Vichwa vya Habari

JIFUNZE KWA NDEGE TAI

NDEGE TAI JIFUNZE KWAKE
Ninampenda Yesu's photo.

Tai huwa hapambani na nyoka juu ya ardhi. Yeye humnyakuwa na kwenda naye juu sana angani, na hivyo kubadilisha uwanja wa mapambano, halafu humshambulia na kumwachia adondoke chini ardhini. Nyoka huwa hana 'stamina', hana nguvu, wala ‘balance’ akiwa hewani. Huwa mdhaifu, mwepesi kudhurika na asiye na uwezo wa kufanya chochote tofauti na awapo juu ya ardhi ambapo huwa ni hatari, mjanja na mwenye nguvu.
Nawe kama mwana wa Mungu, unapokutana na adui zako na kupigwa vita hamishia mapambano yako katika ulimwengu wa Kiroho ambapo Mungu huchukua nafasi. Usipambane na changamoto zako katika ulimwengu wa kimwili; Jifunze kwa Tai na kubadili uwanja wa mapambano kama yeye. Hapo ndipo utakuwa na uhakika wa ushindi usio wa upinzani. Omba na umwachie Mungu ingilie kati.
Lakini unapopambana katika ulimwengu wa Kiroho kumbuka; kutegemea nguvu za Mungu, sio nguvu zako (2 Wakorintho 10:3) kwa sababu kushinda vita hii hauhitaji nguvu za kimwili, bali akili ya kiroho, kukemea kwa jina la Yesu (Matendo Ya Mitume 19:13-17), kukaa ndani ya Yesu na kujikinga kwa kuvaa silaha zote za Mungu (Yohana 15:7, Warumi 13:12-14 na Waefeso 6:10-18), kupigana vita kwa upanga wa roho ambao ni Neno la Mungu, na mwisho kukumbuka kwamba, unapopigana vita vya kiroho na Shetani na mapepo yake, sio kila dhambi au taabu ni pepo ambalo linahitaji kukemewa.
Ngoja nikupe simulizi moja niliyowahi kusimuliwa na mdogo wangu Loveness Mlay; Kuna siku wanamaombi walikuwa wakimwombea binti mmoja aliyekuwa akipiga kelele kama aliyepagawa na pepo; kwa muda mrefu walimwombea na kukemea lakini mapepo hayo hayakutoka, Mchungaji alipokuja akawanong’oneza kuwa anaona huyo binti hana pepo kwa hiyo watoke nje ya chumba na wamwache pekeyake kwa muda… Baada ya muda kidogo kupita binti akiwa ameachwa pekeyake akaacha kupiga zile kelele kama wafanyavyo wapunga pepo, kukawa kimya; nao walipochungulia wakamuona binti akiangaza macho ili kuona kama kuna mtu karibu anamwangalia; alipoona hakuna mtu akainuka na kuondoka zake. Kwa hiyo umwonapo mtu akipiga kelele kama wapunga pepo wafanyavyo mtazame kwa macho ya rohoni kwani wengine hujifanyisha na unapokemea kelele zao unatumia nguvu za Mungu vibaya.
Ila pia unapoona kama vita ni ngumu kwako kumbuka vita si yako bali ni ya Mungu, (2 Mambo Ya Nyakati 20:14-15) kwa hiyo yakupasa upigane kwa imani!
Ninamwomba Mungu akusaidie kufanikiwa kwa hili katika Jina la Yesu Kristo!

No comments:

Post a Comment

NENO NI UZIMA Designed by 5gear Copyright © 2014-2015

Theme images by Jason Morrow. Powered by Blogger.