Vichwa vya Habari

Unaweza Kupata Wapi Amani ya Akili?

Unaweza Kupata Wapi Amani ya Akili?
Kuna tofauti nyingi kati ya wakati wetu na wakati wa Thoreau, aliyetajwa katika makala iliyotangulia. Tofauti moja kubwa ni kwamba leo kuna ushauri kemkemu juu ya kupata amani ya akili. Wanasaikolojia na waandishi wa vitabu vya kujisaidia—hata waandishi wa magazeti—hutoa maoni yao. Huenda ushauri wao ukasaidia kwa muda mfupi; lakini jambo kubwa zaidi linahitajiwa ili kupata masuluhisho ya kudumu. Watu waliotajwa katika makala iliyotangulia walitambua hivyo.
MALEZI na matatizo ya Antônio, Marcos, Gerson, Vania, na Marcelo yalikuwa tofauti. Lakini walikuwa na mambo matatu yanayofanana. Kwanza, kuna wakati ‘walipokuwa hawana tumaini na walikuwa bila Mungu katika ulimwengu.’ (Waefeso 2:12) Pili, walitamani sana amani ya akili. Na tatu, wote walipata amani ya akili waliyotaka baada ya kukubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Walipofanya maendeleo, walikuja kutambua kwamba Mungu anawapenda. Kwa kweli, kama Paulo alivyowaambia Waathene wa wakati wake, Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Kuamini jambo hilo kwa moyo ni muhimu ili kupata amani ya akili.
Kwa Nini Hakuna Amani?
Biblia hutoa sababu mbili za msingi zinazofanya kusiwe na amani ulimwenguni—iwe amani ya akili au amani kati ya watu. Sababu ya kwanza inaelezwa kwenye Yeremia 10:23: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Mwanadamu hana hekima wala busara ya kujitawala bila msaada, na msaada pekee ulio na manufaa ya kweli hutoka kwa Mungu. Wanadamu wasiofuata mwongozo wa Mungu hawatapata kamwe amani yenye kudumu. Sababu ya pili inayofanya kusiwe na amani imetajwa na mtume Yohana: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Bila mwongozo wa Mungu, jitihada za mwanadamu za kupata amani zitazuiwa sikuzote na utendaji wa yule “mwovu,” Shetani, ambaye ni mtu halisi—mwenye nguvu sana—ingawa haonekani.
Kwa sababu hizo mbili—kwamba watu wengi hawatafuti mwongozo wa Mungu na kwamba Shetani ni mwenye utendaji mwingi ulimwenguni—jamii yote ya kibinadamu iko katika hali mbaya sana. Mtume Paulo aliifafanua hali hiyo vema: “Viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.” (Waroma 8:22) Ni nani asiyekubaliana na maoni hayo? Katika nchi tajiri na vilevile nchi maskini, matatizo ya familia, uhalifu, ukosefu wa haki, mahitilafiano ya nyutu, shaka za kiuchumi, chuki za kikabila, uonevu, magonjwa, na kadhalika, hunyima watu amani ya akili.
Mahali pa Kupata Amani ya Akili
Wakati Antônio, Marcos, Gerson, Vania, na Marcelo walipochunguza Neno la Mungu, Biblia, walijifunza mambo yaliyobadili maisha yao. Jambo moja walilojifunza ni kwamba hali ya ulimwengu itabadilika wakati mmoja. Hilo si tumaini tu lenye shaka kwamba mambo yatakuwa mazuri mwishowe. Ni tumaini hakika, lenye msingi mzuri kwamba Mungu ana kusudi fulani kwa wanadamu na kwamba hata sasa tunaweza kunufaika na kusudi hilo tukifanya mapenzi yake. Walitumia maishani mwao yale waliyojifunza katika Biblia, na hali yao ikawa bora. Walipata furaha na amani nyingi zaidi kuliko walivyotazamia.
Antônio sasa hashiriki katika mateto wala mizozo ya wafanyakazi. Anajua kwamba mabadiliko yanayotokana na kufanya hivyo ni machache na ya muda mfupi tu. Kiongozi huyu wa zamani wa wafanyakazi amejifunza juu ya Ufalme wa Mungu. Mamilioni wengi huomba Ufalme huo wanapokariri Sala ya Bwana (au, sala ya Baba Yetu) na kumwambia Mungu hivi: “Ufalme wako uje.” (Mathayo 6:10aZaire Swahili Bible) Antônio alijifunza kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi ya mbinguni ambayo itawaletea wanadamu amani ya kweli.
