la maisha yetu. Maana kamili ya maombi yanatokana na maisha ya anayeomba. Maisha ndio huomba. -Ronald Dunn, Lifestyle Ministries. Je, kukosa kutii kunaweza kuzuia maombi? Jibu la swali hili ni wazi kiasi cha kupuuzwa. Lakini swali hili linatupa jambo la kufikiria. Mara kwa mara sisi hujishughulisha zaidi na jinsi tunavyoomba. Tunataka kujua kama tunasema maneno yanayofaa, kwa sauti inayokubalika kidini. Tunahitaji kukumbushwa kwamba Mungu hujali nia ya nyoyo zetu, kuliko maneno tunayotumia katika maombi. Maombi sharti yawe zaidi ya maneno yanayotamkwa kwa Mungu. Nimeona watu wakiandika maombi mazuri sana ya kusoma hadharani. Maombi hayo kwa hakika husikika kuwa ya kuvutia sana. Je, yana maana? Je, utungaji na uchaguaji wa maneno mazuri humpendeza Mungu? Sidhani hivyo. Hapa kuna kanuni ya kiroho inayofaa tujifundishe. Maisha Ndio huomba. Mwanzo kabisa, wakati wote maisha ndio huomba. Mwandishi wa Zaburi alinena wazi wazi kwamba “Kama ningaliwaza maovu moyoni mwangu, Bwana asingesikia ” (Zaburi 66:18). Bwana Yesu alisisitiza kanuni hii katika Yohana 15:7 aliposema, “Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa.” Unaona “kukaa” kwetu huvuta majibu yake. Ni maisha iombayo. Masharti Mawili kwa Maombi Yanayojibiwa Je umewahi kushangaa kwa nini maombi ya watu wengine hujibiwa haraka kuliko yako? Inaonekana kwamba maombi ya watu wengine husikika hunfikia Mungu mara moja. Mbona hivyo? Naona kwamba kuna mambo mawili muhimu ambayo Mungu huzingatia katika kujibu maombi yetu. Kwanza kabisa, hitaji la kuombewa sharti liwe linaambatana na neno la Mungu. Waraka wa kwanza wa Yohana 5:14 imetueleza jambo hili waziwazi. Isipokuwa uombe kulingana na neno la Mungu, maombi yako hayawezi kujibiwa hata ukiwa na imani au bidii ya namna gani. Jambo la pili ni kwamba anayeomba ni sharti aishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Mungu hutazama maisha ya anayeomba. Maombi hutumwa Mbinguni kutoka kwenye jukwaa la maisha yetu. Kwa hakika, maisha ndio huomba. Kule kudumu ndani yake husababisha maombi kujibiwa. Ubora na Kukubalika Kwa wengine hii itasikika kuwa jambo la kigeni, lakini katika uchumi ya mambo ya Mungu, uwezo wa anayeomba huwa na hatima katika kukubalika kwa maombi yake. Yesu alisisitiza haya katika mahubiri yake mlimani. “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako”. Matahyo (5:23-24). Unaona vile Mungu anavyoangalia mambo? Kwake, ubora wa mtoaji ni muhimu zaidi kuliko kile anachotoa. Anayeabudu ni muhimu kuliko tendo la kuabudu. Mungu hutuangalia kabla kuangalia sala zetu.88 Miaka mingi iliyopita, Robert Murray M’Cheyne alisema “Hali ya mtu anapoomba ndio hali yake halisi.” Naamini hayo maneno hayo kuwa kweli, hasa kama yana maana ya kuomba kwa faragha, kwa sababu katika umati sisi huomba maombi “yasiyo kamili” wakati mwingine. Tunapoomba faraghani, hali yetu halisi hudhihirika. Kwa hivyo ubora wa maisha ya mtu binafsi hutegemea maisha yake ya maombi. Kwa hakika, ni maisha iombayo. Kutotii na Kuomba Tunapoishi katika dhambi tunapoteza ujasiri na imani katika maombi. Ni vigumu kwa moyo iliyo na hukumu kuomba. Waraka wa kwanza wa Yohana 3:20-21 inasema kwamba “...Ikiwa mioyo yetu inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote. Wapenzi mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu.” Nini hutendeka mioyo yetu inapotuhukumu kwa sababu ya dhambi? Sisi hupoteza ushirika na Mungu, huzimisha Roho Mtakatifu, na kukosa ujasiri katika maombi. Shetani huja kwako na kukufunika kwa wingu la hatia kichwani ili usije ukatazama juu. Ni Jambo la kufedhehesha kupoteza uwezo mkuu wa maombi kwa ajili ya dhambi fulani ndogo – “Kama ningaliwaza maovu moyoni mwangu, Bwana asingesikia.” Maisha Yaliyozoroteka na Maombi Yasiyowakilishwa Itakuwa huzuni kubwa mbele ya kiti cha enzi cha hukumu ikiwa Kristo atakuambia kwamba kuna watu aliokusudia kuokoa kupitia kwa maombi yako, lakini kwa sababu ya dhambi fulani katika maisha yako hakuweza kuomba kupitia kwako. Maisha yako yalikuhukumu mpaka Roho Mtakatifu akashindwa kuwa mwombezi ndani yako. Rafiki, hakuna kitu cha maana uliwenguni kinachoweza kusababisha ukose kuwa na nguvu katika maombi. Yakobo 5:16 inasema kwamba “Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii.” Tambua kwamba ni maombi ya mwenye haki tu inayoweza kuwa na matokeo. Maisha ya Kudumu Tukirejelea maneno aliyoyasema Bwana katika Yohana 15:7, “Mkikaa ndani yangu . . . ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa.” Je wewe ni mkristo wa kukaa? Je unaishi maisha ya kukaa ndani ya Kristo hadi kumsababisha kukuhakikishia majibu kwa maombi yako? “Kukaa” ni kudumu, au kuishi katika ushirika na mtu fulani. Katika mafundisho haya Yesu anatumia mfano wa matawi na mzabibu. Kukaa ndani ya Kristo ni kudumu ndani ya Yesu jinsi tawi lidumuvyo kwa mzabibu. Tawi hudumu kwa mzabibu na kuutegemea kwa uhai wake. Tawi lina kusudi moja, ambalo ni kukaa ndani ya mzabibu ili liweze kuzaa matunda. Mimi na wewe tunapaswa kudumu ndani ya Mungu, jinsi tawi lidumuvyo ndani ya mzabibu. Ni mbingu peke yake ijuayo matunda ambayo Mungu anaweza kutoa kupitia kwetu. Je, unaishi maisha iliyo wazi kwa Mungu kwa ajili ya huduma na utakaso? Safari yenye Hatia Nimehisi maishani mwangu mara nyingi kuwa na hatia kwa kutomfanyia Yesu zaidi. Labda nina siku ambayo nilikosa kuomba, kusoma Bibilia , au hata kushuhudia. Tafadhali niamini, nimekuwa na nyakati kama hizo! Alafu najihisi kwamba sifai. Kisha najizatiti, kwa udini tu, kutekeleza yale ambayo nilikosa kufanya. Nikiweza kwenda nyumbani na kuona huzuni usoni mwa mfereji wa maji jikoni, na kumuuliza, “Mfereji, mbona una huzuni leo?” “Bwana,” Mfereji anajibu, “hujanitumia kwa siku nzima. Nilitaka kupoesha kiu chako, kusafisha mikono yako, kukusaidia kuosha vyombo, lakini hukunifungua leo.” Nami namjibu hivi, “Wewe mfereji mpumbavu, ningelikufungua wakati wowote kama ningelitaka. Nilijua uko pale na tayari kutumika. Sitaki ujifungue mwenyewe, kwa sababu utapoteza maji tu na kuharibu vitu.” Mungu amenionyesha kwamba yeye ni mzabibu, nami ni tawi. Nastahili kuwepo bila masharti. Hatufai kupima uaminifu wetu kwa matendo yetu, bali kwa kupatikana kwetu. Kuwa mtu wa kudumu halisi si rahisi. Kuwa wazi kwa Roho Mtakatifu bila masharti ni matokeo ya maisha ya chombo kilichovunjika mbele ya Mungu. Sababu hiyo imesababisha waombezi wa kweli kuwa wachache kanisani. Uungu halisi hutokana na maisha ya kujitoa.89 Kudumu Ndani ya Maneno Ya Yesu Bwana wetu ametaja sharti lingine la kujibiwa kwa maombi. “Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa.” Tazama maneno haya: “na maneno yangu yakikaa ndani yenu.” Kuna uhusiano kamili kati ya maisha yetu ya maombi na kukaa ndani ya Neno La Mungu. Kukaa katika neno lake linamaanisha kwamba neno lake linadumu daima ndani yako. Umelikaribisha neno la Mungu kuishi ndani ya moyo wako. Neno linapopenya katika mioyo yetu, litaanza kuongoza, kurekebisha, na kuelekeza maisha yetu. Kwa wengi wetu, mioyo yetu ni kama hoteli kwa neno la Mungu, kuliko kuwa nyumbani mwa neno la Mungu. Wakati wa kuondoka ni Jumapili mchana. Hebu jiulize hivi: Je, neno la Mungu linadumu daima rohoni mwangu hadi kuongoza maisha yangu? Hivyo ndivyo Yesu alivyomaanisha aliposema kuhusu kukaa katika neno lake. Kutii na Kuomba Tunapoendelea kukaa katika neno lake, maombi yetu yataendelea kuwa yenye maana, kwani “na lolote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake” (1 Yohana 3:22). Hebu fikiri: Je, kuna amri ambayo umekataa kutii? Ikiwa ni hivyo basi, maombi yako hayawezi kuwa na maana. Utakatifu maishani mwako yanaambatana na maombi. Hapo awali tuliongea kuhusu maombi ya David Brainerd ambaye alikuwa mmisheni kwa wahindi Wamarekani ya Kaskazini. E. M. Bounds, katika kitabu chake kizuri sana kiitwacho Power Through Prayer, anaeleza hivi kuhusu Brainerd: “Hebu kila mara tumtazame Brainerd kwenye misitu ya Marekani, akiweka moyo wake wazi kwa Mungu kwa ajili ya makafiri, ambapo hangefurahishwa na lolote isipokuwa waokoke. Maombi ya siri, zingatifu, na ya kuaminika – iko katika shina la uungu ndani ya mtu binafsi.” Mtu aliye shupavu katika maombi ni shupavu pia katika neno. Utakaso unaotokana na neno husababisha maisha yenye maombi. Yesu alisema, “Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia” (Yonana 15:13). Kufyekwa na Kuomba Neno la Mungu katika maisha yako linaweza kukutakasa, na Mungu kukutumia kwa huduma na maombi. Kwa kutumia mfano wa mzabibu na matawi, Yesu alinena juu ya kufyekwa iletayo afya katika mzabibu. Kila mkulima huelewa kwamba ili kuwa na mzabibu iliyo bora, itamlazimu kupunguza matawi, badala ya kuongeza. Wengi wetu wana matawi mengi maishani ambayo yanahitaji kufyekwa na Mungu! Tutazaa matunda mengi ikiwa Mungu atazidi kuondoa matawi katika maisha yetu. Kufyekwa na kutakaswa haimaanishi kuondolewa dhambi tu, bali ni kuondolewa mambo tuyaonayo kuwa mema lakini yanaweza kutuzuia kupata mambo ya Mungu. Vitu kama runinga, michezo, na vitu vingine vingi vinaweza kutufanya tusiombe. Tunaweza kusongwa na shughuli nyingi hadi tukose muda wa kuomba. Baba wa Mbinguni anaweza kukata mambo mengine kutoka kwako ili upate wakati wa kuomba kikamilifu. Je, ungependa Mungu akutumie kama shujaa wa mombi aliye mtakatifu, na mwenye bidii? Jiweke tayari kwa Mungu, kama vile tawi lilivyo tayari kwa mzabibu. Michango 1. E. M. Bounds, Power Through Prayer (Grand Rapis, Michigan: Zondervan Publishing House, 1962), p.24.9091

