Vichwa vya Habari

Unaweza Kupata Amani Katika Ulimwengu?

e, Unaweza Kupata Amani Katika Ulimwengu Huu Wenye Misukosuko?
JE, UNAISHI kwa amani? Kwa watu wengi, jibu lililo wazi ni hapana. Wanaishi katika maeneo yenye vita, misukosuko ya kisiasa, jeuri ya kikabila, au ugaidi. Hata ikiwa hupatwi na misiba hiyo, amani yako inaweza kuvurugwa na uhalifu, mateso, na ugomvi kutoka kwa wafanyabiashara wenzako au majirani. Pia, katika familia nyingi mara nyingi watu wanapigana badala ya kuwa na amani.
Watu wengi wanatamani sana kuwa na amani ya moyoni. Huenda wakatafuta amani hiyo katika dini, madarasa yanayowafundisha watu kutafakari, au vikundi vya mazoezi ya yoga. Wengine wanatumaini kupata amani kwa kuchukua likizo, kupanda milima, kusafiri katika maeneo ya nyika au jangwa, au kutembelea maeneo ambayo yana chemchemi za maji moto. Hata ingawa inaonekana kwamba watu fulani wanaotafuta amani ya moyoni wanapata amani ya kadiri fulani, huenda wakatambua haraka kwamba amani kama hiyo ni ya juujuu tu na ya muda mfupi.
Hivyo basi, unaweza kupata wapi amani ya kweli? Muumba wetu, Yehova Mungu ndiye chanzo cha amani. Kwa nini? Yeye ni “Mungu anayetoa amani.” (Waroma 15:33) Chini ya utawala wa Ufalme wake ambao unakaribia, kutakuwa na “wingi wa amani.” (Zaburi 72:7; Mathayo 6:9, 10) Hiyo ni amani bora zaidi kuliko amani yoyote ile inayopatikana kutokana na mapatano ya wanadamu. Mara nyingi, mapatano hayo yanakomesha uadui kwa muda mfupi tu. Lakini amani ya Mungu itaondoa mambo yote yanayosababisha vita na ugomvi. Kwa kweli, hakuna mtu atakayejifunza vita tena. (Zaburi 46:8, 9) Mwishowe, sote tutafurahia amani ya kweli!
Ingawa tumaini hilo ni zuri ajabu, huenda ukatamani kupata amani ya kadiri hata sasa. Je, kuna njia ya kupata amani ya moyoni ambayo inaweza kukusaidia katika nyakati hizi zenye misukosuko? Inapendeza kujua kwamba Biblia inatuonyesha jinsi ya kupata amani hiyo. Chunguza miongozo fulani katika sura ya 4 ya barua ya mtume Paulo kwa Wafilipi. Tunakuomba usome mstari wa 4 mpaka wa 13 katika Biblia yako mwenyewe.
“Amani ya Mungu”
Tunasoma hivi kwenye mstari wa 7: “Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Amani hiyo haiji kwa kutafakari tu au kwa kujaribu kuboresha utu wetu. Badala yake, ni amani inayotoka kwa Mungu. Amani hiyo ni yenye nguvu sana hivi kwamba ‘ina ubora unaozidi fikira zote.’ Bila shaka, inazidi mahangaiko yetu yote, ujuzi, na fikira zetu. Huenda tukahisi kwamba hatuwezi kushinda matatizo yetu, lakini amani ya Mungu inaweza kutujaza tumaini linalotegemea Biblia la kwamba siku moja matatizo yetu yote yatakwisha.
Je, ni jambo lisilowezekana? Kwa wanadamu haliwezekani; lakini “mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:27) Imani na kumtegemea Mungu kunatusaidia kutohangaika kupita kiasi. Mfikirie mtoto mdogo ambaye amepotea ndani ya duka kubwa. Anajua kwa hakika kwamba kile anachohitaji kufanya tu ni kumpata Mama yake na mambo yote yatakuwa shwari tena. Kama mtoto huyo anavyobebwa anapopatikana, tunaweza pia kuwa na hakika kwamba Mungu atatubeba mikononi mwake kwa njia ya mfano. Atatutuliza na mwishowe ataondoa kabisa mahangaiko yetu yote.