Marcos alijifunza kutumia ushauri wa Biblia wenye hekima kuhusu ndoa. Hivyo, sasa mwanasiasa huyu wa zamani amemrudia mkewe na wana furaha. Yeye pia anatazamia kwa hamu wakati ujao karibuni ambapo Ufalme wa Mungu utaondoa mfumo huu wa ulimwengu wenye pupa na ubinafsi na kuleta ulimwengu bora. Yeye anaelewa vizuri sana ule mstari katika Sala ya Bwana usemao: “Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama mbinguni.” (Mathayo 6:10bZSB) Mapenzi ya Mungu yatakapofanywa duniani, wanadamu wataishi maisha ambayo hawajapata kamwe kuishi.
Namna gani Gerson? Yeye sasa hasafiri bila kusudi wala haibi. Maisha ya Gerson, ambaye zamani alikuwa mtoto mwenye kurandaranda mitaani, sasa yana maana kwa sababu yeye hutumia nguvu zake kuwasaidia wengine wapate amani ya akili. Kama vile mambo hayo yaliyoonwa yaonyeshavyo, kujifunza Biblia na kutumia yale isemayo kunaweza kubadili maisha ya mtu yawe bora.
Amani ya Akili Katika Ulimwengu Wenye Taabu
Yesu Kristo ndiye mhusika mkuu katika kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu, na watu hujifunza mengi sana kumhusu wanapojifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Usiku alipozaliwa, malaika walimwimbia Mungu sifa: “Utukufu katika mahali pa juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani miongoni mwa watu wa nia njema.” (Luka 2:14) Yesu alihangaikia kuboresha maisha ya watu alipokuwa mtu mzima. Alielewa hisia zao na kuwaonyesha huruma ya pekee wenye taabu na wagonjwa. Na, kama maneno ya malaika yaonyeshavyo, Yesu aliwaletea wapole kiasi fulani cha amani ya akili. Mwishoni mwa huduma yake, aliwaambia mitume wake hivi: “Mimi nawaachia nyinyi amani, nawapa amani yangu. Mimi siwapi nyinyi hiyo kwa njia ile ambayo ulimwengu huitoa. Msiache mioyo yenu itaabishwe wala msiiache ikunyatike kwa sababu ya hofu.”—Yohana 14:27.
Yesu hakuwa mfadhili tu. Alijilinganisha na mchungaji, na kuwalinganisha wafuasi wake wenye upole na kondoo aliposema: “Mimi nimekuja ili wapate kuwa na uhai na wapate kuwa nao kwa wingi. Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema hutoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.” (Yohana 10:10, 11) Naam, tofauti na viongozi wengi leo ambao hujihangaikia kwanza, Yesu alitoa uhai wake kwa ajili ya kondoo zake.
Tunaweza kunufaikaje na yale aliyofanya Yesu? Wengi wanafahamu maneno haya: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Kudhihirisha imani katika Yesu huhitaji, kwanza kabisa, tumjue yeye na kumjua Baba yake, Yehova. Kumjua Mungu na Yesu Kristo kunaweza kutokeza uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu ambao utatusaidia kupata amani ya akili.
Yesu alisema: “Kondoo wangu husikiliza sauti yangu, nami nawajua, nao wanifuata mimi. Nami nawapa hawa uhai udumuo milele, na hawataharibiwa kwa vyovyote, na hakuna atakayewanyakua mkononi mwangu.” (Yohana 10:27, 28) Ni maneno yenye shauku na yenye kufariji kama nini! Ni kweli kwamba Yesu alisema maneno hayo miaka ipatayo elfu mbili iliyopita, lakini yana maana ileile hata sasa. Usisahau kwamba Yesu Kristo bado yu hai na anatenda, anatawala sasa akiwa Mfalme aliyetawazwa wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu. Yeye bado anahangaikia wenye upole wanaotamani amani ya akili kama alivyofanya alipokuwa duniani miaka mingi iliyopita. Isitoshe, yeye bado ndiye Mchungaji wa kondoo zake. Tukimfuata, atatusaidia kupata amani ya akili, inayotia ndani matazamio hakika ya kupata amani kamili wakati ujao—amani bila jeuri, vita, na uhalifu.