 KIZUIZI KIKUBWA KWA MAOMBI

 Hakuna kizuizi kingine kwa maombi kama ugomvi ambao haujasuluhishwa. Mng’ang’ano wowote kati yako na mwanadamu mwenzako, ni swala kati yako na Mungu wako. “Mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua…” Waebrania 12:15 Kwa kuwa Mungu hutazama kwanza maisha ya anayeomba kabla kufikiri juu ya maombi yake, inafaa kila mara tuishi maisha anayoweza kutumia. Kuna vizuizi vingi vinavyosababisha kutojibiwa kwa maombi. Tayari tumeangalia mengine kati ya vizuizi hivyo, kama vile dhambi, au kutokuamini. Ingawa hivyo, maneno ya Yesu katika Marko 11:24-26 yanaonyesha kwamba kutokusamehe ni kikwazo kikubwa katika kujibiwa maombi. “Kwa sababu hiyo nawaambia,Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu. Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. [Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.] Moyo Wa Kusamehe Vifungu hivi hufadhaisha watu wengine. Mbona Bwana amesisitiza kutokusamehe kama kikwazo kwa maombi, kati ya vitu vyote ambavyo angeorodhesha kama vikwazo kwa maombi? Mara nyingi Bwana wetu anaonyesha hisia za Mungu kuhusu moyo isiyoweza kusamehe. Katika kifungu cha 25, anatuvumbulia kwamba moyo wa kusamehe hutangulia kujibiwa kwa maombi. Ni dhahiri kwamba swala lolote baina yako na mwanadamu mwenzako, pia ni swala kati yako na Mungu. Uhusiano wetu na wanadamu wenzetu ni funguo muhimu katika uhusiano wetu na Mungu. Lazima tuwe na mausiano sawa sisi kwa sisi ndipo Mungu aweze kuongea nasi! Je, umewahi kuwazia jambo hili, kwamba uwezo wako katika maombi hutegemea uhusiano wako na watu wengine? Kwa sababu hiyo, mwandishi wa Waebrania anatuhimiza kwamba “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, …mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo” (Waebrania 12:14-15). Hatustahili kukosa uwezo katika maombi kwa sababu ya kitu chochote hapa ulimwenguni. Maombi ndio maisha yako. Kwa hivyo lolote litakalosababisha ukose kuomba halifai kukugharimu. Kwa sababu Mungu hawezi kukusamehe usiposamehe, ni vyema usiruhusu moyo wa kutokusamehe “kukufunga.” Kusamehe Bila Kukoma Yesu anapotuamuru “kusamehe” katika Marko 11:25, neno analotumia ni katika tendo la sasa. Maana yake ni “kuendelea kusamehe.” Ni heri kusamehe kuwe hali yako ya maisha. Je, unawawekea wanaokukosea hatia? Yesu alisema kwamba utapoteza haki yako ya kuomba kwa kuwachukulia hatia wanaokukosea. Hakuna kizuiacho maombi kama vile kuwa na uchungu na machukizo. Kusamehe kiwe kitendo cha kila siku katika maisha yako. Hujui utaomba wakati gani na kuhitaji jibu la haraka kutoka kwa Mungu. Ukihitaji kuombea mtoto ambaye amekuwa mgonjwa, huna muda wa kwenda katika nchi nzima ukiwasamehe watu na kuomba msamaha. Unahitaji kuomba sasa! Utachelewa kuweka “upanga wako chini” na kuacha machukio wakati kuna dharura. Kusamehe kunastahili kuwa kitendo cha kila siku, ambacho ni cha kuendelea. Kuamua Kusamehe Mara kwa mara watu wameniambia hivi, “ Barry, kama ungalijua jinsi mtu fulani alivyonitendea, hungeliniuliza nimsamehe. Siwezi kamwe kusamehe yale aliyonitendea.” Kwa kweli, msamaha ni kitu
gani? Watu wengine wanafikiri kimakosa kwamba kumsamehe mtu ni kusahau yale aliyokutendea, na kuishi kama kwamba hakukutendea lo lote. Hii si maana ya kusamehe. Mungu hasemi, “samehe na kusahau.” Ametuamuru “tusamehe.” Kiini cha neno ambalo Yesu alitumia hapa ni “kufukuza, au kuondosha.” Kwa hivyo, kama nitakusamehe, itanilazimu kufukuza hisia za kuumia, za uchungu, au za machukizo niliyo nayo kwako. Siwezi kamwe kubadilisha ulivyonitendea, au uliyoniambia. Hayo ni ya kale. Huwezi kubadilisha. Hata hivyo, naweza kubadilisha tabia yangu kulingana na hayo uliyonifanyia. Hii ndio maana halisi ya kusamehe. Kundoa Machukizo Naamua kukusamehe. Naamua “kufutilia mbali” chuki na uchungu. Wakati fulani nilisikia kusamehe ikielezwa kuwa “kupasua orodha ya deni.” Orodha ya deni ni karatasi ambayo imetiwa sahihi na anayedaiwa, kuonyesha kwamba atalipa deni. Aliye na karatasi hiyo yenye orodha amemfanya anayemwia kuwa na hatia ya deni. Ile orodha ya deni ni swala kati yao. Kusamehe ni kupasua orodha ile ya deni. Wengi wetu wana orodha ya madeni ya watu wengine. Katika mioyo yetu kuna kinyongo, machukizo, na chuki ambazo zimekolea kwa miaka mingi. Vitu hivi vinatuzuia kuwa na upendo wa kweli na ushirika na wale ambao hatujawasamehe. Msamaha wa kweli ni hapo ninapopasua orodha yangu ya deni, na kuamua kwamba deni hilo tayari limelipwa. Hilo linakuwa si swala tena. Hatuwezi kusahau kabisa yale yaliyotendeka, lakini tunaweza kuamua matokeo yake. Uchungu wa moyo wako utamalizika. Hii ndio msamaha. Mungu anahitaji tuishi hivyo. Katika mfano wa maombi ambayo Yesu alituonyesha, aliomba akisema, “Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye” (Luke 11:4). Msamaha Kamili Ikiwa wewe na mimi tunahitaji ushirika na Mungu katika maombi, basi ni lazima tuwe na hakika kwamba hakuna mng’ang’ano wowote katika mioyo yetu ambayo hatujatatua. Yesu akasema, “Unaposimama kusali, samehe, ikiwa una jambo dhidi ya yeyote.” Bwana wetu anatarajia tusamehe kabisa kwa wingi. Haifai kuchagua tutakayesamehe, na tutakayekosa kusamehe. Pia haifai kuchagua ni kitu gani tutasamehe au kitu gani tutakosa kusamehe. Tunahitaji kusamehe bila kujali hatia iliyoko, au mkosaji. Hili ni jambo gumu sana. Watu hututia uchungu, hutuumiza, na kututumia vibaya. Ni rahisi kuchukizwa na mng’ang’ano, badala ya kuutatua. Kumbuka kwamba Yesu hakusema kuendelea kusamehe watu kutakuwa rahisi. Huku “kwenda maili saba zaidi” na “kusamehe sabini mara saba” si kwa walio dhaifu na wenye imani duni. Ni wale tu walio na upendo wa Mungu kwenye vilindini mwa nafsi zao ambao wanaweza kusamehe kabisa, na kwa wingi. “Kukosa ni kibinadamu, lakini kusamehe hutokana na Mungu.” Nguvu Iwekayo Huru Mwanamke mmoja alinieleza matukio yaliyosababisha kuvunjika kwa ndoa yake. Mumewe alikuwa amemuumiza sana. Nilipoendelea kusikiliza, moyo wangu ulishikwa na ghadhabu dhidi ya mtu huyu aliyemtendea mke wake kiimla. Nilielewa kwa nini mwanamke huyu alimchukia . Nilipomwambia amsamehe, macho yake yalijaa hasira sana, akisema, “Siwezi. Hata kamwe, siwezi kumsamehe!” Kwa shida nyingi nilijaribu kumweleza kwamba chuki aliyokuwa nayo haikuwa na uwezo wa kumdhuru aliyekuwa mme wake, isipokuwa kumwangamiza yeye mwenyewe. Kusamehe humfaidi anayesamehe na anayesamehewa. Chuki, ghadhabu, hasira na kukataliwa ni mambo ya kinyume ambayo yatatuharibu. Mungu angependa kutuweka huru kutokana na mapepo haya ili tuweze kuponywa, na kuendelea kuishi maisha yetu. Ndio sababu Mungu ametuamuru tusamehe. Anahitaji tusamehe. Anatupenda, na anatamani tuwe na afya katika akili zetu, na pia tuwe na furaha. Zaidi ya hayo yote, angependa kuwa na ushirika pamoja nasi. Angependa ushirika huo uwe bila kizuizi chochote. Anaelewa kwamba mwanadamu hawezi kumpenda Mungu ambaye hajawahi kumwona, ikiwa hawezi kumpenda ndugu yake ambaye amemwona (1 Yohana 4:20).93 Funguo la Amani Uhisano wote wote wa kibinadamu hutegemea msamaha. Hakuwezi kuwa na amani miongoni mwa watu bila kuwa na msamaha. Mara kwa mara tunasikia watu wakisema, “Nitamsamehe akisikitika. Siwezi kumsamehe akiniomba msamaha wakati wowote.” Je, umewahi kuwa na hisia hizo? Msamaha si tendo lililo kimya. Lina matokeo. Mungu anatufundisha kwamba ni lazima tusamehe bila masharti yo yote. Hasemi, “akisikitika.” Mungu hahusiki nasi hivyo, na kwa hivyo hatuhitaji kuhusiana na wengine hivyo. Ulimwengu wetu ungekuwa katika hali mbaya kabisa ikiwa Mungu angengoja mwanadamu mwenye dhambi aseme, “Nimesikitika” ndipo aamue kutusamehe. Hebu tusisahau kwamba “tulipokuwa tungali wenye dhambi, Kristo alitufia” (Warumi 5:8). Wakati tulikosa kumtafuta Mungu, ama msamaha wake, alitupenda bila masharti, na kutusamehe. Kristo alikufa kwa ajili ya adui zake. Toba hutangulia msamaha. Kama Mungu hangetuonyesha upendo wake mkuu, hatungeweza kuwa na ujasiri ya kuamini kwamba tungesamehewa. Mwana wa Mungu, akifa msalabani alisema, “Baba, wasamehe” – hiyo huturejesha kwa Mungu. Hivyo ndivyo tunavyostahili kuwapenda wengine. Tunasamehe iwapo wanahitaji, au kutafuta upendo na msamaha wetu. Mara nyingi nimeona ikitendeka hivi: aliyekosewa anapomwendea mkosaji kwa upendo, moyo wa mkosaji hubadilishwa na kuwa na amani. Kwa Upande Moja, Bila Masharti “Mnaposimama kuomba, samehe…” Haya ni maneno yenye nguvu kutoka kwa yule aliyethibitisha kwamba yanawezekana. Kuna thamani kujua kwamba “aliyedharauliwa na kukataliwa na watu” ametupenda na kutusamehe. Kwa kufuata mfano wa Kristo, ni lazima tusamehe bila masharti. Kusamehe kwetu kusitegemee kuombwa au kutoombwa msamaha na wanaotukosea. Tusiwawekee hatia. Lazima tutupilie mbali hatia ili tuwe na amani katika fahamu zetu, na amani kwa Mungu. Matokeo ya Kutokusamehe Kwa kuonyesha matokeo mabaya ya moyo usiosamehe, Yesu alitoa mifano ya wazi katika kueleza ukweli huu. Kwa kutilia mkazo alituonyesha jinsi jambo hili ni muhimu kwa Mungu. Uchungu na machukizo husababisha matokeo mawili mabaya. Kujiweka Gerezani Tokeo moja la kutokusamehe limefundishwa katika mafundisho ya Yesu mlimani. Katika Mathayo 5:23- 26, Yesu anasema: “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshtaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.” Maandiko hayo yameweka jambo hili dhahiri mno! Unapoenda kuabudu, na ukakumbushwa na Mungu kwamba ndugu yako ana neno juu yako (kwa sababu umemtendea kitendo), Yesu alisema kwamba umwendee ndugu yako mara moja na kuomba msamaha. Je, itakuwaje ukikataa kupatanishwa naye? Wewe mwenzangu, utajiweka gerezani. Katika vifungu vya 25 na 26, Yesu anamaliza kwa kusema kwamba ukikataa kupatana na mshtaki wako “upesi”, basi utajiweka gerezani, na hutatoka hadi ulipe deni. Je, unadaiwa deni ipi? Ni deni ya kusamehe. Kukosa kusamehe, au kupatana na mshtaki wako ni swala nyeti kati yako na Mungu kwa sababu itakutenganisha na Mungu na kukuweka katika gereza la kiroho. Wakristo wengi wamefungwa kiroho kwa kukosa kulipa deni zao. Hii ni hatari!94 Kuweka Wengine Gerezani Yesu alisimulia kisa kingine ambacho kilitilia mkazo matokeo mabaya ya watu kukataa kusamehe: “Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, akalipwe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia; akamkamata, akamshika koo, akisema, Nilipe uwiwacho. Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa ile deni. Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi; nawe, je? Haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake. Mfano huu ni kati ya mifano mirefu zaidi na yenye ufafanuzi zaidi kuwahi kuandikwa katika vitabu vya injili. Imeandikwa kwa ukali. Mtumishi mwovu, aliyesamehewa kiasi kikubwa cha deni ya dola milioni kumi na bwana wake. Amekataa kumlipa mjoli wake kiasi kidogo cha dola 18, na akamweka gerezani kwa sababu ya deni hilo ambalo halikulipwa. Huyu mtumwa alikuwa mtu asiyekuwa na shukrani wala huruma! Amesamehewa, naye akakataa kuwasamehe wengine. Je, unafahamu mtu yeyote kama huyo? Hiki ni kisa cha kawaida, ama sivyo? Unapokosa kumsamehe mtu mwingine, unamweka gerezani. Hii inamaanisha kwamba umemfunga kwamba hawezi kuwa rafiki yako. Hawezi kukubariki au kukusaidia kwa sababu umemhukumu. Kukasirikia Watu Je, umewahi kukasirikia mtu bila sababu? Je, umewahi kumkasirikia mtu ukaona huwezi kumpenda au kumkubali bila kuwa na sababu? Unamkasirikia tu bila sababu. Nini hutendeka basi? Huyo mtu huwa gerezani kwa sababu umemweka huko. Watu wengi hufanya wachungaji hivyo. Labda amefanya kitu wasichokipenda, au kukubaliana nacho. Je, huyo mchungaji anaweza kuwahudumia kweli? Je, anaweza kuwahubiria neno la Mungu? Hawezi kamwe! Umemweka kifungoni. Umemfunga, na hawezi kukuhudumia. Inawezekana asiweze kufahamu hisia zako kwake, na kutofahamu kuwa umemweka gerezani. Ni vyema tuyazingatie maneno ya Yesu: “Ndivyo na Baba yangu wa Mbingu atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.” Katika Kuomba Tumruhusu Mungu atufundishe kanuni hii mara nyingi: hatuwezi kuwa haki kwa Mungu, hali tu wabaya kwa wenzetu. Tunapokosa kusemezana, naye Mungu hawezi kusema nasi. Amini hayo, yajue hayo na utende kitu kuhusu jambo hilo. Usiruhuru chochote kuharibu nafasi yako kwa Mungu na uwezo wako katika maombi. “Unapoomba, samehe!”95 Michango 1. Kifungu cha 26 kimewekwa kwa kifungo, au kuwekwa kwa upande katika The New American Standard Bible kwa sababu hakikuandikwa kwa maandiko ya kwanza ya Injili ya Marko. Lakini Yesu amefundisha kanuni hii katika maandiko mengine, kama vile ilivyoandikwa katika Mathayo 6:15 na 18:35.9697