Waabudu wengi wa Yehova wamepata amani ya Mungu wakati wa majaribu makali zaidi. Kwa mfano, fikiria kisa cha Nadine, ambaye alizaa mtoto aliyekufa. Anaeleza: “Ninaliona kuwa jambo gumu kuzungumza kuhusu hisia zangu, na sikuzote ninajaribu kujifanya ili ionekane kwamba hali hiyo hainisumbui. Lakini kwa ndani, nilikuwa nimevunjika moyo. Karibu kila siku, nilimwaga moyo wangu kwa Yehova katika sala na kumsihi anisaidie. Nimehisi nguvu za sala, kwa kuwa wakati wowote niliposhuka moyo na kujiambia hivi: ‘Siwezi kuvumilia tena,’ nilipata utulivu na amani ya moyoni. Nilijihisi nikiwa salama salimini.”
Inalinda Moyo na Akili Yako
Na turudi tena kwenye andiko la Wafilipi 4:7. Linasema kwamba amani ya Mungu italinda mioyo na nguvu zetu za akili. Kama vile tu askari anavyolinda kituo chake, amani ya Mungu inalinda moyo wetu, ili mawazo ya kujirundikia vitu vya kimwili, mahangaiko yasiyo ya lazima, na maadili mapotovu yasiingie katika akili na moyo wetu. Fikiria mfano mmoja.
Watu wengi katika ulimwengu huu wenye misukosuko wanaamini kwamba ili wawe wenye furaha na salama, wanahitaji kuwa na pesa au mali nyingi. Kwa kufuata mashauri ya wataalamu, huenda wakanunua hisa ili wahifadhi kiasi fulani cha pesa zao. Je, kweli wanajihisi wakiwa na amani? Si lazima. Huenda wakachunguza hali kila siku wakiwa na wasiwasi kuhusu thamani ya hisa zao, huku wakijiuliza ikiwa wauze, wanunue, au wabaki na hisa hizo. Huenda pia wakawa na wasiwasi bei ya hisa inaposhuka. Bila shaka, Biblia haimkatazi mtu kuwekeza katika biashara, lakini inatoa shauri hili zuri: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili. Usingizi wa mtumishi ni mtamu, bila kujali kama anakula kidogo au kingi; lakini wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.”—Mhubiri 5:10, 12.
Andiko la Wafilipi 4:7 linamalizia kwa kusema kwamba amani ya Mungu inalinda mioyo yetu na nguvu za akili “kwa njia ya Kristo Yesu.” Kuna uhusiano gani kati ya Kristo Yesu na amani ya Mungu? Yesu anatimiza sehemu ya maana sana katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Yesu alitoa uhai wake ili tuweze kukombolewa kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. (Yohana 3:16) Pia, yeye ndiye aliyewekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Hivyo, kujua daraka ambalo Yesu anatimiza kunaweza kuchangia sana amani yetu ya akili na moyo. Jinsi gani?
Tukitubu kikweli dhambi zetu na kuomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, Mungu atatusamehe, na hilo litatusaidia kuwa na amani ya akili na moyo. (Matendo 3:19) Tunapotambua kwamba hatuwezi kufurahia maisha kikamili mpaka Ufalme wa Kristo utakapokuja, tunaepuka kuishi bila kujali kana kwamba hatuna tumaini la kuishi wakati ujao. (1 Timotheo 6:19) Bila shaka, sisi pia tunapatwa na matatizo, lakini tunaweza kufarijiwa na tumaini hakika la kwamba hivi karibuni tutakuwa na maisha bora zaidi.
Jinsi Unavyoweza Kupata Amani ya Mungu