Manufaa za kweli hutokana na kujua na kuamini kwamba Yehova atatusaidia kupitia Yesu. Je, unamkumbuka Vania, ambaye aliachiwa madaraka makubwa akiwa msichana mdogo na kufikiri kwamba Mungu amemwacha? Sasa Vania anajua kwamba Mungu hakumwacha. Yeye asema: “Nilijifunza kwamba Mungu ni mtu halisi mwenye sifa zenye kupendeza. Upendo wake ulimsukuma amtume Mwana wake duniani ili atupatie uhai. Ni muhimu sana kujua jambo hilo.”
Marcelo asema kwamba uhusiano wake na Mungu ni halisi. Marcelo, ambaye zamani alikuwa mwenda-karamuni, aeleza: “Mara nyingi vijana hawajui wafanye nini, na mwishowe hujiumiza tu. Baadhi yao huanza kutumia dawa za kulevya, kama nilivyofanya. Natumaini kwamba vijana wengi zaidi watabarikiwa kama mimi, kwa kujifunza kweli juu ya Mungu na Mwana wake.”
Kupitia funzo la makini la Biblia, Vania na Marcelo walisitawisha imani yenye nguvu katika Mungu na uhakika katika utayari wake wa kuwasaidia kutatua matatizo. Tukifanya vile walivyofanya—kujifunza Biblia na kutumia yale isemayo—sisi pia tutapata amani nyingi sana ya akili. Kisha kitia-moyo hiki cha mtume Paulo kitatufaa kwelikweli: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.
Kupata Amani ya Kweli Leo
Yesu Kristo anawaelekeza wanaotaka kuijua kweli kwenye njia ya uhai udumuo milele katika paradiso ya kidunia. Anapowaongoza kwenye ibada safi ya Mungu, wanapata amani kama ile inayofafanuliwa katika Biblia: “Watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.” (Isaya 32:18) Na huo ni mwonjo tu wa kimbele wa amani watakayopata wakati ujao. Tunasoma hivi: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:11, 29.
Hivyo, je, tunaweza kuwa na amani ya akili leo? Ndiyo. Isitoshe, tunaweza kuwa na hakika kwamba karibuni, Mungu atawabariki wanadamu watiifu kwa amani nyingi kuliko wakati mwingineo wowote. Basi, kwa nini usimwombe kupitia sala akupe amani yake? Ikiwa una matatizo yanayokunyima amani, sali kama alivyosali Mfalme Daudi: “Katika shida za moyo wangu unifanyie nafasi, na kunitoa katika dhiki zangu. Utazame teso langu na taabu yangu; unisamehe dhambi zangu zote.” (Zaburi 25:17, 18) Uwe na hakika kwamba Mungu husikiliza sala za aina hiyo. Yeye hunyosha mkono wake na kuwapa amani wale wote wanaoitafuta kwa unyofu wa moyo. Tunahakikishiwa kwa upendo hivi: “BWANA yu karibu na wote wamwitao, wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.”—Zaburi 145:18, 19.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Mwanadamu hana hekima wala busara ya kujitawala bila msaada, na msaada pekee ulio na manufaa ya kweli hutoka kwa Mungu
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Kumjua Mungu na Yesu Kristo kunaweza kutokeza uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu ambao utatusaidia kupata amani ya akili
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kufuata ushauri wa Biblia husaidia kuwa na maisha ya familia yenye amani

No comments:

Post a Comment

NENO NI UZIMA Designed by 5gear Copyright © 2014-2015

Theme images by Jason Morrow. Powered by Blogger.