 MUNGU ANAPOKOSA KUJIBU MAOMBI YANGU 


Shida kuu la maombi katika kanisa la sasa si ukosefu wa majibu kwa maombi, bali ni maombi yasiyoombwa. Hatupati kwa sababu hatuombi. Swali kuu ambalo limewahi kuulizwa kuhusu maombi ni hili: Mbona Mungu hajibu ninapofikiri nimetimiza mapenzi yake? Hata aliye mwadilifu wa watakatifu wote mara nyingi huona kwamba Mungu hasikii maombi yake anapoenda kuomba. Hii inawezekana hata ingawa umedai ahadi za Mungu kutoka kwa maandiko. Wakati mwingine hata theologia unayofahamu, na uthabiti uliyoweka katika maombi “sahihi” hayana matokeo unayokusudia. Je, utafanya vipi? Yesu alitoa mfano unaohusu maombi, ambayo inajibu vyema swali hili. Imeandikwa katika Luka 18:1-8: “Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu siku zote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima. Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani? Mfano huu ni wa kadhi ambaye hakumcha Mungu wala kumheshimu. Yeye mlaghai kweli, ijapokuwa ni kadhi. Hana moyo wa huruma kwa wajane, lakini alipoona kwamba huyu mwanamke mjane habadiliki, akampa haki yake akisema, “asije akanichosha.” Kitu kinachonishangaza katika mfano huu ni kwamba Mungu anafananishwa na huyu kadhi mlaghai. Tunahitajika kuwa kama huyo mjane. Tunahitaji kuomba bila kukoma au kukata tamaa. Tumwendee Mungu kila mara katika maombi na ujasiri wa huyu mjane mbele ya kadhi mlaghai. Kwa kweli Mungu si kama huyu kadhi kwa hali zote, isipokuwa mbili: Kwanza, Mungu anaheshimu maombi ya dhati kama vile kadhi alivyoendewa mara kwa mara. Pili, Mungu atatupa haki yetu ikiwa tutazingatia na kuomba kwa dhati. Usichoke Mara nyingi maombi ambayo tulidhani hayakujibiwa ni maombi ambayo tulikatisha. Hatukuweka bidii. Hatukutafuta haki kama huyu mjane alivyotafuta. Hii ni kweli katika kuombea watu waliopotea dhambini. Ni lazima tuombe hadi waokolewe. Hi ni kweli katika kuombea jambo lo lote lililo katika mapenzi ya Mungu kama ilivyoandikwa katika maandiko. Yesu akasema, “Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? (Luka 18:7). Hayo maneno yanamaanisha kwamba Mungu anatamani kutujibu na kututendea haki. Lakini kuna mambo ulimwenguni yanayomsababisha kuchelewesha majibu yake na kusababisha watu wake kudumu katika maombi. Maombi Na Mungu Mwenye Enzi Wakati fulani nilikuwa na kikundi cha watalii kule Israeli. Tulitembelea makavazi yaliyoonyesha jinsi Wayahudi walivyoangamizwa. Wayahudi kadhaa katika kikundi chetu walitatizwa sana na ratiba ya picha zilizoonyesha unyama waliotendewa Wayahudi na Wanazi, walipokusanywa kwenye kituo. Wengine walikasirika. Tulipokuwa tukiketi sebuleni na kuongea, mwanamke mmoja Myahudi kutoka Florida98 aliniambia, “Mungu alikuwa wapi wakati Wayahudi walimhitaji huko Yuropa?” Swali kama hilo kweli hututikisa! Kwa kweli mamilioni ya Wayahudi waliomba Yehova Mungu – Mungu wao. Mungu wa Ibrahimu, Isaka, na Yakobo alikuwa wapi? Aliruhusu wendawazimu wa Hitler kuwatendea unyama watu wake wateule. Mioyo yetu hulia, tukiuliza “Kwani nini? Kwani nini? Kwani nini?” Kuona nyuma ni bora kuliko kuona mbele. Historia imetudhibitishia mamlaka ya Mungu katika uaminifu wake kwa Wayahudi. Alisikia kilio chao na kuwakomboa. Amewatendea haki. Wengi watashuku usahihi wa maneno hayo, lakini ni kweli hata hivyo. Mungu, kwa mapenzi yake, aliruhusu Wayahudi kufanyiwa unyama, ili atimize kusudi lake kamilifu kwa taifa la Israeli. Tulipoketi kwenye jumba hilo la maonyesho ya jinsi Wayahudi walivyoangamizwa, nilimweleza yule mwanamke wa Kiyahudi aliyekuwa amekasirika sana hivi, “Je, umewahi kufikiri hivi: Kama hakungekuwa na unyama huo, basi hakungekuwa na taifa la Israeli. Wayahudi waliosalia kule Yuropa hawakuwa na mahali pengine pa kwenda. Walilazimika kwenda Palestina. Basi hapo pana nchi ya kitaifa kwa Wayahudi.” Aliniangalia kwa mshangao na kusema, “Sijawahi kufikiri hivyo.” Nikasema, “Mungu huunda mazuri kutokana na mabaya, na hasa inapolingana na makusudi yake.” Ni Mungu Wa Haki Tunapoendelea kushangaa kwa nini Mungu hatendi kulingana na ratiba yetu, ama kujibu maombi jinsi tunavyodhani anastahili kujibu, kumbuka kwamba anaona “picha kubwa” wakati ambapo tunaona tu “picha ndogo.” Darubini anayotumia ni kubwa, bali sisi tunaona kutumia darubini ya kuonea vitu vidogo sana. Ni lazima tusadiki kwamba “Baba anayafahamu yaliyo mema” na kwamba kila mara atafanya yaliyo mema. Tuwe kama yule mjane aliyekwenda kwa kadhi akidai “haki,” akiamini na kutulia kwa mapenzi ya Mungu mwenye enzi. Yesu alimaliza kusimulia kuhusu kadhi mlaghai kwa kuuliza swali hili, “walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?” (Kifungu cha 8). Kwa hakika, maombi yetu kuhusu amani, upendo, na undugu ulimwenguni hayawezi kujibiwa mpaka hapo Mwana wa Adamu atakaporejea. Kisha kila moja wapo ya maombi hayo yatajibiwa! Tuamini kwamba makusudi yake yanatekelezwa kwa kujibiwa kwa maombi yetu. Hebu tumsumbue kadhi wa walimwengu ambaye kwa kweli ni Baba Wetu aliye mbinguni mwenye mapenzi tele! Kuna sababu nyingine zinazosababisha maombi yetu kutojibiwa, au kutupa jibu “la” kutoka katika kiti cha enzi cha mbinguni. Katika kitabu kingine, niliandika kuhusu maombi yasiyojibiwa kutokana na kitabu cha Yakobo sura ya 4, ambapo tunaona sababu tatu zinazosababisha Mungu kutojibu maombi yetu. Hebu angalia katika sehemu hizi unapoona kwambu Mungu hajibu maombi: Nje. Tazama maombi yako. Yakobo 4:3 inasema “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumia kwa tamaa zenu.” Mungu hawezi kujibu ombi lilioombwa vibaya kwa jibu sahihi. Mara nyingine hatuombi kulingana na mapenzi yake. Ndani. Chunguza maisha yako. Huenda ikawa maisha yako si sahihi. Katika Yakobo 4:4, anaita aliyowaandikia “wazinzi.” Kumbuka, ni maisha yaombayo. Juu. Mtazame Mungu. Anaweza kuwa anajibu maombi yako lakini hata hutambui. Anaweza labda kuchelewesha jibu, au kuijibu toauti kuliko unavyotarajia. Michango 1. Tazama Sura ya 9 katika Questions New Christians Ask (Old Tappan, New Jersey: Fleming H. Revell99