Hivyo basi, unaweza kupata jinsi gani amani ya Mungu? Tunapata madokezo fulani kwenye Wafilipi 4:4, 5, tunaposoma hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana. Mara nyingine tena nitasema, Shangilieni! Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote. Bwana yuko karibu.” Paulo alipoandika maneno hayo, alikuwa amefungwa gerezani isivyo haki huko Roma. (Wafilipi 1:13) Badala ya kulalamika kwa sababu ya kutendewa isivyo haki, aliwatia moyo waamini wenzake washangilie sikuzote katika Bwana. Ni wazi kwamba shangwe yake haikutegemea hali zake, bali ilitegemea uhusiano wake pamoja na Mungu. Sisi pia tunahitaji kujifunza kufurahia kumtumikia Mungu hata hali zetu ziwe namna gani. Kadiri tunavyomjua Yehova vizuri zaidi na kufanya mapenzi yake kikamili, ndivyo tutakavyofurahia kumtumikia. Kufanya hivyo, kutatuletea uradhi na amani ya moyoni.
Zaidi ya hayo, tunatiwa moyo kuwa wenye usawaziko. Tukisitawisha sifa ya usawaziko, hatutatazamia kutimiza mambo mengi zaidi ya uwezo wetu. Tunajua kwamba sisi si wakamilifu; hatuwezi kuwa bora kabisa katika kila jambo. Kwa hiyo, kwa nini tujisumbue tukifikiria jinsi ya kuwa wakamilifu au, angalau, kuwa bora kuliko watu wengine wote? Pia, hatutatazamia wengine wawe wakamilifu. Hivyo, wengine wanapofanya jambo ambalo linatukasirisha tunaweza kubaki watulivu. Tafsiri nyingine ya neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “usawaziko” ni “kukubaliana na-.” Ikiwa tuko tayari kukubaliana na mtu fulani katika mapendezi ya kibinafsi, tutaepuka ugomvi, ambao mara nyingi hauna faida yoyote bali unaharibu kwa muda amani pamoja na wengine na pia amani yetu ya moyoni.
Maneno yafuatayo kwenye Wafilipi 4:5, “Bwana yuko karibu,” huenda yakaonekana hayapatani na mistari mingine. Hivi karibuni Mungu atabadili ulimwengu huu wa kale na kuleta ulimwengu mpya chini ya Ufalme wake. Lakini hata sasa anaweza kuwa karibu na kila mtu anayemkaribia. (Matendo 17:27; Yakobo 4:8) Kutambua kwamba Bwana yuko karibu kunatusaidia kushangilia, kuwa wenye usawaziko, na kutokuwa na mahangaiko kuhusu matatizo ya leo au ya wakati ujao, kama mstari wa 6 unavyoonyesha.
Tunapochunguza mstari wa 6 na wa 7, tunatambua kwamba amani ya Mungu inahusiana moja kwa moja na sala. Watu fulani wanaona sala kuwa tu aina fulani ya kutafakari, wakifikiri kwamba kila aina ya sala inaweza kuongeza utulivu wao wa moyoni. Hata hivyo, Biblia inasema kuhusu mawasiliano ya unyoofu pamoja na Yehova, yaani, mawasiliano ya karibu kama ya mtoto anayemweleza mzazi mwenye upendo shangwe na wasiwasi wake. Inatia moyo kama nini kujua kwamba tunaweza kumkaribia Mungu “katika mambo yote.” Hata iwe tuna mawazo gani ndani kabisa ya akili au mioyo yetu, tunaweza kuyafunua kwa Baba yetu wa mbinguni.
Mstari wa 8 unatutia moyo tukazie akili mawazo mazuri. Hata hivyo, haitoshi tu kufikiria mambo mazuri. Kama mstari wa 9 unavyoeleza, tunapaswa pia kufuata mashauri mazuri ya Biblia. Kufanya hivyo kutatuwezesha kuwa na dhamiri safi. Methali hii ni ya kweli kabisa: Dhamiri nzuri ni mto laini wa kulalia!
Ndiyo, unaweza kupata amani ya moyoni. Inatoka kwa Yehova Mungu, ambaye anawapa wale wanaomkaribia na wanaotaka kufuata mwongozo wake. Ukichunguza Neno lake, Biblia, unaweza kujua vizuri mawazo yake. Hata hivyo, si jambo rahisi kufuata miongozo yake. Lakini jitihada hizo zote si za bure kwa sababu ‘Mungu wa amani atakuwa pamoja nawe.’—Wafilipi 4:9.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
“Amani ya Mungu . . . itailinda mioyo yenu.”—WAFILIPI 4:7

No comments:

Post a Comment

NENO NI UZIMA Designed by 5gear Copyright © 2014-2015

Theme images by Jason Morrow. Powered by Blogger.