KUJIFUNDISHA KUOMBEA WALIOPOTEA DHAMBINI “

Uinjilisti ni nini? Ni kujibwaga tu kwenye uwanja wa vita na kuchukua nyara zinazotokana na ushindi uliopatikana katika maombi.” Je, umewahi kusikia mtu kanisani akiomba hivi: “Oh, ndiyo Bwana. Iwapo kuna watu hapa ambao hawajaokoka, uwaokoe wote. Amin” Maombi kama hayo ni kama kumsikiliza mtoto mchanga akiomba kabla kulala, akisema “Mungu, okoa watu wote ulimwenguni. Amin.” Maombi hayo kwa kweli yanavutia, na yana mwongozo wa roho mtakatifu! Je, kuna mbinu fulani inayohitajika ili kuombea wengine waokoke? Kuomba ukiwa na ufahamu wa Bibilia kunaweza kukuridhisha katika kuombea watu wengine. Mungu anashauku ya kuwaokoa waliopotea katika dhambi. Anaweza kuwaokoa tu kupitia kwa kujitolea kwetu kuwaombea hao waliopotea dhambini. Mungu wa Kusita? Kuna watu wanaofundisha kwamba maombi yetu hayana maana kwa Mungu. Ikiwa ni hivyo, basi kitabu hiki hakina manufaa kwetu na kukiandika ni hasara. Tutakuwa tumepoteza muda wetu bure. Wengine wamehisi kwamba kuwaombea waliopotea dhamibini ni kumwomba Munga ambaye hajali na hahusiki katika kuwaokoa wale tunaowaombea dua. Hivyo sivyo tumwonapo Mungu aliyeelezwa katika maadiko. Kama vile Ibrahimu alivyoombea Sodoma hadi Mungu akawa tayari kuuokoa mji huo iwapo kungepatikana angalau watu kumi waadilifu, ndivyo Yesu anavyotuambia kwamba alitumwa na Baba wa mbinguni aliyejawa na mapenzi tele ili kutafuta na kuokoa waliopotea. Paulo alitumwa na Mungu “ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli” (1 Timotheo 2:4). Petero pia alithibitisha mapenzi ya Mungu kwa waliopotea dhambini alipoandika kwamba “Bwana hakawii kutimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu yeyote apotee, bali wafikilie toba.” (2 Petero 3:9). Jinsi Ya Kuombea Waliopotea Kuombea waliopotea ni dua maalumu. Tunapoombea rafiki zetu ambao hawajaokoka, ni heri tuelewe kwamba Mungu ana nia zaidi ya kuwaokoa, kuliko tunavyowaombea. Tunaamini ahadi ya Mungu ya kuokoa waliopotea. Lakini, tunastahili kuwa na ufahamu katika kuomba. Tutumie vifaa ambavyo Mungu ametukabidhi. Ametupa funguo za uflame ili tuweke huru waliosetwa. Tuna kazi ya “kufunga na kufungua.” Kuombea waliopotea , kwa hakika, ni vita vya kiroho. Si kumsihi Mungu tu. Tunastahili kuyaelekeza makombora yetu kwanza kwa shetani; pili ni kuomba ushawishi wa roho mtakatifu; na tatu ni kuweka hoja zetu mbele ya kiti cha enzi cha Mungu Baba. Adui Na Mateka Wake Shetani, ambaye ni adui wetu nambari moja, hupinga na kuzuia wokovu kwa watu ambao wamepotea. Amewateke nyara na kuwafanya vipofu kwa injili. Wanaishi gizani kiroho, na kwa hivyo, wanahitaji kuona mwangaza wa injili. Pia wanahitaji kufunguliwa minyororo ya shetani, na kuwekwa huru. Mtu aliyepotea hawezi kuona ukweli “…injili yetu imesitirika…kwa hao wanaopotea, ambao ndani yao Mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasiamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wa Kristo …” (2 Wakorintho 4:3-4).100 Aliyepotea dhambini ni mtumwa ambaye ni mateka wa shetani “…ili kama ikiwezekana, Mungu awape kutubu na kujua kweli, wapate tena fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye, hata kuyafanya mapenzi yake.” (2 Timotheo 2:25,26). Hali ya upotevu ni hali mbaya mno. Zamani tulikuwa hivyo, yaani wafungwa na vipofu. Hii ndio sababu mtu asiyeamini huona mambo ya roho kuwa mambo yasiyopendeza. Amepofushwa, asione ukweli. Wakorintho Wa Kwanza 2:14 inatueleza kwamba mambo ya roho ni upuzi kwa mtu kama huyo. Ni Yesu pekee, na nguvu za Roho Mtakatifu, ambaye anaweza kufumbua macho yake aweze kuona ukweli. Basi tunastahili kuombea waliopotea badala ya kuwahukumu. Mtu ambaye hajaokoka ni kipofu na mateka katika dhamira yake. Kwa kuwa akili zake zimepofushwa, anahitaji ufunuo ili aweze kubadilika. Mabadiliko haya yanawezekana tu ikiwa tutajitolea mhanga kumwombea dua kwa Mungu. Ushahidi wetu huwezi kuwa wenye maana iwapo mwenye dhambi hatabadilika. Hawezi kusikiliza tumwambiavyo, na kumpokea Kristo kama angali chini ya mamlaka ya shetani. Maombi kabla ya uinjilisti yanaweza kubadilisha hali ya mpotevu. Ushindi Hatupaswi kamwe kukata tamaa na kuwaacha rafiki zetu kutokomea dhambini. Wamekwisha kombolewa. Kumbuka masomo yetu katika Wakolosai Sura ya 2. Yesu alimshinda na kumpokonya silaha zake mbili ambazo ni dhambi zetu, na mshahara wa dhambi, ambayo ni kifo. Waraka wa Kwanza Wa Yohana 3:8 inatufahamisha kwamba “…kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi.” Jukumu letu ni kutumia ushindi huo kama silaha yetu katika maombi. Waliopotea wangali wapotevu hata ingawa shetani alishindwa kutokana na kufa na kufufuka kwa Yesu Kristo. Wangali mateka wa shetani. Ukombozi wao unaweza kupatikana tu kupitia dua zetu kwa niaba yao. Uhuru wao utapatikana tu ikiwa shetani ataamrishwa kuwaachilia katika jina lenye ushindi la Kristo. Kushindwa kwa shetani, na kutimuliwa kwake kutoka kwa moyo wa binadamu na fikira zake, kutategemea uthabiti wetu dhidi ya shetani. Ni wajibu wetu kutumia funguo za mbinguni, ambazo ni silaha ya maombi kwa kuvuta waliopotea wamjie Kristo. “Maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome.” Kudai Deni Unapomkemea Ibilisi, kumbuka kwamba una haki kumdai rafiki yako aliyepotea dhambini. Yesu tayari amelipa deni ya ukombozi kwa watu wote. Hao si mali ya shetani tena. Unapomkemea shetani ukitumia mamlaka uliyopewa la jina la Yesu, na kushambulia malango ya kuzimu, shetani lazima atatii. Amini ukidai na kuomba katika jina la Yesu! Zaidi Ya Kukemea Kuombea waliopotea ni zaidi ya kukemea adui. Ni kujibwaga kitini pa enzi na kuomba kwa thati kwa niaba ya mpotevu. Mimi huombea mambo mawili ninapoombea waliopotea. Baada ya kumwondosha Ibilisi vitani kwa siku hiyo kwa maombi, humwomba Mungu atume mtu kumshuhudia rafiki yangu ninayemwombea. Kwanza namwomba Yesu mwenyewe amtembelee . Roho Mtakatifu atakuwakilisha kwa mtu huyo ikiwa utamwomba kufanya hivyo. Itakubidi kumwomba roho mtakatifu kila siku kukaripia, kukemea na kushawishi mwenye dhambi kuona hitaji lake. Pili, mwombe Mungu amtume mtu anayeweza kumshuhudia injili. Hi inaweza kuwa kwa njia ya runinga (televisheni), kijitabu cha injili (gospel tract) ambayo labda anaweza kuokota, au hata kupitia kwa mtu fulani asiyemfahamu. Ndiyo, hiyo ni kazi ya Mungu kutenda, lakini tunastahili kumwomba atume wafanyi kazi kwa mavuno (Mathayo 9:38). Tukiomba kwa ufahamu, tutagundua kuwa ni rahisi, mradi tu “tuombe kwa ufahamu.” Ifuatayo ni jinsi tunavyoweza kuombea waliopotea: 1. Kemea adui. Omba, “Ibilisi, naja kinyume chako kwa niaba ya rafiki yangu _____________________. Katika jina la Yesu nakuamuru umwachilie na utambue kwamba101 yeye si wako tena, bali ni wa Bwana Yesu. Kwa hivyo nadai wokovu wake katika jina la Yesu.” Lazima upigane kila siku hadi wokovu upatikane. Jipe moyo. Shetani anapotambua ujasiri wako, atatoroka. Lakini hawezi kutii ikiwa imani yako ni hafifu, na kudumisha uombezi wako. 2. Omba Roho Mtakatifu afanye kazi ya Kumshawishi. Omba Yesu amtembelee rafiki yako leo. Unaweza kuomba hivi: “Bwana Yesu, nakuhitaji ubishe katika moyo wake. Mwonyeshe upendo wako. Fumbua macho yake, na kusema naye leo.” 3. Omba Mungu awatuma Waumini. Unaweza kuomba hivi: “Baba, tuma mtu wa kumshuhudia rafiki yangu. Mzingire na upendo wako. Mwonyeshe mtu atakayekuwa mfano bora kwa maisha yake na kumfanya kuwa karibu nawe.” 4. Shukuru Mungu kwa Wokovu Wake. Dai Yohana 5:14. Amini kwamba rafiki yako anaokolewa. Mshukuru Mungu kwa wokovu wa rafiki yako. Kisha mwachie Mungu atende kazi yake ya kuokoa kwa wakati wake mwenyewe. Lakini zidi kuomba, na kubisha, naye ataokolewa.102103 NAWEZAJE KUWA MWOMBEZI? Mwombezi wa kweli ameishi na kujifunza kwamba sheria ya mavuno ya kiroho hutokana na kifo. “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi.” -Yohana 12:24 Karibu miaka arobaini na mitano iliyopita, Daktari S.D. Gordon aliandika maneno ya changamoto yafuatayo: Watu shupavu ulimwenguni leo ni wanaosali. Si elezi kuhusu watu ambao wanaongea juu ya maombi; ama wale ambao wanaweza kueleza wazi wazi maana ya maombi. Naongea juu ya watu ambao wanatafuta wakati wa kuomba. Hao ndio wanaomtemdea Mungu kazi nyingi katika kuwavuta watu kwa Yesu, kutatua matatizo, kuleta uhuisho makanisani, kujitoa mhanga kibinafsi na kwa fedha kwa kazi ya umisheni, kuwapa changamoto wale ambao wamejitolea kwenda vitani mahali ambapo vita ni vikali, ili ulimwengu wetu udumu, ukiwa wenye maana zaidi. Maneno hayo ni ya ajabu sana. Je, umeona kwamba ni mwombezi anayefanya ulimwengu kuwa wa maana kuudumumisha zaidi? Kudumishwa na kufanywa kuwa yenye maana kwa ulimwengu huu hakutokani na serikali, elimu, utamaduni ama cho chote ambacho mwanadamu anaweza kutenda. Ni maombi ya dhati ndiyo yanaweza tu kutenda hayo. Je, ungependa kuwa moja kati ya watu hao washupavu ambao Mungu angependa kutumia kutimiza makusudi yake duniani? Si tu kusoma kuhusu maombi, ama kuongea juu ya maombi, bali ni kuomba kwa kweli. Kama tulivyoona hapo mbeleni, maombi yanaweza kuchukua hali tofauti. Yanaweza kuwa ni mazungumzo yako na Mungu Baba. Maombi ya kushirikiana na Mungu katika mazungumzo ni muhimu sana. Ni muhimu kupata mahali penye kimya na kuwa na muda wa faragha na Mungu, ili kumsifu na kumwabudu. Inayozidi yote ni kuisikiliza ile sauti ya upole ndani ya roho yako, ili siku yako iwe chini ya mwongozo wa Mungu. Pili, katika maombi unaweza kumwomba Mungu mahitaji yako binafsi. Ni mwenye dhambi ambaye anamwomba Mungu msamaha wa dhambi na mahitaji ya kila siku kwa unyenyekevu. Mombi pia yanaweza kuwa dua kwa niaba ya watu wengine. Watu ambao huingia katika huduma ya maombi huwa wameingia katika utumishi mkubwa kabisa hata kukaribia Patakatifu pa Watakatifu. Kuwa mwombezi ni kujitambulisha na Yesu ambaye ni mwenye upendo na huruma kwa ulimwengu uliopotea dhambini. Maombi ya ushirika (Communion) ni ya kibinafsi - kwa maana yananihusu mimi. Maombi ya sala (petition) pi ani ya kibinafsi – kwa maana hunifikia ndani. Maombi ya uombezi (intercession) yanahusu mambo ya nje ya mwombaji, na hubadilisha ulimwengu mzima! S.D. Gordon huita uombezi kilele cha maombi. Anamaanisha kwamba kupitia maombi (Ibaada) Mungu anaweza kutugusa ili atutumie kuugusa ulimwengu. Kwa maombi na dua, tunaweza kujazwa nguvu zake. Basi nguvu hizi zinadhihirika katika kuwaombea watu wengine. Huwezi kuwa mwombezi ikiwa hujakwea mlimani na kukutana na Mwenyezi Mungu. Mtu anapokutana na Mungu basi yeye huweza kuhudumia kabisa ulimwengu uliopotea kwenye dhambi, kwa maana Mungu mwenyewe anauombea ulimwengu wetu. Kuwa karibu na Mungu ni kushiriki mzigo wa moyo wake kwa ulimwengu uliopotoka. Waingiao katika huduma hii ya uombezi ni watu “walioona mwangaza” nafsini mwao ili wauone ulimwengu ulivyo gizani. Kuwa Mwombezi Je, mtu yeyote anaweza kujiunga na huduma hii? Tunaweza kujibu hivi: ndiyo, na sivyo. Tunapotazama maandiko, tunafundishwa kuombea wengine. Paulo anatuambia tuombe “…kwa ajili ya watu wote, kwa104 ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka …” (1 Timotheo 2:1-2). Mkristo anastahili kuombea “watu wote”. Kila mkristo mwaminifu anastahili kuishi maisah ya uombezi. Lakini si wakristo wengi wanaoweza kuwa mashujaa wa maombi, ambao wamejitolea mhanga kwa Mungu, na kuishi maisha ya kuombea watu wengine. Waombezi ni wale ambao wamejiunga na Mungu katika kutambua kwamba ulimwengu umepotea na unahitaji kukombolewa. Huduma hii si ya watu hafifu wa moyo ama wale walio dhaifu katika imani yao. Wateule Huduma ya kuombea watu ni huduma ya watu walioteuliwa. Washiriki wake ni wachache, wakiwemo watu mashuhuri, na wasiotambulika. Musa aliteuliwa katika huduma hii. Alitoa maisha yake vilivyo kwa Mungu. Alisimama “katika pengo” kwa sababu ya taifa. Alikuwa tayari kutoa uhai wake kuzuia ghadhabu ya Mungu iliyowaka dhidi ya Waisraeli walioasi. Akiwa ameweka maisha yake hatarini, aliomba hivi: “Aa! Watu hawa wametenda dhambi kuu. Wamejifanyia miungu ya dhahabu. Walakini sasa, ikiwa utawasamehe dhambi yao – na kama sivyo, unifute, nakusihi, katika kitabu chako ulichoandika” (Kutoka 32:31,32). Paulo, mtume mpendwa, amehitimu kuwa katika kikundi hiki. Alijitwika mzigo wa taifa lililopotea la Wayahudi. Katika kitabu cha Warumi, alikiri hivi: “Ndugu zangu, nitakayo sana moyoni mwangu, na dua yangu nimwombavyo Mungu ni kwa ajili yao, ili waokolewe” (Warumi 10:1). “Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika roho mtakatifu, ya kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu kwa maana ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili” (Warumi 9:1-3). Tunaona mtu ambaye alitambua upotevu na uchungu wa watu wengine kiasi cha kutoa uhai wake kwa ajili yao. Hicho ndicho kiini cha maombezi, na kilele cha maombi. Paulo alikuwa mwombezi shupavu. Katika Matendo Ya Mitume 20:21 aliwakumbusha Waefeso kwamba “mkikumbuka kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi.” Paulo alikuwa ni mwalimu, mmisheni, mtume, mwandishi, na muinjilisti. Hayo, yalikuwa ni kando na mwito wake halisi, ambayo ilikuwa ni uombezi. Yesu, Mwombezi Wamfuataye Bwana huanza kufanana naye. Karne nyingi kabla Yesu kuzaliwa, nabii Isaya alimtaja kuwa ni mwombezi. “Kwa hivyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari, kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi” (Isaya 53:12). Bwana wetu Yesu ndiye Masihi wa ahadi. Kwa kweli alikuwa ni mwombezi hodari aliyeishi, aliyependa, aliyeomba na kufa kwa niaba ya wengine. Katika Luka Mtakatifu 22:32, Yesu alimwombea Simoni Petero ambaye Yesu alijua atamsaliti. Alisema, “Simoni, nimekuombea ili ukibadilishwa, utunze kondoo zangu.” (Maneno ya mwandishi). Katika Yohana sura ya 17 tunaona sala ya Bwana. Tunaona maombi ya ukuhani wa Kristo katika kuombea kanisa lake. Anaombea wafuasi wake na wale ambao wataokolewa karne nyingi baadaye kutokana na ushahidi wa wafuasi hao, tukiwa miongoni mwao. Yesu alikuombea, rafiki yangu. Aliniombe pia. Alikuwa mwombezi, si katika uhai wake tu, bali hata katika kifo chake. Alihesabiwa pamoja na waasi, naye akawaombea. Alipokuwa akifa msalabani, aliomba kwa105 Mungu akisema, “Baba wasamehe, maana hawajui watendalo” (Luka 23:34). Mwombezi wetu shupavu aliombea wengine hata katika kifo chake msalabani. Yesu Kristo hivi sasa ameketi mkono wa kuume wa Mungu akituombea! Waebrania 7:25 inatueleza hivi kuhusu Bwana Yesu: “Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” Kitu ambacho ni cha maana sana kwa Kristo kwa wakati huu ni maombezi. Yesu anatuombea wakati huu, na anaishi makusudi ya kutuombea. Yeye ni mwombezi wetu! Maisha na Usemi Je, unawaombea watu wengine kwa uaminifu? Kuwa mwombezi ni huduma iliyo ngumu sana, kwa sababu kwa kawaida, sisi hujipenda. Kuishi maisha ya maombi tu ndio kutatuwezesha kuombea wengine. Hii inamaanisha kwamba ni lazima tutambue udhia za watu wengine ikiwa tutawaombea kikamilifu. Wazazi hujali watoto wao, na kwa hivyo huwaombea. Vivyo hivyo, tunapowajali wengine, basi tutawaombea kwa kutambua dhiki zao. Hatuwezi kuombea watu wengine isipokuwa kwa kuishi maisha ya maombi. Kutambulikana Musa aliwaombea wana wa Israeli kwa sababu alijitambulisha nao kama moja wao. Alichukua jukumu la wana wa Israeli waliotangatanga jangwani kama lake. Aliwajibika katika dhambi zao, kuasi kwao, na mahitaji yao. Kwa sababu hiyo aliwaombea. Bwana Yesu alikuombea. Aliniombea pia. Akiwa Masihi, na pia mwokozi, alihesabiwa pamoja na waasi. Hiyo inamaanasha Yesu alijitambulisha na dhambi za walimwengu. Yesu alipomwendea Yohana mbatizaji ili abatizwe naye (Mathayo 3:13-17), ingawa hakuwa na dhambi, Yohana kwa unyenyekevu mwingi alimjibu, “Mimi nahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu?” Lakini Yesu akamwambia, “Kubali hivi sasa, kwa kuwa ndivyo itupasavyo kutimiza haki yote.” Katika kubatizwa, Kristo alijitambulisha na dhambi za walimwengu. Alikuwa karibu sana na wenye dhambi hadi kujitambulisha nao katika ubatizo. Ilikuwa ni mfano wa yale aliyotenda msalabani - kujitwika dhambi zetu. Waraka wa Kwanza wa Petero 1:18,19 inatuambia kwamba tulikombolewa, si kwa vitu viharibikavyo kama vile fedha au dhahabu, bali kwa damu ya thamani ya Yesu Kristo. Kuombea wengine ni matokeo ya maisha ya maombi. Maisha ni lazima yapatie usemi mwelekeo. Isipokuwa nijitambulishe na wengine katika haja zao, ni vigumu sana niweze kuwaombea. Nilipokuwa chuoni, kulitokea tukio ambalo lilitikisa uliwengu wa uinjilisti. Wamisheni wengi waliuawa sana kule Marekani ya Kusini. Moja wao anayejulikana kama Jim Elliot, aliuawa na Wahindi ambao alikuwa akijaribu kuwashuhudia kuhusu upendo wa Mungu. Jim alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Wheaton, karibu na mji wa Chicago, Illinois, alikuwa kila wakati akiandika katika kitabu chake chenye habari za mambo ya kila siku (diary). Alikuwa na moyo wa kujihusisha na huduma sana hadi akaamua kuwa mmisheni. Alikuwa na lengo la kupeleka injili kwa watu ambao hawajasikia injili ya Kristo. Jim, akiwa na rafiki yake moja kwa jina Nathaniel Saint, alisikia habari za kabila moja la wahindi walioishi katika msitu wa Peru. Kabila hilo halikuwa limesikia kamwe habari za Kristo. Miaka mingi kabla kwenda kwake Marekani Ya Kusini, Jim alianza kuomba na kuandika maombi yake katika kitabu chake chenye habari za mambo ya kila siku, akimsihi Mungu ampe nafasi ya kwenda kuwahubiria kabila hilo la Wahindi kuhusu Yesu. Siku moja Jim aliandika maneno haya: “Mungu, unifanye kuwa mtu matata. Wafanye wale wanaokutana nami kuamua. Nisiwe kama kibao cha kuonyesha watu njia, bali nifanye kuwa kama uma, ili watu wanaokutana nami wageukie njia moja au nyingine wanapokutana na Kristo ndani yangu.” Jim Elliot alikuwa mwombezi. Katika uhai wake, alijitambulisha na dhiki na upoteveu wa kabila nzima la watu. Hakuomba tu, bali aliweka maombi yake katika vitendo, alipojitolea kuwahubiria Wahindi wa Quechua habari za Yesu. Kuombea watu wengine ni matokeo ya maisha ya maombi. Ni vigumu kuwa na huduma ya kuombea wengine hadi utakapoanza kujali watu. Usipokuwa tayari kuhusika katika dhiki, na kutambua mahitaji na maumivu ya wengine, basi hutaweza kulipa gharama ya kuwaombea.

 Ni Zaidi Ya Maombi 

Huduma ya kuombea wengine ni wazi kwa wale wanaoutafuta na kuwa tayari kulipa gharama yake. Huduma hii si sawa na kuombea watu tu. Mtu moja kwa jina Norman Grubb, kwa utangulizi wa kitabu

kinachoitwa The Intercession of Rees Howells, anamtaja Howells akisema, “Maombi yameshindwa. Ni maombezi tu yanayoweza kutupatia ushindi.” Hebu tazama tofauti. Maombezi ni tofauti na kuombea watu tu. Ni mara ngapi umehisi kuwajibika, ukaonyesha kujali wengine kwa kujihusisha na huduma au kuanza kuombea watu? Baada ya kitambo kidogo ukaona kwamba huwezi kuendelea. Kwa sababu gani? Ni kwa sababu hukudumisha moyo huo na shauku ya kuwaombea wengine katika maombi yako. Uombezi ni mtindo wa maisha. Si mzigo tu wa muda, ama kuwajali watu kwa muda mfupi tu. Uombezi hutokana na moyo uliovunjika. Ni matokeo ya kutembea katika roho na kukaa ndani ya Kristo. Katika kitabu cha Zakaria 12:10, Roho Mtakatifu ameitwa roho wa maombi. Hii ni kusema kwamba asili ya Roho Mtakatifu anayeishi ndani ya waumini ni kuombea wengine. Maandiko yanasema katika Warumi 8:26 kwamba Roho Mtakatifu hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Roho Mtakatifu ni mwombezi. Maisha ya Yesu hapa ulimwenguni ilikuwa maisha ya kuombea wenye dhambi. Alikufa kama mwombezi, na kuomba maombi ya uombezi. Tukimruhusu Yesu kukaa ndani yetu na kutuongoza, basi tutakuwa na asili yake. Tutakuwa na moyo wa kuombea wengine na kuishi maisha ya kuombea wengine. Tunapoishi kwa kumtii Yesu, tutaishi tukiombea watu kama vile alivyoishi. Tutaiga namna alivyoombea watu. Rees Howells na John Hyde Katika historia ya kanisa, watu wengi wamehusika katika maombezi hadi wakatambulika katika huduma hiyo ya maombezi. John Hyde aliishi maisha yake yote kule India akiwa mmisheni. Alikuwa na mzigo mkubwa sana moyoni mwake kwa ajili ya watu waliopotea. Alizingatia sana maisha ya maombi, hadi akabandikwa jina “Hyde mwombaji.” Ilisemekana kwamba Hyde “Alidhibitisha kwamba maombi yalikuwa na nguvu sana huko India kuleta watu kwa Kristo, wakati ambapo kwa imani alidai mtu moja kwa siku, kisha wawili, alafu wanne.” Rees Howells, ambaye alikuwa wa chuo cha Bibilia cha Wales, pia alikuwa mtu wa namna hiyo. Ni mbingu tu iwezayo kutambua nguvu za maombi ya Howells. Ukimtaja miongoni mwa watu wanaofahamu kanisa liombalo, watakuambia kwamba Rees alikuwa mwombezi. Ijapokuwa alikufa mnamo mwaka wa 1950, atakumbukwa daima kama mtu ambaye maisha yake aliutoa kwa kuomba. Maombezi ni njia inayopitiwa na watu wachache sana. Hewa ya maombi si sawa sana kwa wengine wetu. Ukitamani kuwa mwombezi, itakulazimu upatane sana na Kristo kiasi cha Roho wake kumiliki maisha yako. Kuishi kama mwombezi kunatokana na kudumu ndani ya Kristo. Unapowajali watu, unapowaoembea, na hata kutenga nafasi na kuacha shughuli zako ili uombe, basi Kristo anaomba kupitia kwako. Mwombezi Anafahamu Ushindi Tunapodumu katika Kristo, tutambue kwamba maombi yetu yatajibiwa. Mwombezi humwakilisha Mungu. Yeye ni mpatanishi baina ya Mungu na mwanadamu. Humwakilisha anayemwombea katika maombi. Hisia zake na uchungu anaopata, ni kwa niaba ya anayemwombea. Yeye husimama katika pengo bila kukoma, hadi ushindi upatikane. “Tukikaa ndani ya Kristo, na maneno yake yakikaa ndani yetu, tujue kwamba tuombalo lote tutatendewa” (Yohana 15:7). Mwombezi, katika kusimama imara pamoja na Mungu, ni mshindi. Mungu aongeze watu wengi kama hao katika kanisa lake. Lango la Maombezi ni wazi kwa wote walio na ujasiri wa kuingia kwenye huduma hii. Mamia ya makanisa huendelea juma baada ya juma, na mwaka baada ya mwaka, bila kuwa na waombezi ambao ni washiriki. Wapi watu wanaoweza kuomba hadi Bwana wa Mavuno arudi? Je, kuna watu unaowaombea kila siku bila kukoma? Je, kuna yeyote unayemsumbukia moyoni, ukimwombea na kusema, “Mungu msaidie huyu, ama sivyo nahisi kufa”? Je, umewahi “kusimama katika pengo” kwa niaba ya mtu yeyote? Huduma ya maombezi ni kwa wale walio tayari kuchukua mizigo ya wengine.107 Namshukuru Mungu kila siku kwa wale waaminifu wanaoniombea na kuombea huduma ambayo Mungu amenipa. Mara nyingi nimehisi uwepo wa maombi ya watu wa Mungu ninapohubiri, hudumu, na kushuhudia katika sehemu nyingi za uliwengu. Wakati fulani, kwa majuma matatu hivi, nilienda kuhudumu kule Hungary, Romania, Czechoslovakia, na Poland. Mara nyingi nilijipata katika hali ngumu sana. Nilifuatwa mara nying na makachero. Nyakati zingine walinisumbua na kudadisi mambo yangu. Kila mara niliona nguvu za Mungu. Alifanya miujiza kwa kujibu maombi. Mungu alinilinda na kunipitisha katika mipaka ya wakomunisti! Rafiki zangu wengi “walisimama pengoni” kwa niaba yangu. Maombi yao yalifungua njia pana kwangu. Katika huduma ya maombezi, Mungu huheshimu maombi ya waumini waliojazwa na roho. Mkristo anapojiachilia kwa Kristo na kudumu ndani yake, ndipo maombi yake yanaweza kubadili na kuleta tofauti katika ulimwengu wake. Anaweza kumhusisha Mungu katika vita kwa nguvu zinazotokana na maombezi yake. Natamani Mungu akuite katika huduma hii ya maombezi. Unaweza kuwa na huduma ya kipekee ya maombi ambayo inaweza kubadili ulimwengu wako. Maombi yako yanaweza kuleta totauti. Tukiungana pamoja katika maombi, tutaweza “kutia sukari katika ulimwengu huu”, hadi Kristo atakaporudi. Michango 1. S.D. Gordon, Quiet Talks on Prayer (Grand Rapids, Michigan: Baker book House, 1980),pp.13,14 2. Ibid.,p43 3. Elizabeth Elliot, Through the Gates of Splendor (Wheaton, Illinois: Tyndale House Publishers, 1981). 4. Doris M. Rucoe, The Intercession of Rees Howells (Fort Washington, Pnnyslvania: Christian Literature Crusade, 1983), p.9. 5. Francis McGaw, Praying Hyde (Minneapolis, Minnesota: Bethany Fellowship, 1970), p.9.108109



KUFUNGA NI NINI? INAHUSIANA VIPI NA MAOMBI?


 Je” Tunawezaje kurudia nguvu za mitume na huku tunapuuza kufuata desturi ya mitume? Tunawezaje kutarajia nguvu itiririke kama hatujatayarisha njia? Kufunga ni njia ambayo imechaguliwa na Mungu ya kuwezesha neema na nguvu zake ziweze kutiririka. --Arther Wallis, God’s Chosen Fast. Je, kufunga ina mahali maalumu katika maisha ya Mkristo wa kisasa katika karne ya ishirini? Dhana yangu ni kwamba asili mia tisini na tano ya Wakristo hawajawahi kushuhudia masaa ishirini na manne ya kufunga kulingana na Biblia. Waumini wachache wanaelewa vyema maana ya maombi na kufunga. Kufunga Ni Nini? Tusidhani kwamba kila mtu anaelewa maana ya kufunga. Wengine wanafikiri kufunga ni kutokula, wengine wanafikiri kufunga ni tendo la kale la kidini ambalo halina nafasi katika kanisa la kisasa. Tunamaanisha nini tunapowasihi watu “wafunge na kusali” (Mathayo 17:21)? Katika Agano la Kale, neno hili kwa Kiebrania linamaanisha “kufunga kinywa”, katika Agano Jipya, neno hilo kwa Kiyunani linamaanisha ‘kutokula’, ama kujiepusha na kula. Hata hivyo, kufunga ni zaidi ya kutokula kwa muda fulani. Mafundisho ya Bibilia kuhusu maombi na kufunga hayakutiliwa maanani katika makanisa niliyoshiriki nilipokuwa kijana. Sikumbuki jambo hili likifunndishwa, au likifanywa miongoni mwa wakristo niliowajua. Mtu wa kwanza niliyempata akiwa mzoefu wa kufunga alikuwa si mtu wa kawaida. Kufungwa Msalabani Mnamo mwaka wa 1969, nilipata fursa ya kuwa mchungaji wa First Baptist Church, Beverly Hills, California. Kulikuwa na mtindo wa “hippie” katika nyakati hizo. Vijana wengi waasi walikutanika huko Sunset strip magharibi mwa Hollywood, California kwa shughuli zao zilizoongozwa na misisimko. Kanisa langu ndogo halikuwa mbali na mahali hapo. Ilikuwa hapo mtaani, nilipokuwa nikishuhudia hawa vijana ambao walikuwa wamepoteza mwelekeo, ambapo nilikutana na Reverend Arthur Blessitt kwa mara ya kwanza. Arthur alikuwa na mkahawa ambapo alikuwa na huduma ya kuwapa watu kahawa. Maisha yake na pia huduma yake iliwagusa maelfu ya watu na kuwaelekeza kwa Mungu. Mwenye nyumba ambapo Arthur aliweka mkahawa alikataa kuendelea kumkodisha nyumba hiyo, akidai aondoke hapo pamoja na wakristo aliokuwa nao na kuihama Sunset Strip. Wakristo ambao walikuwa na ushuhuda wa Yesu Kristo walikuwa pingamizi kwa biashara zilizohusika na ukahaba, madawa za kulevya, vyumba vya ushoga, na anasa ambazo zinaambatana na usherati. Wenye majumba hayo ya anasa waliungana na kuagana kwamba hakuna mmoja wao atakayekodisha Arthur nyumba kwa huduma yake ya kahawa. Kwa kususia kufukuzwa kwake kutoka kwa jumba lake la kahawa, Arthur alijifunga kwa msalaba wa kimo cha futi nane na kuketi kando ya njia nje ya jumba maarufu la starehe kwa vijana, liitwalo “The Whiskey A Go – Go.” Alijiegemeza kwa boriti ya simu iliyokuwa imefungiwa nyororo, na kufunga mkono wake kwa upande mwingine wa hiyo nyororo. Alishuhudia, akasali, na kufunga kwa muda wa siku ishirini na nane. Hakula chochote ila kunywa maji tu, au maji ya sharbeti. Nilipomwona nilidhani kwamba amerukwa na akili. Kwa majuma hayo manne ulimwengu wote ulimtazama Arthur. Alichoshwa sana na jua kali la California. Hata hivyo Mungu alikuwa naye. Huko kuteseka kulileta matokeo mema. Mamia ya watu waliokoka kwa kuja kumtazama mwenye “vioja vya Yesu.” Wakristo walijiunga naye katika mgomo wake na kumtia moyo. Mungu alitukuzwa na maisha ya watu yakabadilishwa. Nilikuwa mmoja wa wale waliobadilishwa.110 Ujuzi wa Arthur ulinifanya nisome Biblia ili niweze kuelewa yale Mungu alisema kuhusu kufunga. Uvumbuzi wangu ulinishangaza! Nilishangazwa kwamba nilikuwa nimeyapuuza mafundisho haya maalum kuhusu kufunga. Mtu hawezi kuishi maisha ya maombi na maombezi bila kuwa na huduma ya kufunga. Ukitafuta maneno “funga” ama “kufunga” katika itifaki yoyote ya Bibilia, utashangazwa vile Mungu amehusisha itikadi hii ya jadi kuwa jambo la kawaida katika maisha ya Mkristo mtiifu. Nataka kushiriki pamoja nawe uvumbuzi wangu kuhusu kufunga na kusali. Aina Mbili Za Kufunga Kuna jinsi mbili za kufunga, yaani kufunga kidunia, na kufunga kiroho. 1. Kufunga Kidunia Kuna namna mbili katika kufunga kidunia. Inaweza kumaanisha kutokula ili kupunguza uzito kwa sababu za kiafya. Madaktari wanaojua manufaa yanayotokana na kufunga huwaagiza wagonjwa wafunge kwa muda fulani. Inaweza kuwa kufunga kula aina fulani za chakula kwa sababu za kiafya. Watu wengine hudhani kimakosa kwamba kufunga ni kujiua kwa njaa. Wanaona kwamba ni mbaya kiafya na basi inastahili kuepukwa. Labda hilo ni wazo lililo sawa na kweli. Aina zingine za kufunga zina manufaa sana kiafya. Kufunga kunasaidia katika kusafisha mwili na kutoa taka na uchafu wowote. Tumbo na matumbo yakiwa wazi, mwili huanza kujilisha kwanza kwa kutoa vitu visivyohitajika na mwili, kama vile taka, uchafu, mafuta, na mengineo. Kuzoe kufunga kunaweza kuwa na manufaa zaidi kwa mtu yeyote, hasa akiwa chini ya uangalifu wa daktari, ama afisa wa afya. Kufunga kwa masaa ishirini na nne tu, na kunywa maji kunaweza kupunguza ulegevu, kupa mwili wako nguvu, na kukuwezesha kuzingatia mambo ya rohoni. Tutaongea mengi baadaye kuhusu manufaa ya kiroho yanayotokana na kufunga. Aina zingine za kufunga kidunia zinaweza kuwa na namna za kidini, lakini si sawa na kufunga itokanayo na mwomgozo wa Bibilia, ambayo tunaongea juu yake. Kwa makafiri wengi, kufunga kidini ni sehemu muhimu ya kuabudu. Huyu kafiri anaweza kuabudu kwa kufunga ili kutesa mwili wake ili akubalike na mungu wake. Kitendo hiki cha kuabudu kinaweza kuhusu kujijeruhi kutumia misumari, pini na vifaa vingine. Huku si kufunga kulingana na Bibilia. Mwili si kitu kiovu ambacho kinastahili kuadhibiwa. III. Kufunga Kiroho. Neno la Mungu linatupa sababu za kiroho katika kufunga. Tunakosa kula au kunywa kwa sababu tunatafuta kuwa na ushirika zaidi na Mungu. Kufunga, kama vile maandiko yaelezavyo, si kufunga kula ili kupunguza uzito, ama kuadhibu mwili. Ikiwa Mkristo ana uzito wa kupindukia, basi kufunga kunaweza kuwa mwito kutoka kwa Mungu ili awekwe huru kutokana na utumwa wa tamaa za mwili. Kufunga kulingana na Biblia kuna manufaa za kiroho, wala si za kimwili ama za kidunia. Mbona Tufunge? Wakristo wengi wamehudhuria kanisa kwa miaka mingi na kuishi maisha ambayo yanadhaniwa kuwa ya Mkristo wa kawaida, lakini hawajaweka agano na Mungu katika kufunga. Swali la kawaida ni “kwa nini nifunge?”. Hebu nikueleze manufaa ya kufunga (kuacha kula) mara kwa mara kwa kila muumini. Tumesikia mara nyingi msemo usemao kwamba njia ya kuelekea katika moyo wa mtu ni kupitia kwa tumbo lake. Msemo huu ni kweli kuliko tunavyodhania. Milango yetu ya maarifa, yaani kuona kwa macho, kusikia, kunusa, kuonja na kugusa, ni za kuelekea moyoni. Shetani anaelewa hayo kuliko tujuavyo. Katika Biblia tunaona shetani akiingia katika roho ya binadamu kupitia kwa tumbo lake. Aliweza kufikia Awa, kule shambani la Edeni kupitia kwa hamu yake ya chakula. Kitabu cha mwanzo kinasimulia kwamba aliona tunda hilo likiwa nzuri. Watu hawa wawili wa kwanza waliangushwa na hisia zao. Mwili ni mlango wa moyo.111 Shetani alitumia njia hii pia kumfikia Nuhu baada ya gharika. Katika kitabu cha mwanzo sura ya 9 tunaona Nuhu akilewa mvinyo kutoka kwa shamba lake la mizabibu, na wana wake wakimwona akiwa uchi. Hii inaonyesha kwamba dhambi ya tamaa ya mwili ilimshinda Nuhu. Kumbuka wana wa Isaka, yaani Esau na Yakobo. Esau aliuza uridhi wake kwa sababu ya bakuli ya supu! Shetani anatumia tamaa za mwili kufikia moyo na roho ya mwanadamu. Je, hii ina uhusiano gani na kufunga? Biblia inatufundisha kwamba Mungu ndiye chanzo cha tamaa za mwili, na kwa hivyo taamaa hizo hazina uovu. Kutumia vibaya, au kutesa mwili ndio dhambi. Ni lazima tumiliki na kutia miili yetu nidhamu kutokana na tamaa za mwili. Lazima miili yetu iwe chini ya mamlaka yetu, na kuwa mtumwa wetu ili Roho aweze kuutawala. Tusiiruhusu mwili itutawale. Jangwani Imeandikwa katika kitabu cha Mathayo sura ya nne kwamba Yesu alifunga siku arobaini, mchana na usiku. Kwa siku arobaini hakula chochote. Baada ya kipindi hiki, Bibilia inasema “mwisho akaona njaa” Shetani akaja kumjaribu Mungu wetu. Ni ombi gani ambalo shetani aliomba kwanza? Huyu adui alimjaribu Yesu kwa kumwambia aamuru mawe kuwa mkate, kuonyesha kwamba mwili wake ulihitaji chakula. Hata hivyo, kufunga kwake Yesu kulimfanya kuwa “shupavu” katika roho. Alifanya mwili wake kuwa mtumwa wake. Mwokozi wetu alikuwa na njaa, lakini njia ya kuingia rohoni mwake haikuwa kupitia tumboni mwake. Kuna uhusiano kati ya tamaa za mwili wa mwanadamu, na maisha yake ya rohoni. Adabu mwilini huenda sambamba na mtu wa rohoni (hii si kweli kila wakati). Kufunga “hukwamua” uzito ambao tamaa zetu za mwili zimeweka katika nia zetu. Kufunga kuna manufaa kama vile maadiko yanavyofundisha. Mbona itikadi hii inazingatiwa na wakristo wachache tu? Labda uko kama rafiki yangu mmoja mhubiri mnene aliyesema kwa ujeuri, “hainihusu mimi!” Basi, mbona siye? Sababu Zinazofanya Watu Kukosa Kufunga Hebu kwa kifupi nieleze sababu zinazofanya watu wapuuze kufunga. Usheria Watu huogopa kwamba kufunga kunaweza kufanyika kuwa tamaduni au kanuni za dini ambazo ni sharti zifuatwe. Wanaona ni kama kuwa chini ya sheria, badala ya kuwa chini ya neema. Watu wengi huogopa hali hiyo ya utumwa. Je, mbona tunahisia hizo kuhusu kufunga. Kwa nini hatuhisi hivyo kuhusu sala, kushuhudia, au fungu la kumi? Jambo lolote katika ukristo unaweza kuwa sheria, au sivyo?. Kutoa fungu la kumi linaweza kuwa sheria, lakini sisi wainjilisti kwa hakika hatujadharau mafundisho yanayohusu kutoa fungu la kumi. Utawa Jambo la pili ni kwamba, kufunga kumepuuzwa kwa sababu watu wameogopa utawa. Mnamo zamani za kati (middle ages), kanisa la kirumi la kikatoliki lilianza kutilia maanani mambo ya utawa, maisha ya desturi yakujitenga na mambo ya dunia ili kujifunza mambo ya kidini (monastic life), na kuishi mbali na jamii ili kuzuia uigizaji wa tabia fulani. Kuishi kwa namna hiyo kulifanya kufunga kuwa sehemu muhimu katika maisha ya utawa. Kwa hakika utawa ni nini hasa? Kwa kawaida, mtawa ni mtu atiaye mwili wake uchungu, na kuupigapiga kwa nguvu. Lengo lake ni kushinda, kutesa, na kuadhibu mwili kwa sababu za kiroho. Dini nyingi za kikafiri zina utawa. Mara kwa mara tunasoma kuhusu watu wanaojidunga na visumari mwilini na kufunga, ama wanakufa njaa ili waweze kufurahisha miungu yao. Labda wakristo wengi wa kisasa wameasi dhidi ya aina hii ya wazimu wa kidini. Lakini Bibilia imeeleza wazi wazi kwamba kufunga si utawa. Ungwana Wahubiri na waalimu wengi wanafundisha kwamba kufunga hakuna maana kwetu siku hizi. Hii imesababisha watu kudharau kufunga. Wengine husema kwamba, kufunga ilikuwa na maana tu kwa Wayuda wa kale, wala hayahusu wakristo wa enzi hizi. Watakatifu wote wakuu wa Mungu walifunga wakisali, wakishuhudia, na kuhubiri.112 Waombezi wa Agano la Kale Musa , mwadhama katika agano la kale, ndiye mfano mzuri kwetu katika kutambua uhusiano kati ya sala, maombezi na kufunga. Musa ndiye pia mfano mzuri wa mwombezi aliyetumia kufunga kama njia ya kuleta mawasiliano mazuri katika roho. Musa alifunga kwa siku arobaini mara mbili bila chakula wala maji. Kufunga hakuwezekani kwa nguvu za mwili, ila kwa nguvu za ajabu. Musa alikaa siku themanini bila maji wala chakula, hali mtu atakufa asipokunywa maji baada ya siku kama kumi na tano hivi. Tendo la Musa lilikuwa la kimiujiza. Eliya alifunga kwa muda wa siku arobaini. Malkia Esta alifunga kwa muda wa siku tatu, mchana na usiku akimlilia Mungu aweze kuwaepusha Wayahudi na amri ya Mfalme. Watakatifu wote katika Bibilia, wakiwemo Daudi, Nehemia, Ezra, Yeremia na Isaya walikuwa wanaume na wanawake waliokuwa na uzoefu wa kufunga, kusali na uombezi. Mafundisho ya Yesu kuhusu Kufunga Katika mafundisho ya Yesu mlimani, alieleza mambo muhimu kuhusu kufunga. Katika kitabu cha Mathayo sura ya sita, Yesu alifundisha vitu vitatu vya maana katika dini, yaani sadaka na zaka, sala, na kufunga. Aliongea pia kuhusu utumizi mbaya wa vitu hivyo vitatu. Katika Mathayo sura ya sita haya ya pili hadi ya nne, Yesu aliongea kuhusu utoaji wa zaka, fedha na kutoa vipawa kwa maskini. “Basi utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani ili watukuzwe na watu. Amini, nawaambieni wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kishoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri na baba yako aonaye sirini atakujazia.” Yesu anatufundisha vivyo hivyo kuhusu utoaji. Anasema “utoapo.” Ukristo ni kutoa, au sivyo? Yesu hakusema “kama ukitoa” akidhani kwamba tutatoa ili tuwape masikini. Anasema, ‘utoapo’, halafu anaeleza unavyopaswa kutoa. Anasema usijisifu, wala kutoa hadharani, ila kwa siri bila kujali utukufu utakayopata kutokana na kutoa kwako. Halafu, katika Mathayo 6:5-15 akaeleza kuhusua sala. Maombi ni huduma ambayo tumepewa na Mungu. Hebu tumsifu Bwana kwa huduma ya maombi. Lakini maombi inaweza kutumiwa vibaya. Yesu anaongea kuhusu utumizi mbaya wa maombi. Anatoa mfano wa maombi tuliopewa katika mwanzo wa haya ya tisa. Anasema unaposali, sali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni … ’’ Kisha anaeleza jinsi unavyoweza kuomba. Katika aya ya 15 anatueleza kuhusu kuomba na kusamehe wengine, ndipo nasi tupate msamaha kutoka kwa Baba yetu. Yesu alidhani kwamba wakristo watasali, ndipo hakusema kama mkiomba, bali “mwombapo.” Jambo la tatu la kidini aliloongea juu yake linapatikana katika aya ya kwanza hadi ya kumi na nane, ambalo ni jukumu la kufunga!. “Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amini,nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazia” (Mathayo 6:5-6). Hii ina umuhimu gani? Yesu alisema, “utoapo”, “uombapo”, na “afungapo.” Swali si kama unastahili kufunga, bali ni ufungapo. Tunaweza kuona kwamba Yesu alieweka kufunga katika kiwango sawa na maombi na utoaji.113 Ni wazi kwamba mkristo anahitajika kutoa na kuomba. Basi, mbona tunaleta maswali kuhusu kufunga? Mbona tunautupilia mbali? Yesu alisema, “unapofunga” wala si “kama ukifunga.” Alidhani kwamba kila muumini atafanya kufunga kuwa sehemu muhimu katika huduma na maisha yake ya kikristo. Yesu alidhani tutafanya jambo ambalo wengi wetu hatufanyi! Watu wengine wamesema, “Naam, je yale mafundisho ya Yesu mlimani yalikuwa ya watu wote siku zote?” Wengine pia wamesema kwamba hatuwezi kuzingatia mafundisho hayo kwa sababu yalihusu wale waliokuwepo kabla Pentekote, na kwa hivyo yalihusika na sheria kwa nyakati za kale. Wanaendelea kusema kwamba mafundisho hayo yalikusudiwa Wayahudi, na kwa hivyo yanahusu waumini wa kiyahudi tu. Kwa hivyo wanasema kwamba haya maandishi kuhusu kufunga hayahusu wakati huu. Mimi sikubaliani na maelezo hayo kwa sababu naamini kwamba haya mafundisho ni ya kila wakati. Inahusu kila muumini wa kweli wa Kristo. Hata hivyo, Yesu alitufundisha mahali pengine kuhusu kufunga katika maisha ya kanisa. Mathayo 9:14, inasema hivi, “Wakati ule wanafunzi wake Yohana wakamwendea, wakasema, Kwa nini sisi na mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi?” Mafarisayo walikuwa wakifunga mara mbili kwa juma. Hawakuamrishwa na Mungu kufunga mara mbili kwa juma. Katika neno la Mungu kuna amri moja tu kuhusu kufunga, nayo ilihusiana na Siku ya Tambiko (Day of Atonement), iliyoitwa ‘Yom Kippur’. Ni siku hiyo tu ambapo Mungu aliamuru saumu. Lakini Wafarisayo walizingatia sheria sana hadi wakaamua kufunga mara mbili kwa juma, na kutilia najisi agizo la Bibilia kuhusu kufunga. Wafuasi wa Yohana Mbatizaji walifunga. Wafuasi wa Yesu hawakufunga maana Yesu hakuwa amewafundisha kufunga. Kwa hivyo wafuasi wa Yohana walichanganyikiwa. Kwa nini wanafunzi wa Yesu hawakuwa wakifunga? Yesu, alipoona kuchanganyikiwa kwao, aliwaeleza, akisema, “Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda Bwana arusi akiwapo pamoja noa? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi: ndipo watakapofunga” (Mathayo 9:15). Hakukuwa na haja ya wanafunzi wa Yesu kuomboleza na kufanya saumu alipokuwa pamoja nao. Bwana arusi alikuwa bado yu pamoja na wale walioalikwa arusini. Sherehe zilikuwa bado zikiendelea. Haukuwa wakati wa huzuni, bali furaha. Haukuwa wakati wa kufunga, bali kusherehekea. Wazo la kuomboleza lilihusishwa na kumtafuta Mungu. Hawakuwa na sababu ya kumtafuta Mungu, kwani alikuwa nao, na kwa hivyo walihitaji kufurahi, kusherehekea, kujifundisha na kukua. Yesu alikuwa akisema, “niko nao; ni wakati wa furaha. Watakuwa na wakati wa kutosha wa kufunga baada ya kuondoka kwangu. Watafunga; kisha watanitafuta mimi.” Bwana arusi hayuko leo, kwani alienda. Hatarudi hadi wakati wake wa kurudi mara ya pili uwadie, atakaporejea kumchukua bibi yake, ambaye ni kanisa lake. Yesu anasema kanisa litafunga kati ya wakati wa kwenda kwake na kurudi kwake. Haya ni mafundisho yaliyo wazi kuhusu kufunga kutoka kwa Yesu, inayolingana na Bibilia. Kwa sababu Bwana arusi ameenda, kanisa la kwanza lilikuwa na mazoea ya kuomba, wakiambatanisha na kufunga. Baada ya kukutana na Yesu katika barabara ya kuelekea Dameski, Sauli wa Torso alikaa kwa siku tatu akiwa amefunga kabisa bila kula chakula wala kunywa maji. Kornelio, katika kitabu cha Matendo ya Mitume sura 10, alifunga na kumngojea Petero kwa kutii ono aliloona. Katika Matendo 13:2-3 kanisa la Antiokia lilifunga na kuomba, “Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.” Kutumwa kwa Paulo na Baarnaba kama wamisheni wa kwanza kulitanguliwa na kipindi cha kusali na kufunga. (Matendo 14:23; “Na walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila kanisa, na kuomba pamoja na kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini.”) Walianzisha makanisa mijini katika huduma yao ya kuhubiri injili katika bara Asia. Walipokuwa wakiondoka waliteua wazee wa kuendeleza kanisa. Je wangetambuaje wazee wa kuacha kwa huduma hiyo, isipokuwa tu kwa kumtafuta Bwana kwa kuomba na kufunga?114 Aina tofauti Za Kufunga Aina nne za kufunga zimeelezwa katika Biblia. I. Kufunga kwa kiwango Danieli 10;3 inaeleza kuhusu kufunga kwa kiwango. “Sikula chakula kitamu wala nyama wala divai haikuingia kinyani mwangu” Katika kufunga kwake, Danieli alikula tu mboga. Kufunga kwa kiwango ni kujiepusha na kula vitu vitamu, kama vile kitumba (cake), na vinginevyo. Kwa hivyo, kama umefunga kwa kiwango kwa sababu za kiroho, unaweza tu kula mlo moja kwa siku, ama ukose kula aina fulani ya vyakula, isipokuwa mboga tu, jinsi Danieli alivyofanya. Kufunga kwa kiwango ni kula chakula kidogo kwa kujizuia . Unaweza tu kufanya hivyo kama Mungu amekuita kufanya hivyo. II. Aina Maarufu ya kufunga Sehemu hii ni ya kile tutakachokiita “aina maarufu ya kufunga” kwa sababu hii ndio inayojulikana sana katika Bibilia. Kwa sababu hiyo, wengine wameiita kufunga kwa kawaida. Kufunga huku kunahusu kutokula chakula chochote ila kunywa maji tu, au maji ya sharubati. Yesu alifunga hivyo usiku na mchana kwa siku arobaini alipokuwa jangwani, katika Mathayo sura 4. Bibilia inasema kwa siku arobaini, mchana na usiku, aliona njaa. Je, watambua kwamba Bibilia haisemi aliona kiu pia? Pia Shetani akamjaribu akimwambia ageuze jiwe kuwa mkate, wala hakumjaribu na kiu. Kunaweza kuwa na hoja kuhusu jambo hili, lakini nadhani kwamba Yesu alifunga kawaida, na kwamba alikuwa na maji kwa siku hizo arobaini. Kama hakuwa na maji, basi alikuwa na msaada wa ajabu ya kumwezesha kuishi kutoka kwa Mungu. III. Kufunga Halisi Musa alifunga halisi. Aliyefunga halisi hali chakula au kunywa maji kwa muda fulani aliyoutenga. Musa angekufa kama Mungu hangeliingilia kati. Ni nguvu za kipekee ndizo zinazoweza kumfanya mtu kufanya Musa alivyofanya. Musa ndiye aliyefunga kwa muda mrefu sana katika Bibilia. Alifuatisha siku 40 za kufunga mara mbili, yaani siku 80, bila kula chakula au kunywa maji. Kuna matukio mengi katika Biblia yanayoonyesha kwamba watu walifunga halisi kwa siku tatu. Labda siku tatu ndizo zinafaa kwa kufunga. Paulo alifunga kwa siku tatu bila kula chakula au kunywa maji kabla kubatizwa kwake. (Matendo ya Mitume 9:9). Ezra alimtafuta Bwana kwa kutangaza kwamba wana wa Israeli wafunge. Walifunga kwa siku tatu kando ya mto Ahava mchana na usiku. Ezra sura ya 8 inaeleza hivi, “Basi tukafunga, tukamsihi Mungu wetu kwa ajili ya hayo; naye akatutakabali” (Ezra 8:23). Katika kitabu cha Esta 4:16, Esta aliwaita watu wake Wayahudi waombe na kufunga, au waangamizwe. Walifunga kamili, bila chakula wala kunywa maji kwa siku tatu. Esta, pamoja na wanawali wake pia waliomba na kufunga. IV. Kufunga kwa Kirefu Kufung kwa siku zinazozidi tatu imetajwa katika Bibilia. Siku nyingi sana ambazo zimetajwa katika Bibilia ni kama siku 15, 20 au hata 40. Sijawahi kufunga kwa muda wa siku zaidi ya tano, lakini najua rafiki zangu wengi ambao wamefunga kwa siku 20. Nilimtazama Arthur Blessit, pale Sunset Strip akifunga kwa muda wa siku 28, na kunywa tu maji ya sharubati. Baadaye alifunga kwa siku 40, akiwa Washington, D.C. Huu ndio mfano wa kufunga kwa muda mrefu, ambapo mtu hunywa maji peke yake. Wanaofunga Je kufunga ni kwa watu ambao hawaeleweki au wale ambao hawakubaliki katika kanisa? Je kuna nafasi ya kufunga katika maisha ya kila Mkristo? Je, Mkristo yeyote anaweza kufunga? Kwa hakika maishani115 mwangu nina nafasi ya kufunga. Hata hivyo, Mungu hakuamuru kanisa kufunga kwa nyakati hizi. Yeye hutuita kwa huduma ya kuomba na maombezi. Mara nyingi huduma hii itahitaji kufunga ili kuwezesha roho zetu kupata nidhamu ili tuweze kukabiliana na vita vilivyoko. Katika kitabu cha Mambo ya Nyakati wa Pili 7:14 tunaona hitaji la kuomba na kuomboleza kwa taifa letu lililojawa na dhambi, ingawa kufunga hakujatajwa, “ikiwa watu wangu walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha.” Hebu tilia mkazo neno “watajinyenyekeza.” Hakuna kiwezacho kumnyenyekeza mtu kama vile kufunga. Unaweza kuhisi hitaji kuu la kuombea mtu fulani, au mwito wa Mungu kwa kusudi fulani, au hitaji fulani, ama kutenga nyakati bila kula wala kunywa. Utafanya hivyo kwa sababu za kiroho kwa muda wa masaa ishirini na nne, ama kwa wakati fulani ambao Mungu amekuelekeza. Sababu Za Kufunga Hebu tuangalie sababu za kufunga kiroho. Je, kuna faida gani za kiroho katika kufunga? Kufunga ili kumtafuta Mungu Katika Biblia, lengo la kufunga huwa ni la kiroho. Kufunga kulingana na neno la Mungu huwa kwa ajili ya kumtafuta Bwana. Mungu anaponielekeza kufunga huwa ana sababu fulani, na sina mng’ang’ano katika kufanya hivyo. Sijawahi kuona njaa, au kuwa na tatizo kutokana na huko kufunga. Mara nyingine nimefunga kwa siku tano, bila kuwa na tatizo. Hata hivyo, nilipoamua kufunga bila kuelekezwa na Mungu kufanya hivyo, basi ikawa tu kama kujinyima chakula ili kupunguza uzito! Sifikirii jambo lolote ila chakula tu. Ni heri Mungu anipe mwito wa kufunga kwa siku arobaini kuliko kujinyima chakula kwa kusudi la kupunguza uzito. Bila kuitwa, nitafiki tu chakula mchana wote. Nia ya Mungu katika kukuita kufunga ni ya kiroho, ambayo ina baraka kwako. Hii Ndio maana Bibilia inaeleza kuhusu saumu ambayo Mungu atauchagua, (tazama Isaiah 58). Unapaswa kufunga Mungu anapokuelekeza kufanya hivyo. Hivyo utaongozwa na roho katika kufunga. Kufunga kwa kujuta dhambi Kwanza, kuna kufunga kwa kuonyesha huzuni sababu ya dhambi. Kufunga kunaweza kuwa kifaa cha kutuongoza kutubu, kunyenyekea, au kumtafuta Mungu. Kuna nguvu za ajabu katika kufunga iwezayo kufanya roho zetu kunyenyekea. Inasaidia katika kuweka roho nidhamu. Pia inaweza kutuongoza kutubu na kumtafuta Bwana. Katika Zaburi 35:13, Daudi alisema, “Nalijitesa nafsi yangu kwa kufunga.” Tena Daudi alisema, “Nilipolia na kuadhibu roho yangu kwa kufunga” (Zaburi 69:10). Ezra anawaambia watu kwamba wataamuru saumu kando ya mto Ahava ili wapate kuzinyenyekesha nafsi zao mbele za Bwana (Ezra 8:21). Kufunga ili kunyenyekesha roho Karibu watumishi wote wa Mungu walioteuliwa walizoea kufunga ili kunyenyekesha roho zao. Shujaa wangu mmoja katika imani ni John Wesley. Katika fundisho lake moja maarufu kuhusu kufunga, alinena: “Kwanza, hebu ifanyike kwa utukufu wa Mungu, macho yetu yakiwa yameelekezwa kwake. Hebu nia yetu iwe moja tu, yaani kwa utukufu wa Baba aliye Mbinguni, kuonyesha huzuni na aibu yetu kwa sababu ya kwenda kinyume cha kanuni yake takatifu, na kungojea ongezeko la neema yake inayotakasa, tukivutiwa na mambo yaliyo juu; na kutia juhudi na kujitolea katika maombi; ili tuepuke ghadhabu ya Mungu; na kupata ahadi za ajabu na za thamani ambazo ametuahidi katika Yesu… Tutahadhari tusije tukajitwalia lililo la Mungu katika kufunga kwetu.”116 Mungu anatuita tufunge ili atunyenyekeshe, na ili tutafute uso wake ulio takatifu. Tunafunga kwa ajili yake, na kwa ajili yetu. Fikira yoyote ya chakula iwe ni mwito wa kusali na kumtafuta Mungu. Kufunga kunatuonyesha kudhoofika kwa maisha yetu. Tu viumbe vya kutegemea, ambao wanalazimika kuwa na mkate wa kila siku ili kuishi. Kufunga kunanyenyekesha nafsi. Inatukumbusha kwamba tu mavumbi na Mungu ndiye asili yetu. Kufunga kunaweza kuvunja minyororo ya mambo ya mwili na kuweka huru roho ili iweze kupaa na Mungu. Kufunga kunaweza kutuondolea kiburi. Inapendeza jinsi Bibilia inasimulia mara nyingi kwamba walizini “tumbo zao zilipokuwa zimejaa.” Bibilia inasema watu wa sodoma walilisha tumbo zao kwa vyakula na vinywaji, kisha wakaenda kufanya usherati. Walijawa na kiburi rohoni. Ni jambo la kushangaza kwamba watu walio wanene kwa kutokuwa na kiasi mara nyingi huwa watu wenye kiburu, wanaojihusisha na mambo mengine yanayoambatana na kutokuwa na kiasi. Katika Biblia, kufunga huleta hali ya kufanya mtu kunyenyekea. Pia hufanya roho yenye kiburi kuwa na majuto mbele za Mungu, na kuweka nafsi huru kumtafuta Bwana. Katika kufunga mwili hutiwa adabu na kufanywa tiifu. Kufunga pia kunaweza kuonyesha hali ya kuwa na majonzi . Katika Mathayo 5:4, Yesu alinena jinsi walio na huzuni wana heri kwa sababu watafarijika. Katika Mathayo 9:15 Yesu anatumia kwa usawa maneno kuomboleza na kufunga. Kuomboleza na kufunga ni maneno yanayotumika sawa. Kwa hivyo kufunga ina maana ya kunyenyekesha roho mbele za Mungu. Kufunga ili kufanywa takatifu Je umewahi kufikia wakati fulani katika maisha yako ambapo ulitamani kumwona Mungu? Ulikuwa na shauku ya kutembea karibu sana na Mungu, kumjua zaidi, na kuelewa neno lake zaidi. Je, ulifahamu kwamba katika Bibilia kufunga kumeambatanishwa na kumtafuta Mungu, kufanywa wakfu, na kujitenga kwa ajili ya Mungu? Je, unadhani Yesu alikaa jangwani siku arobaini kwa nini? Alifanya hivyo kabla kuanza huduma yake kwa watu. Yesu alifunga ili autafute uso wa Bwana katika maisha yake, na katika huduma yake. Mkristo mara kwa mara hushurutiswa kufunga kabla kupewa mwito, au kazi muhimu, ama kujazwa na roho mtakatifu. Katika matendo 13, tunaona Paulo na Barnaba wakitumwa kama wamisheni. Walimtafuta Bwana kwa kufanywa watakatifu, na pia kwa ajili ya huduma zao. Kanisa liliomba na kufunga, kisha likawawekea mikono Paulo na Barnaba na kuwatuma wakiwa wakfu kwa Kristo. Kufunga pia kunaweza kuambatanishwa na kutafuta ufunuo kutoka kwa Mungu. Unaweza kuwa unatafuta mapenzi ya Mungu kuhusu jambo fulani, lakini hujui Mungu angehitaji ufanye vipi. Bibilia inatuonyesha kwamba kujipeana mhanga kwa Mungu - yaani kwa roho, nafsi na mwili - na kuweka kila wazo mateka kwa Mungu, kunawezekana kwa njia ya kuomba na kufunga. Tunahitaji kumfungia Bwana peke yake, wala si mtu mwingine. Katika matendo 13:2 tunaona kwamba kanisa lilifunga kwa ajili ya Bwana. Kama Wakristo tunajiuliza “Mbona nifanya saumu,” au “nitafaidika vipi kwa kufanya saumu?” Tunamfanyia Bwana saumu. Nabii Ana katika Luka 2 aliabudu kwa kufunga. Katika kuabudu na kufunga, unamtafuta Mungu kwa nafsi yako yote. Kufunga kwa kujali Katika Bibilia, kufunga kulihusisha kuombea wengine. Hebu tuongee kuhusu kuomba na kufunga. Kufunga peke yake hakumaanishi kitu. Bibilia inaonyesha kufunga kama kitendo kinachoambatana na kusudi, na lengo fulani. Bibilia inaongea kuhusu kuomba na kufunga, kukesha na kufunga, kuabudu na kufunga, na kutafuta Bwana na kufunga. Kufunga huambatana na kitu kingine. Inaambatanishwa na maombi kwa sababu inalete hali ya117 kuomba, kusoma neno la Mungu, na kumtafuta Bwana. Inafanya nafsi kuwa huru kumtafuta Mungu. Utafiti wa kisayansi umegundua kwamba watu wanaofunga ni makini, na wenye macho ya kung’aa. Utaona kwamba u makini sana wakati wa kufunga kuliko nyakati zingine. Mwili wako unapotakaswa, roho yako inakuwa huru kuelewa mambo ya roho unapofunga na kuomba. Kuomba na kufunga kumeniwezesha kufahamu mambo makuu kutoka katika neno la Mungu. Nimeona neno la Mungu likiwa hai kwangu kutokana na kuomba na kufunga. Ushirika wangu na Mungu pia umeimarika sana wakati wa kuomba na kufunga kuliko nyakati zingine. Kuomba na kufunga Kufunga huambatana na maombi kwa jinsi hizi tatu. I. Kufunga na maombezi Unaweza kufunga na kuomba ili kuombea wengine. Kitabu cha Esta kinatuonyesha vile Esta alivyowaita watu ili waombee wayahudi ili wasiangamizwe na mfalme. Waliomba na kufunga kwa ajili ya taifa lao. Tunaona hayo pia yakitendeka katika Ezra 8, kama nilivyotaja hapo awali. Tunaona watu wa Mungu wakiomba na kunyenyekesha nafsi zao ili Mungu asiangamize taifa lao. Katika hadithi ya Yona na Nineva, mfalme wa Nineva aliagiza taifa nzima kuomba na kufunga ili Mungu asiliangamize. Katika Bibilia, tunaona kufunga na kuomba zikiambatana pamoja na maombezi. II. Kufunga na uhuisho Mara nyingi nimewasikia watu kanisani na wahubiri wakiongea kuhusu uhuisho. Tunahitaji uhuisho makanisani mwetu. Pia tunahitaji uhuisho katika nchi ya Amerika. Hukuwezi kuwa na uhuisho katika nchi ya America bila maombi. Uhuisho na kufanywa upya katika Bibilia imeshirikishwa na maombi pamoja na kufunga. Nionyeshe kanisa, au mtu aliye na shauku juu ya Mungu, na nitakuonyesha mtu anayemtafuta Mungu kwa dhati hadi kukosa hamu ya chakula! Mungu ataliheshimu kanisa kama hilo, au mtu kama huyo! Kuomba na kufunga inahusiana kikamilifu na uhuisho. Shetani ametupofusha tusiweze kuona njia hii ya ajabu ya kumfikia Mungu. III. Kufunga na ukombozi Watu wengine wanaweza kukombolewa kwa kuomba na kufunga. Bibilia inasema tunaweza kutoa watu wengine utumwani kwa kuomba na kufunga. Huu ni ukombozi wa aina gani? Katika kitabu cha Kumbukumbu La Torati, Musa aliombea wana wa israeli akisema, “Nikaanguka chini mbele za Bwana siku arobaini usiku na mchana, kama pale kwanza; sikula chakula wala kunywa maji; kwa sababu ya makosa yenu yote mliyokosa…”(Kumbukumbu La Torati 9:18). Musa alifunga kwa sababu ya mtu mwingine. Alisimama katikati ya pengo kama mwombezi, akiwa tayari kupoteza uhai wake kwa sababu ya Israeli. Maombezi yake yalikomboa taifa nzima. Tunaweza pia kusimama katikati ya pengo kwa ajili ya walio utumwani. Bila shaka unajua watu walio wagonjwa katika mwili, katika hisia, na hata katika roho. Wanahitaji ukombozi , hasa walio wagonjwa kutokana na dhambi. Mlevi, mwenye kutumia madawa za kulevya, na waliodhulumiwa kiroho kwa sababu ya dhambi wanahitaji kuwekwa huru. Je, hii inawezekanaje? Kuna somo la ajabu kuhusu kuomba na kufunga katika Mathayo 17:1-21. Mtoto wa mtu mmoja alikuwa amepagawa na pepo. Mara kwa mara, alijibwaga motoni, ama kujaribu kujiua alipokamtwa na pepo huyo. Wanafunzi wa Yesu walifahamu kwamba alikuwa amepagawa na pepo. Ibilisi alikuwa akijaribu kumuua. Wanafunzi hao wa Yesu walijaribu kumwondoa huyo118 pepo lakini hawakuwa na uwezo dhidi yake. Baba yake alimwendea Yesu na kumweleza jinsii wanafunzi wake walivyoshindwa kuwafukuza pepo. Yesu aliamuru mtoto aletwe, kisha akaamuru pepo amwache. Mara moja akapata ukombozi. Baadaye wanafunzi walimwendea Yesu faraghani wakamuuliza, wakisema “Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu akawaambia, kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana amini nawaambia, mkiwa na inami kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga” (Matthayo 17:20-21). Yesu anataka tufahamu kwamba mtu yeyote ambaye ni mfungwa wa kiroho wa aina yoyote, anaweza kuwekwa huru. Kinachohitajika ni mtu mwenye imani atakayesimama katika pengo kwa niaba ya huyo mtu. Anayehitajika ni mwombezi atakayefunga na kuomba hadi ushindi upatikane. Mtu mmoja kwa jina Andrew Murray aliponena kuhusu vifungu hivi, alisema kwamba “Imani inahitaji maombi ili iweze kukomaa kamili. Nayo maombi inahitaji kufunga ili iweze kukomaa kamili. Maombi ni mkono unaotuwezesha kushika kisichoonekana; bali kufunga ni mkono huo mwingine unaotuwezesha kufungua na kutupilia mbali kinachoonekana.” Bila shaka Ibilisi atatupinga. Hashindwi upesi. Ni jukumu la kila kanisa “kuteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo,” na kuangusha ngome za Shetani (2 Wakarintho 10:4-5). Mara nyingi kuomba pekee hakutoshi. Kufunga na kuomba huongezea uzito maneno yetu. Ni kutoa maisha yako, na kumwambia Mungu na adui kwamba “siwezi kula hadi ushindi upatikane.” Kufunga ni kuomba bila kutamka kwa kinywa, na inaonyesha uamuzi wa mwombezi. Mtu mmoja kwa jina Arthur Willis, katika kitabu chake kiitwacho Gods Chosen Fast anamnukuu Andrew Murray akisema: “Mbele za Mungu, kufunga kwetu kunaonyesha waziwazi kwamba jambo tunaloliombea ni la kweli na lenye maana sana kwetu. Pia inatilia mkazo juhudi na nguvu zinazopatikana katika maombi, na daima kuwa ishara ya kuonyesha maombi kwa vitendo, bila kutamka kwa kinywa…” Unapofunga Kama vile ambavyo umesoma katika mafundisho haya kuhusu kusali na kufunga, umetambua kuwa kama mfuasi wa Kristo swala kubwa si “iwapo inakupasa kufunga,” bali ni “unapofunga.” Hebu tenga kipindi cha masaa 24, labda kutoka saa sita mchana hadi saa sita mchana siku ya pili. Mwili kwa kawaida huzoea kufunga kwa viwango. Kwa masaa 24, huwezi kuona njaa kwa hakika, ila tu kwa fikira zako. Tumbo lako laweza kunguruma kwa kuzoa kulishwa kwa nyakati fulani. Hebu tumia wakati wa kuwazia chakula kama mwito kwako ili uombe na kumtafuta Mungu. Amua kumfanyia Bwana saumu. Tumia muda huo kujiweka wakfu kwa Bwana. Uwe na azimio katika kufunga. Inaweza kuwa kwa sababu za masikitiko, au kuwekwa wakfu, au maombezi. Funga na kuomba ili uweze kusimama katika pengo kwa niaba ya wengine. Nimewahi kufunga na kuombea nchi fulani, au Mkristo aliye katika huduma fulani katika nchi geni. Je, unaweza kufunga kabisa, au kwa kiwango? Unaweza kuamua kufunga kabisa, yaani bila chakula au maji. Hiyo ni juu yako wewe na Mungu. Labda una woga, au mashaka, ama hata huna hakika kwamba unaweza kufunga. Nakuhakikishia kwamba Baba yako aliye mbinguni anapokuita kufanya saumu, basi atakudumisha, atakukubariki, na kukufurahisha na uwepo wake. Furaha ya Bwana itakuwa nguvu yako.119 Wanaotamani kuwa mashujaa wa maombi wanawajibika “kupenya” hadi palipo takatifu. Kufunga kutakuwa rahisi kama askari anayeweka risasi ndani ya bunduki lake. Ni silaha tunayotumia na kufurahia. Tupe nia ya kufuata hisia zetu, Tupe nguvu za kutenda tujuavyo, Tupe azimio, iliyo na nyuzinyuzi na upindo wa chuma, Tuweze kupiga. --John Drinkwater Misaada 1. John Wesley, ametajwa na Arthur wallis, Gods chosen fast (Fort Washington, Pennsylvania: Christian crusade, inc., 1968), pp.34,35. 2. Andrew murray, With Christ in the School of Prayer (Old Tappan, New Jersey: Fleming H. Revell company, 1965), p.74. 3. Warns, God’s Chosen Fast p. 55 4. Quoted in Warns, p. 84.120121


MSAADA ZAIDI 

Bounds, E M Power through Prayer. Springdale, Pennsylvania: Whitaker House, 1983. - A Treasury Of Prayer. Minneapolis: bethany House, 1981 - Chadwick Samuel. The Path Of Prayer. Fort Washington, Pennsylvania: Christian Literature Crusade,inc., 1963 Gordon, S.D. Quiet Talks On Prayer. Grand Rapids, Michigan: Baker Book House, 1980 Grubb, Norna. Rees Howells, Intercessor. Fort Washingtone, Pennsylvania: Christian Literature Crusade. Inc., 196-1967. Hallesby , o. Prayer. Minneapolis: Augsburg publishing House,1975 Hayford ,Jack. Prayer Is Invading The Impossible . South plain-field, New Jersey: Bridge publishing company, 1977. Huegel, F.J. The Ministry Of Intercession. Minneapolis: Bethany House,1971 Miller, Basil. George Muller: Man Of Faith . Minneapolis: Bethany House,1979 The Kneeling Christian. Grand Rapids, Michigan: Zondervan publishing House,1979 M’Intyer, David M. The Hidden Lift Of Prayer. Grand Rapids, Michigan: Baker Book House, 1979 Morgan , G. Campbell. The Practice Of Prayer Morgan Library). Grand Rapids, Michigan: Baker Book House. Murray,Andrew. Helps To Intercession. Fort Washington, Pennsylvania: Christian Literature Crusade, inc., 1965.175 - The Ministry Of Intercession. Old Tappan, new jersy: Fleming H. Revell company, 1952 - The Power Of The Blood. Fort Washington, Pennsylvania: Christian Literature Crusade, Inc.,1965 - With Christ In The School Pf Prayer. Springdale, Pennsylvania: Whitaker House, 1981. Parker, William R. Prayer Can Change Your Life. New York: Cornerstone, 1974 Prince, Derek. Shaping History Through Prayer And Fasting. Fort Lauderdale, Florida: Derek Prince Ministries Publications, 1973 Rinker , Rosalind. Conversational Prayer. Waco, Texas: Word Books, 1976. - Prayer: Conversing With God. Grand Rapids, Michigan Zondervan Publishing House, 1959 - Sanders, J. Oswald. Effective Prayer. Robesonia, Pennsylvania: OMF Books, 1961 Searle, Walter. David Brainerd’s Personal Testimony. Grand Rpids. Michigan: Baker Book House, 1979 Simpson , A.B. The Lift Of Prayer. Harrisburg ,Pennsylvania: Christian Publications, 1975 Torrey, R.A How To Pray. Chicago: Moody press. Wallis, Arthur. God’s Chosen Fast. Fort Washington, Pennsylvania: Christian Literature Crusade,Inc., 1970.

No comments:

Post a Comment

NENO NI UZIMA Designed by 5gear Copyright © 2014-2015

Theme images by Jason Morrow. Powered by Blogger.